- Mwaka 2002, ufukwe wa Dunga uliopo ndani ya eneo kubwa la oevu la Dunga katika mji wa Kisumu kando ya Ziwa Victoria nchini Kenya, ulikuwa umejaa mifuko ya plastiki iliyoziba na kuharibu mazingira. Uoto wa asili wa cyperus papyrusulikuwa ukivunwa kwa kiwango cha kutisha.
- Wanachama wa umoja unaojulikana kama Dunga Ecotourism and Environmental Association, kwa kutambua fursa zitokanazo na utalii wa ziwa, waliamua kuondoa mirundikano ya taka za plastiki zilizokuwa zimeharibu mandhari ya eneo hilo.
- Bwawa la Dunga limeorodheshwa kama eneo Muhimu la Bioanuwai (Key Biodiversity Area), lakini liko miongoni mwa mabwawayaliyo hatarini kutokana na uchafuzi wa mazingira pamoja na uvunaji usio endelevu wa mafunjo.
- Ukosefu wa takwimu sahihi umeleta changamoto kwa DECTTAkufanikisha jitihada zake za kushawishi eneo hilo litangazwe rasmi kwenye gazeti ili liweze kunufaika kikamilifu na faida za uhifadhi.
Miale ya jua imechomoza na kutengeneza mwanga wa kupendeza juu ya Ziwa Victoria, Afrika Mashariki. Upepo mwanana kutoka ziwani umebeba sauti za kuvutia za ndege, huku mitumbwi ya mbao ya kawaida ikitia nanga taratibu ufukweni. Maji yametulia.
Mara kwa mara, ndege aina ya African sacred ibis (Threskiornis aethiopicus) huruka kwa ustadi mkubwa na kunyakua samaki kwa midomo yao kisha hupaa. Mazingira ya Ufukwe wa Dunga ni ya utulivu na amani. Baada ya saa chache, wauza samaki watawasili kuanza majadiliano ya bei na wavuvi waliokesha usiku kucha wakivuta nyavu, ambazo mara nyingi hurudi zikiwa karibu tupu.
Kwenye kijito kilichopo nyuma ya msururu wa vibanda vilivyojengwa kwa mbao na bati, njia nyembamba iliyozibwa na mashina ya magugu maji (water hyacinth) yaliyokaushwa imepinda kuelekea kwenye njia ya mbao iliyoinuliwa.
Victor Ochieng’ Didi, mwenye umri wa miaka 32, anatembea juu ya mbao hizo akiwa na kundi la watalii wa Kenya. Watazamaji wa ndege kwa mwaka mzima wamekuwa wakipanga kutembelea eneo hilo na kushuhudia mandhari ya kuvutia yenye ndege aina ya papyrus gonolek (Laniarius mufumbiri), ambaye kwa mujibu wa Orodha Nyekundu ya IUCN, ameorodheshwa kama aliye katika hatari ya kutoweka (near threatened). Kulingana na tovuti ya ufuatiliaji wa ndege ya EBird, ndege huyo alionekana mara ya mwisho katika eneo oevu la Dunga mwaka 2024.

Juhudi za kuokoa bwawa la Dunga
Mnamo mwaka 2002, ufukwe wa Dunga, uliopo ndani ya eneo kubwa la ardhi oevu ya Dunga katika mji wa Kisumu, kando ya Ziwa Victoria nchini Kenya, ulikuwa ukikabiliwa na tatizo kubwa la uchafu unaotokana na mifuko ya plastiki iliyotapakaa kila mahali. Wakati huohuo, uoto mnene wa mafunjo (cyperus papyrus) ulikuwa ukivunwa kwa kasi ya kutisha.
“Samaki walikuwa wakipungua sana. Hivyo watu wakaanza kugeukia kazi za mikono, wakivuna mafunjo kutengeneza kofia na samani, ambavyo vilipata umaarufu mkubwa,” anasema Didi.
Wavuvi wakirejea ufuoni baada ya kazi katika Ziwa Victoria. Picha na Achieng’ Otieno.Ili kuingilia kati uharibifu huo, Chama cha Utalii na Uhifadhi wa Mazingira cha Dunga (DECTTA), kilichoundwa na Ushirika wa Ufukwe wa Dunga, kililazimika kuweka kambi kwenye ufukwe huo kwa lengo la kuurudisha katika hali yake ya awali. Lengo la wavuvi hao lilikuwa kutumia fursa za utalii katika ziwa hilo, sambamba na kuondoa mlundikano wa taka za plastiki zilizokuwa zimegeuka kuwa kero na doa lililotia aibu katika eneo hilo.
