- Mito iliyotegemea barafu ya Mlima Kenya sasa imesalia miteremko tu, na baadhi ya mito mingine ikakauka kabisa, ikihatarisha usalama wa maji na shughuli za kilimo na ufugaji wa samaki.
- Wakulima na wafugaji wanakabiliwa na ukame, huku baadhi yao wakisogea hadi nyanda za juu ili kufuata maji na hali bora ya kukuza samaki aina ya trout.
- Kupungua kwa barafu kunadhoofisha usambazaji wa maji, kunapunguza usalama wa mifumo ya maji ya kanda, na kuathiri uzalishaji wa umeme kutoka Mto Tana, ambao hutoa asilimia 70 ya umeme nchini Kenya.
- Jamii karibu na Mlima Kenya wameshughulika uhifadhi wa misitu, kupanda miti, kuanzisha muungano wa watumiaji wa maji, na kutumia kilimo himilivu.
Hii ni nakala ya pili katika Mfululizo wa Mongabay – Kinachotokea mlimani hakisalii mlimani. Soma nakala ya kwanza hapa.
Kumbukumbu za maisha ya utotoni za Gerald Ngatia, afisa mstaafu wa misitu, mwenye umri wa miaka 74, zimemwezesha kusimulia jinsi hapo awali Mto Sagana ungeweza kumbeba tembo na kumpelekea nyanda za chini.
“Leo hata panya anaweza kuuvuka mto. Wakati mwingine tunafanya mikutano ya uhifadhi huku tukikalia mawe katikati ya mto uliokauka kati ya mwezi wa Septemba na mwezi Oktoba, wakati mtiririko wake wa kimazingira uko chini sana,” Ngatia, ambaye ameishi pembezoni mwa Msitu wa Hombe katika Mpango wa Makazi ya Sagana tangu utotoni, aliielezea Mongabay.


Hata hivyo, Mto Sagana sio pekee ulioko kwenye mfumo tata wa ikolojia ya Mlima Kenya, ambao viwango vyake vya maji vimepungua mara kadhaa. Mito Rigati na Thegu, ambayo hupokea maji yao kutoka Mlima Kenya na katika hatua mbalimbali kuungana na Mto Sagana, pia inajikakamua.
Juu zaidi ya nyanda za juu za Laikipia, Mongabay ilipata mito mingine mikavu. Wafugaji wa mbuzi walikaa juu ya mawe yaliyopogwa kwa maji huku mifugo wao wakijaribu kunywa maji kutoka kwenye vidimbwi madogo yenye harufu kwenye mito hiyo mikavu.
Ruth Waithera, anayeishi karibu na Mto Nanyuki, anahadithia kwamba alilazimika kufua nguo katika kile alikitaja kama kijimto cha msimu wakati mabomba ya maji yalikua yamekauka.


“Unaweza kuwa unafua nguo katikati ya mto, wakati ghafla unapigwa na harufu mbaya ilio kali mno, kisha ikifuatiwa na kinyesi kutoka katika makazi duni yalioko karibu. Maji hayo hayatumiki tena,” Waithera aliiambia Mongabay.
Mto Naro Moru nao unakabwa kutokana na kupotea kwa barafu kwenye Mlima Kenya na uchafuzi wa mazingira. Mlima wa jaa la takataka ulioko mita chache kutoka kwa mto huo unaachilia vichafuzi vilivyonaswa na mizizi iliyokunjana ya miti ya mierezi inayoonekana waziwazi katikati ya mto. Wakati mvua inaponyesha, kinachosalia kutoka kwa jaa la takataka baada ya ng’ombe na watoto wa kuranda mitaani kuchakura, husombwa hadi mtoni.
Katika kijiji cha Kanyoni, karibu na kituo cha elimu cha William Holden, ilani ya kijani iliobandikwa kwenye mti inaonya: “Jamii isiyo na maji ni jamii isiyo na maisha.” Kibao hiki kiko karibu na daraja la Mto Likii, ambako uondoaji wa maji yake baridi kutoka Mlima Kenya huanza.
