- Kwa zaidi ya miongo miwili sasa, eneo la Kuruwitu limejulikana sana kwa uhifadhi wa mazingira ya bahari.
- Kuruwitu ni eneo la kwanza katika ukanda wa pwani ambalo jamii ilipata msukumo kutokana na hali mbaya ya mazingira ya bahari, na kutafuta mbinu za kurudisha mazingira hayo katika hali ya awali.
- Hali hiyo mbaya ya mazingira ya bahari ilichangia upungufu maradufu wa samaki na viumbe wengine wa baharini.
- Eneo hili linalindwa na wanajamii, hivyo kusababisha samaki kuwa na mazingira mwafaka ya kuzaana zaidi, na kumiminika hadi sehemu ambazo wavuvi wanaruhusiwa kuvua, hivyo basi kuongeza kipato.
Kwa zaidi ya miongo miwili sasa, eneo la Kuruwitu limejulikana sana kwa uhifadhi wa mazingira ya Bahari kiasi kwamba kizazi kipya cha rika la vijana (hususan Gen Z), wanalitambua. Hii ilidhihirika wazi pale nilipotua kituo cha basi cha Shariani, barabara kuu ya kutoka Mombasa kuelekea Malindi, na kuulizia mwelekeo kufika baharini.
“Unaenda Kuruwitu ile ya uhifadhi wa mazingira ya baharini?” aliniuliza kijana wa rika, mwendesha pikipiki. Na baada ya dakika kama saba, nilikuwa nimefika eneo hilo.
Mkurugenzi mkuu wa shirika la Kuruwitu Conservation Welfare and Association Daniel Mwangunya alikuwa ameshawasili tayari kuhojiwa kuhusu shughuli zao za uhifadhi wa mazingira ya bahari katika bandari ya Kinuni.
Lakini kwanza aliomba tumsubiri mkuu wa kitengo cha uhifadhi wa matumbawe, ambaye kwa wakati huo alikuwa amepeleka wageni kuzama na kutalii mandhari ndani ya bahari.
Tengefu ni eneo la bahari lililotengwa na kusimamiwa na wanajamii kwa ajili ya uhifadhi wa viumbe na mazingira ya baharini.

Katika mantiki ya tengefu, hili ni eneo ambalo uvuvi wa samaki hauruhusiwi. Eneo hili linalindwa na wanajamii, hivyo kusababisha samaki kuwa na mazingira mwafaka ya kuzaana na kuongezeka. Wanapokuwa wengi, wanamiminika hadi sehemu ambazo wavuvi wanaruhusiwa kuvua, hivyo basi kuongeza kipato.
Utulivu ulionikaribisha hapo ni ishara kwamba hakuna shughuli za uvuvi zinazoendelea, bali ni pilkapilka za kupokea wageni, kutayarisha vifaa kama vile mashua na zana za kuzamia kwenye bahari.
Katana Ngala ni mzaliwa wa kijiji cha Kuruwitu, na ni miongoni mwa waanzilishi wa tengefu hiyo. Kwa sasa anaongoza kitengo cha urejeshaji wa matumbawe, taaluma ambayo ameifanya kwa zaidi ya miongo miwili, na kujizolea sifa kedekede.

Ngala alikua miongoni mwa watu wachache waliompokea na kumuonyesha Mfalme Charles III wa Uingereza jinsi matumbawe yanavyorejeshwa baharini. Mfalme huyo alizuru Kenya mwezi Novemba mwaka 2023 kujionea shughuli za uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
“Chama cha uhifadhi wa mazingira ya bahari hapa Kuruwitu kilianzishwa na wavuvi na wachuuzi wa samaki mwaka wa 2003, baada ya kuona mabadiliko hususan upungufu wa samaki. Mapungufu haya tulianza kuyaona baada ya mvua kubwa ya El Niño ya mwaka 1997 na 1998, ambapo tulishuhudia uharibifu wa matumbawe na uhaba wa samaki,” alisema Ngala.
Tatizo jingine lilikuwa ongezeko la uvuvi haramu na uvuvi wa samaki wa marembo, ambao walikua wanasafirishwa nje ya nchi bila jamii kufaidika.