DECTTA, huku ikifanya kazi kwa karibu na vijana wa eneo hilo, iliua ndege wawili kwa jiwe moja: yaani kuondoa mlundikano wa takataka za plastiki zilizokuwa zimetupwatupwa ovyo eneo hilo na pia kutoa ajira katika sekta ya utalii wa ikolojia. Makumi ya vijana walipata ajira kama waendeshaji wa mitumbwi, waongoza boti za mbao na pia wasindikizaji wa watalii waliokuwa wakizunguka juu ya maji ya ziwa hilo kubwa zaidi la tropiki duniani.
Hata hivyo, ari na matumaini waliyokuwa nayo mwanzo wa mradi huo yalididimia haraka. Kufikia mwaka 2006, maeneo ya mazalia ya samaki yalikuwa yamevamiwa, huku wavuvi wakitanua wigo wa uvuvi wao. Walitupa nyavu zao hadi katika maeneo ya kuzaliana kwa samaki, wakivua si tu vifaranga vya samaki bali pia nyasi za viboko (Vossia cuspidata) zinazozunguka mwambao wa ziwa.
Maduka yaliyokuwa yakiuza samani na bidhaa nyingine za ufundi zilizotengenezwa kwa mafunjo yaliongezeka kwa kasi. Kutokana na hali hiyo, DECTTA ilipoteza nguvu na hadhi yake ya awali, ikibaki kama kivuli cha ilivyokuwa mwanzo. Vijana wengi hawakuwa tena na hamasa ya shughuli za uhifadhi.
“Wananchi wengi waligundua kuwa watalii waliokuwa wakimiminika kwa ajili ya safari za boti walivutiwa zaidi na bidhaa zilizotengenezwa kwa mafunjo. Kila mtu aligeuka kuwa msanii, kasi ya uvunaji wa mafunjo ikaendelea kuwa kubwa kuliko ile ya kustawi kwake,” Didi aliiambia Mongabay katika mahojiano yaliyofanyika kwenye ufukwe wa Dunga.

Kurudi kwenye mstari
Mnamo mwaka 2008, DECTTA ilifufuliwa upya. Vijana, wengi wao wakiwa wametoka mijini na kurejea kijijini kufuatia hali ya kisiasa isiyotabirika, walirudisha tena hadhi na uzuri wa ufukwe wa Dunga uliowahi kuwa wa kuvutia sana. Didi alijitoa kikamilifu kusimamia juhudi hizo, akipiga simu na kubisha hodi kila mahali ili kufanikisha ndoto hiyo.
Mnamo mwaka 2015, wazo la kuanzisha maonyesho ya ardhi oevu (wetland gallery) lililobuniwa na mwanafunzi kutoka Chuo Kikuu ya Uppsala nchini Sweden, lilianza kutekelezwa, na baadaye njia ya mbao (boardwalk) ya Dunga ikajengwa.
“DECTTA inajikita sana katika utalii wa ikolojia. Tunatoza ada ndogo kwa wanaotaka kujifunza kuhusu ardhi oevu. Fedha tunazokusanya hutumika katika matengenezo pamoja na programu za chakula kwa wazee na shule wakati wa siku za masomo,” anasema Didi.
Kundi hilo pia linamiliki boti mbili za mbao, ambazo huingizia fedha zinazotumika kulipia umeme na bili nyingine za uendeshaji. Mmoja wa wanachama wa kundi hilo, ambaye pia ni mweka hazina wa DECTTA, Faith Adhiambo, anasema shughuli hizi zimewaongezea hamasa na ari ya uhifadhi.
“Ukweli ni, watu wana haja ya kipato. Pale utalii unapowaletea mapato na wakati huohuo kufadhili programu za chakula kwa wazee, inakuwa rahisi zaidi kuwashawishi watu wengi, wakiwemo vijana na wazee, kuacha kuvuna mafunjo,” Didi aliiambia Mongabay.