Barafu zinazotoweka zinadhoofisha imani
Kila siku ya Jumapili, Mchungaji Leonard Mwaeke wa kanisa la Kenya Assemblies of God huyachukua makundi ya waongofu katika Mto Naro Moru ili kuwabatiza. Mongabay ilikutana naye mtoni Jumapili moja mwezi Desemba, alipokuwa akifua kaptula aliyokuwa amevaa wakati akiwabatiza waongofu 38 waliotoka katika makanisa kadhaa yajulikanayo kwa pamoja kama Wilaya ya Samaria katika kaunti ya Laikipia nchini Kenya.

Mchungaji Leonard Mwaeke wa kanisa la Kenya Assemblies of God akiwa na waongofu katika Mto Naro Moru alipokwenda kuwabatiza. Picha na Amos Kareithi, Mongabay.
Alikuwa na wasiwasi: “Huu ndio mtiririko wa chini kabisa ambao nimeushuhudia. Watu wanauua mto huu. Kuna sehemu nyingi za uondoaji na uingizaji wa maji. Nakumbuka kati ya mwaka 1999 na 2008, Mto Naro Moru ulikuwa na maji mengi sana. Nashangaa kitachotokea kwa watu wa nyanda za chini ya mto huko Kaunti ya Samburu na kwingineko, ambao hutegemea maji haya tu.”
Ngatia pia ana wasiwasi kuhusu siku za usoni, licha ya kujitolea maisha yake yote ya utu uzima katika uhifadhi wa mazingira. Akiwa hakuzi miche kwenye kitalu cha miti cha Jamii ya Hombe, huwa yuko katika afisi yake mjini Nakuru au anazuru sehemu tofauti za Kenya akifuatilia na kuratibu shughuli za uhifadhi. Msimamizi huyu wa misitu aliyestaafu ni Mwenyekiti wa Muungano wa Kitaifa wa Mashirika ya Misitu ya Jamii (NACOFA), shirika la kitaifa linalojumuisha vyama 200 vya miungano ya misitu ya jamii.
Mhifadhi aliyefadhaika
Wakati wa mahojiano yetu karibu na Msitu wa Hombe, Ngatia alionekana amefadhaika na kina cha Mto Sagana. Cha kushangaza ni kwamba mhifadhi huyo alilelewa katika ardhi yenye ukubwa wa ekari 2.4228 iliogawiwa babake pamoja na wanafamilia wengine 169 wakati serikali ya Kenya ilipoitenga ardhi hio kutoka Msitu wa Hombe katika Hifadhi ya Misitu ya Mlima Kenya ili kubuni Mpango wa Makazi wa Sagana mwaka 1962.
Baada ya Kenya kujinyakulia uhuru, kulikuwa na majaribio ya serikali na watu wenye ushawishi mkubwa kunyakua sehemu kubwa ya misitu ili kuibadilisha na kuwa mashamba katika miaka ya 1980 na 1990.
Jaribio kuu la ujasiri lilifanywa mnamo mwaka 2001 wakati serikali ilipotangaza nia yake ya kutenga hekta 167,000 za ardhi ya misitu kutoka kwenye Mlima Kenya. Maendeleo hayo yalisababisha hisia kali kutoka kwa umma, zilizompa motisha Profesa Wangari Maathai na vuguvugu lake la Greenbelt Movement kuanzisha kampeni iliookoa hekta 1,825.12 za ardhi zilizopaswa kutengwa kutoka kwenye misitu ya Mlima Kenya.
Upandaji upya wa miti na kampeni ya demokrasia ilichangia uteuzi wa Wangari Maathai kwa Tuzo ya Amani ya Nobel mwaka wa 2004 “kwa kuwazia kimataifa na kutenda mashinani”. Vikundi vingine zaidi pia vilipinga jaribio kama hilo.
