- Kwa mujibu wa taarifa ya Guinness World Records iliyochapishwa kwenye tovuti yake Januari 26 mwaka 2026, rekodi ya muda mrefu zaidi ya kukumbatia mti mfululizo ni saa 72, iliyofikiwa na Truphena Muthoni (Kenya).
- Mafanikio haya ya saa 72 yamevuka rekodi yake ya awali aliyoiweka mnamo Februari mwaka 2025, alipokumbatia mti kwa saa 48 katika Bustani ya Kumbukumbu ya Michuki, jijini Nairobi.
- Siku chache kabla ya tangazo hili la pili rasmi la Guinness World Records, Truphena alitajwa na Timely Kenya kuwa miongoni mwa wanawake mashuhuri nchini Kenya wanaobadilisha maisha ya Wakenya kwa namna mbalimbali.
- Ili kudumisha mabadiliko hayo, Truphena amekuwa mstari wa mbele kuhamasisha kizazi cha vijana nchini Kenya kushiriki katika upandaji miti.
Mwanaharakati chipukizi wa mazingira, Truphena Muthoni, ameweka historia tena kwa kuingia katika Kitabu cha Rekodi cha Guinness kwa mara ya pili, baada ya kukumbatia mti kwa saa 72 mfululizo kama njia ya “maandamano ya kimya kimya’’ kupinga uharibifu wa misitu ya asili.
Kwa mujibu wa taarifa ya Guinness World Records iliyochapishwa kwenye tovuti yake Januari 26 mwaka 2026, rekodi ya muda mrefu zaidi ya kukumbatia mti mfululizo ni saa 72, iliyofikiwa na Truphena Muthoni (Kenya) jijini Nairobi, Kenya, kuanzia Desemba 8 hadi 11 mwaka 2025.
Katika maelezo yake kwa Guinness World Records, Truphena alisema aliamua kufanya jaribio hilo “ili kupaza sauti kutetea ulinzi wa miti ya asili pamoja na kuheshimu hekima ya jamii za asili, ambazo mifumo yake ya maarifa inaendelea kuwa nguzo muhimu katika kutafuta suluhisho za kimataifa za mabadiliko ya tabianchi.”
Mafanikio haya ya saa 72, akiwa katika Kaunti ya Nyeri, yamevuka rekodi yake ya awali aliyoiweka mnamo Februari mwaka 2025, alipokumbatia mti kwa saa 48 katika Bustani ya Kumbukumbu ya Michuki, jijini Nairobi. Rekodi hiyo ya awali pia ilitambuliwa rasmi na Guinness World Records mwezi Desemba mwaka 2025.
Akiwa na dhamira thabiti ya kuonyesha kile kilicho ndani ya uwezo wake kwa dunia nzima, Truphena hakula, hakulala wala hakuachilia shina la mti hadi alipotimiza lengo lake. Katika matukio yote mawili, alizungukwa na wahudumu wa afya pamoja na wananchi waliokuwa wakifuatilia tukio hilo.

“Kitendo hiki ni zaidi ya kuweka rekodi,” alisikika akisema katika video aliyojirekodi wakati akiendelea kuukumbatia mti wa mwerezi (cedar) mjini Nyeri, chini ya Mlima Kenya. “Huu ni wito wa kulinda misitu ya asili, kuponya akili zilizoathirika na kutukumbusha kwamba kupotea kwa misitu ni sawa na kupotea kwa sehemu ya nafsi zetu,” alisema katika video hiyo.
Siku chache kabla ya tangazo hili la pili rasmi la Guinness World Records, Truphena alitajwa na Timely Kenya kuwa miongoni mwa wanawake mashuhuri nchini Kenya wanaobadilisha maisha ya Wakenya kwa namna mbalimbali. Alitambuliwa pamoja na viongozi wanawake katika sekta za utawala, afya, siasa na mazingira, akiwemo seneta na gavana.
Akizungumza kuhusu heshima hiyo, Truphena alisema: “Ninamshukuru Mungu kwa kuniamini na kunikabidhi jukumu hili takatifu. Ninatoa maisha yangu na kazi yangu kwake. Mbele ya wananchi wa Kenya na mbele ya mataifa mengine duniani, najitoa kuwa chombo cha uponyaji kwa ulimwengu.”
Baada ya tangazo la pili la Guinness World Records, Truphena alitembelea ofisi ya Gavana wa Kaunti ya Nyeri, Mutahi Kahiga, ambako alipokelewa na kupongezwa rasmi. Ni katika eneo la ofisi hiyo ndipo Truphena alipokumbatia mti kwa muda wa saa 72 mfululizo.
“Tulifanikisha kwa msaada wa Mungu. Nimeshika rekodi ya dunia mara mbili,” aliandika kwenye ukurasa wake wa Facebook saa chache baada ya kutangazwa rasmi kwa rekodi hiyo.
Mwanaharakati huyo kijana amewahamasisha watu wengi nchini Kenya, huku baadhi yao wakianza kukumbatia miti kwa muda mrefu zaidi kwa sababu mbalimbali.
Katika mji wa Nanyuki, mwanamume mwenye umri wa miaka 43, Paul Kago alikumbatia mti wa mwerezi kwa saa 96 kama njia ya kuhamasisha amani kuelekea uchaguzi mkuu wa Kenya wa mwaka 2027. Alifanya hivyo kufuatia mvutano wa kisiasa katika siku za hivi karibuni.