Ardhi oevu ya Dunga
Ufukwe wa Dunga uko ndani ya ardhi oevu ya Dunga, maarufu pia kama bwawa la Dunga, ambalo ni hifadhi muhimu ya kaboni na makazi muhimu kwa viumbe adimu, wakiwemo swala aina ya Sitatunga (Tragelaphus spekii) aliye hatarini na ndege ambao kitalaam wanajulikana kama Calamonastides gracilirostris.
Ndege wa papyrus gonolek (Laniarius mufumbiri) pia hupatikana kwenye bonde la maji la Dunga. Ndege huyo ana manyoya mekundu na meusi na taji la rangi ya njano huku macho yake yakiwa yaliyopauka. Hupatikana kwenye mabonde ya papyrus kama vile Dunga na bonde la Yala katika Kaunti ya Siaya, ambapo papyrus (Cyperus papyrus) inakua kwa wingi.

Hata hivyo, ndege huyu anakaribia kuingizwa kwenye orodha ya kundi la ndege walio hatarini nchini Kenya. Hii inatokana na uharibifu wa papyrus unaotokana na kuingiliwa na shughuli za binadamu pamoja na uchafuzi wa mazingira.
Ripoti ya Sensa ya Wanyamapori ya Kenya ya mwaka 2021 ilionyesha kuwa kulikuwa na swala 473 wa Sitatunga, “ambao kati yao 424 walirekodiwa katika Eneo la Hifadhi la Magharibi na 49 kwenye eneo la Central Rift Conservation.” Ripoti ya Sensa mpya ya Wanyamapori ya mwaka 2025 ilionyesha takwimu zilezile katika maeneo yaliyotajwa kwenye ripoti ya mwaka 2021, ambapo pwani ya Dunga na Impala A na B huko Kisumu zilihesabiwa kuwa na swala 25 tu, sawa na asilimia 5.29 ya idadi yote ya watu.
Bonde la Dunga limeorodheshwa kama Eneo Muhimu la Bioanuwai (Key Biodiversity Area). Pia limeorodheshwa kuwa chini ya tishio kutokana na uchafuzi pamoja na uvunaji usio endelevu wa majani ya mafunjo.
Changamoto zinazokabili Dunga
Miongoni mwa changamoto kubwa zinazoikabili Dunga ni pamoja na kukosekana kwa sera moja ya kitaifa inayosimamia kikamilifu masuala yote yanayohusiana na maeneo oevu (wetlands). Tatizo hilo limefanya usimamizi kuwa mgumu. Kutokana na kukosekana kwa sheria mama (Act) moja, usimamizi wa maeneo oevu usimamizi wake unategemea Sera ya Kitaifa ya Uhifadhi na Usimamizi wa Maeneo Oevu, Kanuni za Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi na Uratibu wa Mazingira (Uhifadhi na Usimamizi wa Maeneo Oevu) za mwaka 2009, pamoja na mikakati ya ngazi ya kaunti.
Mnamo Februari mwaka 2025, NEMA ilitoa tangazo kwa umma likieleza mipango ya kurekebisha kanuni za mwaka 2009 ili ziendane na Katiba ya Kenya ya mwaka 2010, lakini pia zizingatie changamoto zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi, na kutoa mwongozo wa kisasa zaidi kuhusu usimamizi wa maeneo oevu.
Kwa mujibu wa Dkt. Paul Abuom, kutoka Idara ya Sayansi ya Mazingira ya Chuo Kikuu cha Maseno, changamoto zinazolikabili eneo la Dunga zinachochewa zaidi na utekelezaji dhaifu wa sera zilizopo, unaosababishwa na mifumo dhaifu ya taasisi pamoja na ukosefu wa uratibu kati ya wizara na serikali za kaunti.
Faith Omole, mtaalam wa Sayansi ya Mazingira, ambaye amewahi kuwa Kiongozi wa Kiufundi wa Mradi wa WASH wa UNICEF huko Kakuma, Kenya, ambako kuna maelfu ya wakimbizi wa vita na mabadiliko ya tabianchi, amesisitiza pia umuhimu wa taasisi za serikali kufanya kazi kwa pamoja kulinda maeneo oevu.