Kwa mujibu wa Ngala, zamani kabla nyenzo mbaya za uvuvi kukithiri, wazee walikuwa wakivua karibu na ufuo wa bahari na kupata hata kilo 40 za samaki. Baadaye, hali ilibadilika na wavuvi wakalazimika kwenda mbali sana kutafuta samaki.
Hofu waliyokuwa nayo wavuvi wa Kuruwitu kuhusu uhaba wa samaki ilithibitishwa na utafiti uliofanywa na wanasayansi kutoka shirika la kiserikali la utafiti wa baharini la KMFRI, mashirika yasiyo ya kiserikali kama vile Wildlife Conservation Society (WCS) na Coastal Oceans Research and Development in the Indian Ocean (CORDIO).
Kutokana na thibitisho hilo, Ngala alisema wavuvi na wachuuzi kutoka bandari sita za Bureni, Vipingo, Kinuni, Kuruwitu, Kijangwani na Mwanamia waliamua kuungana, lengo lao kubwa likiwa ni kuhifadhi mazingira ya baharini na kukomesha uvuvi haramu.
“Ilipofika mwaka wa 2006, sote tulikubaliana kuweka alama katika sehemu ambayo tumeona itatufaa kwa huo uhifadhi. Baada ya kuchagua eneo la uhifadhi kulikua na haja ya kupata mafunzo kuhusu tengefu. Hapo ndipo shirika la East African Wildlife Society lilipotafuta na kupata ufadhili kutoka kwa shirika la African Foundation for Endangered Wildlife (AFEW),” alisema Ngala.
Ufadhili huo uliwawezesha kwenda nchini Tanzania na kujifunza jinsi ya kuanzisha na kuendesha tengefu. Hatimaye walianzisha tengefu ya Kuruwitu, kwanza kwa muda wa miezi sita kama majaribio.
Matokeo, kwa mujibu wa Ngala, yalikua ya kuridhisha. “Samaki walikuwa wengi na kufika mpaka ufuoni mwa bahari. Tuliamua kuendelea kuhifadhi eneo hilo lenye ukubwa wa hekta 30,” Ngala aliiambia Mongabay.
Baada ya mafanikio hayo, Kuruwitu Conservation Welfare and Association ilianzisha mchakato mwingine wa uhifadhi wa mazingira ya baharini kwa kurejesha matumbawe ambayo pia yaliathiriwa kutokana na mabadiliko ya tabianchi na uvuvi mbaya katika tengefu hiyo.
Urejeshaji wa matumbawe
Ngala alisema walianza kazi hiyo ya urejeshaji kwa kuchukua vipande vya matumbawe yaliyovunjika na kuyatundika kwenye miamba ya matumbawe. Baada ya muda yalianza kumea.
Mwaka wa 2019 ndio walipoanza rasmi urejeshaji wa matumbawe baharini, baada ya majaribio kuonyesha matokeo chanya. Wameendeleza shughuli hizo hadi sasa na kuvutia wadau mbalimbali kote ulimwenguni kuja kujionea ili kuiga na kutengeneza maeneo yao.


Hifadhi ya Kuruwitu haikusudiwi kuongeza idadi ya samaki tu, bali pia eneo hilo limekuwa kivutio kikubwa sana cha watalii kutoka Kenya na hata mataifa mengine.
Watalii wamiminika pwani
Meneja wa Miradi wa Hifadhi hiyo Daniel Mwangunya alisema ujio wa wageni hutegemea hali ilivyo nchini. Kwa mfano, mwaka wa 2024 walipokea wageni zaidi ya 1,480, kulingana na takwimu zao.
“Idadi hii tumeipata kulingana na wageni ambao kawaida hulipa kielektroniki kwa benki. Mwaka wa 2025 tulipata watalii 1,350 kutoka Kenya na kwingineko, ambao waliokaa hadi Desemba 31,” alisema Mwangunya.