Wasemavyo wasomi
Katika utafiti wake wa mwaka 2006, ulioitwa “Common Heritage, Diverse Interests: Deforestation and Conservation Alternatives for Mount Kenya (Urithi wa Pamoja, Maslahi Tofauti: Ukataji Miti na Njia Mbadala za Uhifadhi Mlima Kenya)” Joseph Kariuki aliangazia majaribio kadhaa ya kunyakua na kurejesha misitu.
Juhudi za kuutunza Mlima Kenya zilianza mwaka 1934, wakati ulipofanywa hifadhi ya kitaifa kwa mara ya kwanza, na zikafikia kilele mwaka 1949 wakati ilipopandishwa hadhi na kuwa mbuga ya kitaifa, na kupelekea kutambuliwa kwake na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) mwaka 1978 kama hifadhi ambayo uhai waweza kuwepo, chini ya mpango wa Binadamu na Bayosfia.
Utafiti wa mwaka 2019 uliofanywa na shirika la Nature Kenya ukishirikiana na Darwin Initiative, ulionyesha kuwa ingawa sehemu ilioko chini ya msitu kwenye Mbuga ya kitaifa ya Mlima Kenya na hifadhi ya Msitu wa Mlima Kenya kwa pamoja una ukubwa wa hekta 277,525, mwavuli wake ukipungua kwa kiasi kikubwa kutokana na ukataji miti kiholela, malisho kwa mifugo, matukio ya moto misituni na mabadiliko ya hali ya hewa.
Lakini ni ripoti hii ya pamoja iliyochapishwa mwaka 2018 inayoonyesha kiwango cha barafu kufifia juu ya kilele cha Mlima Kenya. Waandishi wanasema barafu ni muhimu, kwa sababu hufanya kazi kama kichujio cha mabadiliko ya hali ya hewa ya muda mfupi na ni viashiria muhimu vya mabadiliko ya tabianchi.

Watafiti hao waliwasilisha data inayoashiria namna tangu mwaka 1934 barafu ya Mlima Kenya imeshuhudia mabadiliko kadhaa. Kwa mujibu wa ripot hiyo, kati ya mwaka 1899 na 2004, idadi kamili ya maeneo 18 ya barafu kwenye Mlima Kenya ilipungua kutoka kilomita mraba 1.64 hadi 0.27.
Ripoti hiyo pia imesema: “Maeneo nane ya barafu yalitoweka, huku eneo kubwa zaidi la barafu la Lewis likinakili viwango vya juu kurudi miaka ya nyuma kati ya mwaka 1934 na 2010, kwani ilipoteza asilimia 90 ya ujazo wake wote.”
Kushuka kwa viwango hivyo kulitokana na angahewa kukauka na kusababisha mawingu machache, kunyesha kwa theluji na albedo (kipimo kinachoeleza kiasi cha mwanga (hasa mwanga wa jua) kinachoakisiwa na uso au kitu, badala ya kufyonzwa. Kwa mfano, uso wenye albedo kubwa , kama vile barafu au theluji nyeupe, huakisi mwanga mwingi, ilhali uso wenye albedo ndogo, kama vile ardhi yenye giza au bahari, hufyonza mwanga mwingi.
Tafiti hiyo inapendekeza kuangaziwa upya orodha ya kiwango cha barafu ya Mlima Kenya.
Simon Gitau, anayeishi pembezoni mwa Mlima Kenya, ameshuhudia mabadiliko ya idadi ya barafu kileleni kwa miaka 33 sasa. Gitau alihitimu kutoka Chuo kikuu cha Kenyatta mnamo mwaka 1993, kisha akajiunga na shirika la Huduma ya Wanyamapori ya Kenya (KWS) kama afisa mwokozi wa Milimani.
“Nimeona mabadiliko katika Mlima Kenya tangu nilipoukwea kwa mara ya kwanza mwaka 1993, na kufika kileleni. Kuna wakati nilikuwa nikiukwea mara moja kwa mwezi. Hewa ilikuwa baridi sana, safi na ya kuvutia, ikinisukuma kupanda mlima tena na tena. Lakini hii imekua ikibadilika awamu kwa awamu. Barafu zimepotea,” aliiambia Mongabay.