“Kwa sasa, ni chini ya asilimia 10 tu ya maeneo oevu yaliyoko chini ya ulinzi wa kisheria uliotangazwa rasmi. Badala ya kila wizara kufanya jitihada za peke yake, inahitajika sheria zilizoratibiwa zitakazohakikisha juhudi za uhifadhi zinafanywa kwa ushirikiano na zinakuwa jumuishi,” aliiambia Mongabay.
Vivyo hivyo, kushindwa kuingiza kikamilifu uhifadhi wa bayoanuai katika mikakati ya urejeshaji, upungufu wa takwimu za msingi, pamoja na ukosefu wa mifumo sanifu ya ufuatiliaji na utoaji wa taarifa, ni changamoto nyingine kubwa katika kulinda na kurejesha maeneo oevu, anasema Dkt. Abuom.
Licha ya juhudi za muda mrefu kutoka kwa makundi ya watetezi wa mazingira, eneo oevu la Dunga bado halijatambuliwa rasmi (halijatangazwa kwenye gazeti) kama eneo linalotakiwa kulindwa.
Tom Togo, aliyewahi kuwa Mkurugenzi wa NEMA katika Kaunti ya Kisumu, anataja ukosefu wa ushiriki wa jamii katika mipango ya uhifadhi kama kikwazo kikubwa, akikumbuka jitihada zake za kuishawishi serikali ya Kaunti ya Kisumu kutangaza Dunga na maeneo mengine oevu kuwa maeneo yanayotakiwa kulindwa.
“Mara yatakapotangazwa rasmi kama maeneo yaliyohifadhiwa, itakuwa rahisi zaidi kuyasimamia. Changamoto ni kwamba maeneo haya oevu yapo ndani ya mashamba ya watu binafsi, na wana hati miliki. Huwezi kuwaamuru watu namna ya kutumia ardhi yao. Ndiyo maana tunaona uharibifu mkubwa,” aliiambia Mongabay katika mahojiano kwa njia ya simu.
Msukumo huu umeibua mgogoro kati ya jamii na wanaharakati wa uhifadhi wa mazingira, ambao mara nyingi wameshutumiwa kuwa na maslahi binafsi ya kifedha.


Michael Nyaguti, anayefanya kazi kwa karibu na DECTTA, amekuwa akiwahamasisha wakazi wa kijiji cha Usoma ili waondoke katika maeneo ya hifadhi ya maji (riparian land). “Hawaelewi kwamba hili ni eneo oevu. Lakini baada ya mafuriko ya Ziwa Victoria baadhi yao walilazimika kuhama, hilo limenisaidia kuwashawishi waondoke,” anasema.
Didi anaeleza ugumu mkubwa wa kukabiliana na makampuni makubwa yanayojenga miundombinu ndani ya eneo oevu. Hoteli nyingi zinazojivunia mandhari ya kuvutia kando ya ziwa huharibu kwa kiasi kikubwa mafunjo na nyasi za viboko (Vossia cuspidata) wakati wa ujenzi. “Hatutashinda kwa sababu hawa watu wana fedha nyingi. Juhudi zetu hazina nguvu ya kisheria,” anasema.
Mapambano ya kisheria kuokoa eneo oevu
Mnamo Oktoba mwaka 2025, Mahakama ya Mazingira na Ardhi iliyokaa katika mji wa kando ya Ziwa Victoria wa Kisumu, iliwakuta na hatia magavana wawili wa zamani pamoja na ofisa mmoja mwandamizi kutoka Wizara ya Mazingira ya Kenya kwa kuvamia maeneo ya hifadhi ya maji (riparian land) yanayozunguka Ziwa Victoria. Mahakama iliamuru majengo yao yaliyojengwa katika maeneo hayo yabomolewe ndani ya siku 90. Kesi hiyo, iliyofunguliwa na Nyaguti, ilikuwa imekwama mahakamani tangu mwaka 2013.
“Huu ni ushindi. Ni kama kujenga nyumba. Hili ni tofali moja muhimu, ambalo tutakuwa tukilirejelea kila wakati tunapojenga hoja ya kutenganisha na kutambua rasmi eneo oevu, au kila panapojitokeza jaribio jipya la kuvamia,” alisema Nyaguti.