James Irungu kutoka Murang’a, nchini Kenya, hakufanikiwa kutimiza azma yake ya kukumbatia mti kwa saa 80 baada ya kuugua saa moja tu kabla ya kufikia lengo lake. Lengo lake lilikuwa ni kuongeza uelewa kuhusu ugonjwa wa saratani na kuitaka Serikali kuuchukulia ugonjwa huo kama tishio kubwa kwa afya ya jamii. Mnamo Januari 6, Truphena aliungana naye kama ishara ya mshikamano, wakapiga picha za pamoja.
Hata hivyo, mitandao ya kijamii haikuwa na huruma kwake. “Wanaume wa kweli wanapaswa kukumbatia transfoma za umeme, nungu, simba na chatu…” aliandika mmoja wa watumiaji wa Facebook baada ya Truphena kuchapisha picha hiyo. Mwingine alijibu akisema: “Hatuingii kwenye mashindano; tunalia kwa sauti. Sio rekodi inayohesabika, bali ujumbe! Ninaupenda mshikamano huu.”
Tukio jingine la kukumbatia mti lililodumu kwa saa 50, lilifanywa na Stephen Gachanja, mtoto wa miaka 14, katika Bustani ya Jevanjee jijini Nairobi, akiwa na lengo la kuchangisha fedha ili kumsaidia kaka yake kulipia upasuaji muhimu wa kiafya.

Mwelekeo huu wa kukumbatia miti uliibua hisia tofauti kutoka kwa watu mbalimbali, baadhi wakionyesha kuvutiwa na wengine kutilia shaka harakati hizo. Hata hivyo, tukio la mtoto mmoja lilimgusa sana Truphena, hali iliyomfanya aungane naye, wapige picha ya pamoja na kuichapisha akiwa na ujumbe: “Kabla mtoto hajaamini kwa sababu yako, kazi bado haijakamilika.”
Maandamano yake ya kimya kimya yaliyoibua mjadala wa masuala ya mazingira katika mazungumzo ya kila siku hayakulenga tu kuokoa miti ya asili, bali pia yalilenga kutetea afya ya akili na kuhamasisha jamii kuhusu manufaa ya kisaikolojia ya kutumia muda katika mazingira ya asili.
Ili kudumisha mabadiliko hayo, Truphena amekuwa mstari wa mbele kuhamasisha kizazi cha vijana nchini Kenya kushiriki katika upandaji miti. Anashirikiana na Shirika la Huduma za Misitu Kenya (Kenya Forest Service) katika juhudi za kufufua hifadhi ya misitu, huku akifurahia uteuzi wake kama balozi kwenye mpango wa Serikali ya Kenya wa kupanda miti bilioni 15 ifikapo mwaka 2032.
Kupitia jukumu hilo, analenga kuongeza mafanikio ya mpango huo kwa kuwahusisha vijana katika upandaji miti, urejeshaji wa mazingira na elimu ya mazingira.
Picha ya bango: Truphena Muthoni katika ofisi ya Gavana wa Nyeri, Mutahi Kahiga, muda mfupi baada ya Guinness World Records kutambua changamoto yake ya kukumbatia mti kwa saa 72 aliyofanikisha mwishoni mwa mwaka 2025. Picha kwa hisani ya ukurasa wa Facebook wa Truphena.