Gitau, ambaye baadae alipandishwa madaraka na kuwa msimamizi mkuu wa mlima huo, kisha baadae kustaafu mwaka 2025 kama Mkurugenzi Msaidizi wa KWS, anakumbukwa jinsi barafu ya Lewis katika kilele cha Lenana wakati mmoja kilichukua ukubwa wa kilomita mraba 3. Anasema: “Kila nilipoukwea, nilitembea kwenye barafu. Tangu wakati huo, kimepoteza asilimia 46 ya barafu hio.”
Alielezea Mongabay kuwa kuyeyuka kwa barafu ya Lewis kutakuwa na athari ya moja kwa moja katika Mto Naro Moru.

Chanzo cha kupunguka kwa viwango vya maji
Dkt. Andrew Wambua, mtafiti na mtaalamu wa mazingira, ambaye ni mwanzilishi mwenza wa shirika la Africa Voices Dialogue, alifafanulia Mongabay athari kupungua kwa barafu katika Mlima Kenya.
“Hasara hii sio mabadiliko tu katika mandhari bali ni jambo la msingi la mabadiliko kwenye mfumo wa minara ya maji nchini Kenya inayohatarisha uhai na uthabiti wa mfumo wa ikolojia. Hasara hio pia itadhohofisha mizani ya maji ya kanda hio,” alisema.
Aliongezea: “Wakati Mto Tana unapokea asilimia ndogo ya jumla ya ujazo wake kamili kutoka kwa kuyeyuka kwa barafu, barafu hizo huwa kama vidhibiti muhimu vya msimu wa kiangazi, ikiachilia maji wakati mvua ni chache. Bila barafu, mtiririko wa mto utakuwa ni wa msimu na usioaminika.”
Wambua anatabiri mustakabali wa baadae unaotawaliwa na migao ya umeme na gharama za juu za nishati kwa sababu viwango vya chini vya maji vitaathiri uzalishaji wa nguvu za umeme kingoni mwa Mto Tana. Mto huo unazalisha asilimia 70 ya umeme nchini Kenya. Aidha anatarajia kuwepo kwa uhaba wa chakula kutokana na uzalishaji wa chini katika miradi ya umwagiliaji kama ile ya Bura na Hola. “Hii inaweza kuwa chanzo cha migogoro itokanayo na maji,” alisema.
Kupungua kwa barafu katika Mlima Kenya ni kielelezo kwa kanda ya Afrika Mashariki kwa sababu huo upoteaji hupunguza athari ya baridi katika hali ya hewa ya mashinani, ikichochea kuongeza kasi ya kupotea kwa mimea (ikikadiriwa kufika asilimia 55 ifikapo mwaka 2040) na kukausha katika nyanda za mwinuko wa juu unaofanya kama vimezaji hewa kaa, mtaalamu alieleza.
Mongabay pia ilizungumza na Dkt. Isaac Kalua, Msimamizi mkuu wa Wakfu wa Green Africa, ambaye hivi karibuni aliteuliwa kuwa Mlezi wa Heshima (Honorary Warden) wa KWS chini ya kategoria ya heshima ya Nation Cadre. Hii ni moja ya tuzo za juu kabisa zinazotolewa kwa raia wanaoonesha ushawishi wa kipekee kitaifa na kujitolea kwa muda mrefu katika uhifadhi wa mazingira.
KKalua alisisitiza kuwa barafu za Mlima Kenya zina jukumu muhimu kwenye mfumo wa ikolojia unaojumuisha misitiu, ardhi oevu, chemichemi na maji ardhini.
Kwa mjibu wa Kalua, kupotea kwa barafu kunaashiria ukosefu wa uthabiti unaoongezeka: “Tunashuhudia misimu yenye joto zaidi la kiangazi, mvua hafifu, utiririshaji wa maji kwa kasi, mimomonyoko, na michanga mizito zaidi.”