Mapungufu ya takwimu katika kuokoa eneo oevu
Matokeo ya programu ya ufuatiliaji wa kisayansi uliofanyika kwa agizo la Tume ya Bonde la Ziwa Victoria Basin (LVBC) yamebaini kuongezeka kwa uchafuzi wa maji katika maeneo ya karibu na ufukwe wa ziwa.
Uchafuzi huo unasababishwa na maji taka yasiyotibiwa, mtiririko wa mabaki ya kilimo, pamoja na utupaji wa taka ngumu. Utafiti huo, ambao bado haujachapishwa, ulifanywa kwa ushirikiano kati ya Kenya, Uganda na Tanzania, na ulijumuisha zaidi ya maeneo 44 katika ziwa lote, ikiwemo maeneo ya mijini yaliyoathirika zaidi kama Kisumu, Kampala, Entebbe na Mwanza.

Kwa mujibu wa Afisa wa Usimamizi wa Rasilimali za Maji wa LVBC Mhandisi Simon Otoung, tathmini hiyo ilichunguza vigezo mbalimbali, ikiwemo kiwango cha asidi (pH), joto la maji, ukungu wa maji (turbidity), oksijeni iliyoyeyushwa, pamoja na mionzi inayotumika katika usanisinuru (Photosynthetically active radiation (PAR)). Uchambuzi wa virutubisho ulionyesha viwango vya juu vya nitrojeni na fosforasi, ambavyo ni vichocheo vikuu vya ukuaji wa mwani, pamoja na silika, alkalini na chembechembe jumla zinazosimamishwa ndani ya maji.
“Tunachohitaji ni takwimu zitakazotusaidia kupanga hatua sahihi za kuingilia kati. Tunachobaini ni kwamba uhifadhi lazima uanze juu ya mto, upitie kwenye maeneo oevu, na hatimaye uingie ziwani,” anasema Otoung.
Didi, mwenye shahada ya kwanza ya Sayansi ya Mazingira, analalamika kuwa ukosefu wa takwimu sahihi unaendelea kuwa changamoto kubwa kwa DECTTA katika jitihada zake za kulitangazia rasmi eneo oevu ili lipate manufaa kamili ya uhifadhi.
“Ukubwa halisi wa eneo oevu haujulikani. Hivyo tunapozungumzia uharibifu kwa kutumia sampuli kutoka maeneo fulani, tunaulizwa ni kwa vigezo gani tunaamua kuwa eneo hilo ni sehemu ya ardhi oevu. Tunahitaji takwimu sahihi kutoka vyuo vikuu na taasisi husika za serikali,” anasema Didi.
Dkt. Christopher Aura, Mkurugenzi wa Mifumo ya Maji Safi katika Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi na Bahari ya Kenya (KMFRI), anasisitiza umuhimu wa kutumia mkabala jumuishi katika uhifadhi wa maeneo oevu. “Maeneo oevu ni mapafu ya ziwa. Ndiyo chujio la mwisho kabla ya maji kutoka maeneo mengine yote kuingia ziwani. Kushindwa kulinda mapafu ni sawa na kujihakikishia kifo. Ziwa litakufa,” anasema Dkt. Aura.

Katika ngazi ya kimataifa, Mpango wa Mazingira wa Umoja wa Mataifa (UNEP) na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) wanaendesha kampeni mbalimbali zinazolenga kurejesha mifumo ya ikolojia, ikiwemo maeneo oevu.
Muongo wa Umoja wa Mataifa wa Urejeshaji wa Ikolojia (2021- 2030) unalenga kuongeza uelewa, kuhamasisha ushirikiano, na kuharakisha urejeshaji wa mifumo ya ikolojia ya nchi kavu na ya majini. Mikakati hii ya pande mbili na ya kimataifa inalenga kuboresha usalama wa chakula na maji, pamoja na kuzuia upotevu wa bayoanuai.
Hatua inayofuata kwa Dunga
Kikundi cha Vijana cha Utalii wa Ikolojia na Mazingira cha Dunga (Dunga Ecotourism and Environmental Youth Group) kimeanzisha mazungumzo na FAO, serikali ya Kaunti ya Kisumu, pamoja na wadau wengine, kwa lengo la kuanzisha dhana ya bustani ya eneo oevu (wetland garden).