Alisema barafu za milimani kama zile zilizoko kileleni mwa Mlima Kenya ni “adimu na zenye umuhimu kisayansi”, na kuwa kutoweka kwao kunamaanisha kupoteza viashiria muhimu vya hali ya hewa duniani ambavyo vinatuonyesha namna ongezeko la joto ulimwenguni linavyotokea.
Wawili hawa wanahofia kuwa athari za kupungua kwa barafu huenda zikazidisha gharama za kiuchumi hadi mamilioni ya dola katika kupotea kwa uzalishaji wa kilimo. Wazalishaji viwandani pia wanaweza kulazimika kutafuta njia mbadala za gharama ya juu zaidi za nishati.
Kenya pia inakodolea macho gharama za kijamii kwa sababu ya migogoro mikubwa zaidi baina ya wakulima na wafugaji wanaohangaika kutafuta maji, kama ilivyoshuhudiwa mwaka 2017.
Kalua anasema kupotea kwa barafu nyingi milimani kunapunguza utalii, huathiri usalama wa milima na kuongeza gharama za mda mrefu za kukabiliana na nyanda za chini za mto, kando na kutuma ujumbe mzito wa kimataifa kwamba iwapo barafu za milima mirefu barani Afrika zitafifia, basi athari zaidi za mabadiliko ya hali ya hewa zaja.
Kupunguza majanga zaidi
Jamii na mashirika yanajaribu kupunguza majanga zaidi. Pamoja na upandaji miti upya wa mnara wa mani wa Mlima Kenya, serikali ya Kenya ilizindua mpango madhubuti kupanda miti bilioni 15 ifikapo mwaka 2032. Serikali ya Kenya imetenga siku moja ya likizo ya kitaifa ya kupanda miti. Uvunaji maji pia umeimarishwa, huku tafiti zaidi zikihimiza hili ili kuhakikisha utegemeaji wa vyanzo vya jadi kwa matumizi ya nyumbani na kilimo unapunguzwa.
Wakulima pia wanatekeleza kilimo himilivu. Wambua anasema kiwango cha chini cha usumbufu wa udongo hutokea wanapofanya kilimo cha hifadhi na mda mwingine kusambaza unyunyizaji kwa njia ya matone ili kupunguza kupotea kwa maji katika unyunyizaji mimmea.

Hata hivyo, Wambua anasema kwa kuwa kuyeyuka barafu kwatokana na viwango vya joto ulimwenguni, uongzi wa Kenya katika nishati mbadala ni mfano wa kuigwa. Anasema kupunguza shinikizo katika misitu ni muhimu, ila shinikizo la kimataifa sharti lidumishwe kwa mataifa yanayotema moshi mwingi kupunguza.
Kalua alisema: “Kenya pekee haiwezi kunusuru barafu ya Mlima Kenya. Dunia sharti ichukue hatua za haraka kupunguza utoaji wa hewa chafu ulimwenguni.”
Alisisitiza uhifadhi wa mnara wa maji wa Mlima Kenya ili kuokoa misitu, maeneo yenye mianzi, ardhi oevu, na chemichemi. Pia aliangazia umuhimu wa kuhifadhi sehemu zilizo kando ya kingo za mito kama kipaombele kwa serikali, na wahusika wa kitaifa na kimataifa. “Matumizi ya busara ya maji na kupanga vyema pia kunaweza kusaidia hata kama barafu itayeyuka,” alisema Kalua.
Alihitisha kusema: “Ingawa kufifia kwa barafu ifikapo mwaka 2040 huenda kusisimamishe Mto Tana, kutasababisha kupotea kwa utulivu, misimu mikali ya kiangazi, mafuriko, kuongezeka kwa mmomonyoko wa ardhi na kurundikana mchanga kwenye mabwawa.”

Mabadiliko ya hali ya hewa, kuyeyuka kwa barafu na kupungua kwa kina cha maji zimeleta athari kubwa kwa ufugaji wa samaki aina ya trauti kwa jamii zinazopakana na Mlima Kenya. Tayari wengi wameachana na biashara hiyo na wengine kuhamishiwa hifadhi hadi katika sehemu zenye ubaridi.
Jinsi jamii zinastahimili
Baadhi ya wakulima sasa wanaekeza kwa kiasi kikubwa kwenye mifumo ya kurejesha hewa safi na matumizi ya miale ya kiza (UV) ili kupunguza bakteria kwenye madimbwi yao bandia.
Mkurugenzi wa ufugaji samaki kwenye taasisi ya utafiti wa bahari na uvuvi (KMFRI) Dkt. Jonathan Munguti, alifafanua kuwa takriban mashamba 70 ya samaki katika baadhi ya sehemu kame yamefungwa kwa sababu ya uhaba wa maji. Baadhi ya wakulima katika mfumo iklojia wa Mlima Kenya wamesogea katika nyanda za juu kwenye mito inayotokana na halijoto bora ya kukua kwa samaki aina ya trauti.
Ngatia alisema mzunguko wa ukame, ambao haujasaza kitovu cha misitu ya Mlima Kenya kama vile Msitu wa Hombe umeifunza jamii kwamba ni ima wastahimili au waangamie.
“Baada ya ukame mbaya zaidi uliotokea Hombe mwaka 1978, wazazi wangu walianza kutegemea virutubishi vya njaa, jambo ambalo halikuwa la kawaida. Watu walianza kuchota maji kutoka kwenye Mto Sagana na mito mingine kunyunyizia mashamba yao. Tangu wakati huo wakulima wengi wametumia kilimo cha unyunyizaji maji na kuacha kutegemea mvua.”
Hatua hii ilikuwa ni ya mabadiliko iliyosababisha kuanzishwa kwa Mradi wa Maji wa Unyunyizaji mashamba wa Sagana, ambao kwa sasa una wanachama zaidi ya 1,000 waliobobea katika kilimo cha bustani. Eneo hilo sasa ni maarufu kwa kilimo cha maua ya kukata, kabichi, karoti, maharagwe, stroberi na ufugaji wa maziwa.
Uhitaji wa maji kwa ajili ya unyunyizaji mashamba na matumizi ya nyumbani umeongezeka mara kwa mara kama inavyoonyeshwa na idadi ya vituo vya uondoaji vilivyopanda kutoka moja mwaka 1978 hadi 48 ambavyo sasa vinaenea kutoka kwenye daraja karibu na kituo cha kutolea samaki wadogo cha Sagana hadi mlimani.
Ili kudumisha usawa, mwaka 2001, wakulima walibuni muungano wa watumiaji rasilimali maji ya Sagana, ambayo pia ilibuni Muungano wa Misitu ya Jamii ya Hombe, ambayo huzalisha miche 200,000 na 500,000.
“Tumerejesha hekta 1,200 za misitu kati ya mwaka 2001 na 2003 na tangu wakati huo tumekuwa tukipanda wastani wa hekta 100 kila mwaka. Kuhimiza ukuaji wa miti, kitalu chetu kimeanzisha baadhi ya miti ya matunda kama parachichi na makadamia, ambayo husambazwa kwa wanachama,” Ngaatia aliesema.
Kwa uendelevu, Muungano wa Misitu ya Jamii imeungana na shule katika miradi ya uvunaji wa maji, ambapo kila taasisi imepewa angalau matanki mawili ya maji kwa ajili ya kutumia maji ya mvua na kupunguza utegemezi wa mito. Mashamba ya miti yameanzishwa shuleni, makanisani na taasisi zingine ili kupanua eneo la misitu.
“Hatutategemea mifumo asili ya chakula. Kuna vigezo vingi ambavyo hatuwezi kuvidhibiti. Tunaweza kudhibiti joto na hivyo tunawahimiza wakulima kuboresha,” mwanasayansi Munguti aliiambia Mongabay.
Picha ya bango: Ng’ombe akila kwenye taka mita chache kutoka kwa Mto Naro Moru ambao pia umeathirika na kuyeyuka kwa barafu kwenye vilele vya Mlima Kenya. Picha na Amos Kareithi, Mongabay.