Dhana hii inalenga kuunda mfumo mdogo wa ikolojia wenye bayoanuai kwa kuiga maeneo oevu ya asili kwa kutumia maji yenye kina kifupi, maeneo yenye unyevunyevu tofauti, na mimea asilia ili kuvutia viumbe kama vyura, ndege na wadudu wachavushaji.
Miundo hii hutengenezwa kwa kutumia vitambaa maalum na viwango tofauti vya kina cha maji ili kuhimili viumbe wa majini na kusaidia kuchuja maji, hivyo kufanya kazi kama pambo na mbadala wa bustani za maji ya mvua.
Didi ana matumaini kuwa kwa kuingiza kipendele cha mapato, mbinu hii itawahamasisha wananchi kuhifadhi eneo oevu kubwa zaidi. “Tunapanga kuwa na maonyesho mbalimbali, kwa mfano, kaya moja iwe na aquarium, nyingine iwe na shamba la mfano, na nyingine njia ya mbao. Hii itasaidia kujenga hali ya umiliki miongoni mwa jamii,” anasema.
Kwa kutambua umuhimu wa uwepo wa sheria madhubuti, Didi anasema ataendelea kushawishi ili Dunga pamoja na maeneo oevu mengine saba yatangazwe rasmi. “Bado tunatafuta viongozi wanaoweza kuwasilisha muswada wa sheria kwa ajili ya kutangazwa rasmi katika bunge la kaunti. Gavana wa Kaunti ya Kisumu amekuwa akijaribu kutetea uhifadhi, lakini juhudi hizi zinahitaji kuimarishwa kisheria,” Didi aliiambia Mongabay.
Adhiambo, Mweka Hazina wa DECTTA, ana uzoefu wa moja kwa moja unaoonyesha jinsi urejeshaji wa maeneo oevu unavyoweza kubadilisha maisha. “Nilianza kama msaidizi wa ofisi katika DECTTA. Kadri muda ulivyopita, nimeona jinsi eneo hili lilivyokuwa safi na lenye mpangilio mzuri zaidi. Tukifanikiwa kupata njia ya uhakika ya kipato, tutakuwa na watu wengi zaidi watakaosaidia katika juhudi za uhifadhi,” Adhiambo anasema.

Shirika la Kimataifa la Uhifadhi wa Wanyamapori na Mazingira (WWF)–Kenya limekuwa likiendesha kampeni za uhifadhi wa maeneo oevu nchini Kenya na Tanzania. Meneja wa Mpango wa Mandhari ya Kusini mwa Kenya wa WWF–Kenya, Dkt. Martin Mulama, anasema kampeni hiyo inalenga kuongeza uelewa kuhusu uharibifu wa vyanzo vya maji.
“Watu wengi sasa wanaelewa kuwa maji hayatoki tu kwenye bomba; huanzia kwenye misitu, maeneo oevu na vyanzo vya maji vilivyopo milimani ambavyo lazima vilindwe,” aliiambia Mongabay katika mahojiano kwa njia ya simu.
Kwa sasa, DECTTA inaweka akiba ili kununua boti ya fiberglass kwa lengo la kuongeza fursa zake za kiuchumi. Fedha zitakazopatikana kupitia chanzo hiki, wanasema, zitatumika kuanzisha bustani ya eneo oevu.
Kikundi hicho kinafanya kazi kwa karibu na vikundi vingine viwili vya vijana chini ya Dunga Swamp Site Support Group. Vijana hao pia wanatoa huduma za uongozaji wa watalii, hususan wale wanaopenda kutazama ndege katika maeneo ya Dunga na Hippo Focus, ambayo hutoa huduma maalum za safari za boti.
Didi anaamini kuwa juhudi hizi za pamoja hatimaye zitaisukuma serikali kuchukua hatua za kutangaza rasmi bwawa la Dunga kama eneo linalolindwa, na hivyo kuokoa bayoanuai ambayo kwa sasa iko hatarini.
Picha ya Bango: Mafunjo ya papyrus yakikua katika Ufukwe wa Dunga upande wa Kenya wa Ziwa Victoria. Picha na Achieng’ Otieno.
Nukuu:
Otieno, Nickson & Matiku, Paul & Kiragu, Anthony & Musila, Simon. (2005). Kenya’s Important Bird Areas Status and Trends 2004. 10.13140/RG.2.2.10970.20160