Kwa mujibu wa Mwangunya, watalii wanoenda kuangalia tengefu hutumia boti na vifaa vya kuzamia kuangalia mandhari ya bahari.
“Sio tu watalii na wanasayansi, bali tunapata makundi ya wavuvi, yaani BMU, na wanamazingira wanaokuja kujifunza ni vipi tumeweza kushamiri katika uhifadhi. Kwa mfano, tumepata wageni kutoka Lamu na Kwale, ambao pia wameanzisha ama wananuia kuanzisha tengefu,” alisema meneja huyo.
“Pia wamekuja wanamazingira kutoka Zanzibar, na mataifa kama vile Mozambique na Madagascar kujifunza kutokana na kazi tunayoifanya,” alisema Mwangunya, akiongeza kuwa katika eneo hilo wanafanya uhifadhi na utalii na hivi sasa wako katika mikakati ya kutafuta masoko, haswa kwa kutumia mitandao ili wawafikie watu wengi duniani kote.
Moja ya BMU ambayo iliwahi kutembelea tengefu ya Kuruwitu na kuanzisha hifadhi yao ni Kibuyuni, iliyoko Kaunti ya Kwale, kusini mwa pwani ya Kenya.
Kibuyuni, ipatikanayo kilomita 165 kutoka tengefu hiyo ya Kuruwitu, ni kijiji chenye wanajamii wengi wanaotegemea bahari kujikimu. Wanaume wakiwa wavuvi, wanawake huhifadhi mazingira ya bahari kwa njia ya upanzi na uuzaji wa mwani.

Kulingana na Mwenyekiti wa BMU hiyo Mohamed Jasho, walikuwa na ardhi kubwa ya kufanya uhifadhi kupitia tengefu na mwaka wa 2007 walianza mipango. Hii iliwalazimu kutafuta elimu kuhusu swala hilo.
“Tayari wenzetu wa Wasini walikuwa wameshaanzisha tengefu na walikuwa wanatutia motisha. Kitu kilichotuvutia zaidi ni kwamba wenzetu walianza kupata watalii. Tulipata mafunzo kutoka kwa mashirika kama vile East African Wildlife Society, Idara ya Uvuvi ambao walitusaidia kupima eneo na ufadhili wa maboya.
“Lakini kabla ya kuweka maboya, tuliwahamasisha wavuvi wetu na kuwafahamisha kuhusu mipango ya kuanzisha tengefu na faida zinazotokana na mbinu hiyo ya uhifadhi,” alisema Jasho.
Tengefu ya Kibuyuni iko na ukubwa wa kilomita za mraba 2.8, lakini walianza na kilomita za mraba 2. Baadaye walipata ufadhili na kupanua eneo hilo.
Hamid Juma, mmoja wa waasisi wa tengefu ya Kibuyuni, alisema walianza kwa udogo sana na walifanya juhudi za kupata usajili kabla ya kuanza rasmi shughuli za uhifadhi. Kwa mujibu wa Hamid, lengo lilikuwa kukuza utalii na kutengeza mazingira bora kwa samaki kuzaana.
“Wavuvi walipatiwa hamasa ya kutosha kuhusu sababu na malengo ya kuanzisha tengefu na sheria zilizowekwa za uhifadhi. Baadaye viongozi wa BMU walipoanza kuzembea, walianza kuvua katika eneo ambalo lilikuwa limetengwa.

“Wakati tukianza tengefu hii, eneo ambalo lilikuwa linafanya vizuri katika uhifadhi lilikuwa la Kuruwitu pekee. Tulivutiwa sana kwa sababu tayari walikuwa na askari wa kushika doria na vifaa kama vile boti za kutembeza wageni,” alisema Hamid.
Aliongezea kuwa baadhi ya wanachama wa Kibuyuni BMU walienda Kuruwitu kujionea na kujifunza mambo mengi kuhusu usimamizi wa tengefu.
“Kikubwa tulichojifunza kutoka Kuruwitu lilikuwa nidhamu ya wavuvi, pamoja na kuheshimu na kutii sheria zilizowekwa, hasa katika swala la kutovua kabisa katika eneo lililotengwa kwa ajili ya mazalia ya samaki na uhifadhi wa matumbawe.
“Jambo jingine lililotuvutia sana ni jinsi walivyokuwa wakinufaika na utalii na idadi kubwa ya wageni waliotembelea hifadhi hiyo kuangalia mandhari mazuri chini ya bahari, kama vile matumbawe na aina mbalimbali za viumbe,” alisema Hamid.
Remy Oddenyo, mwanasayansi na mtafiti wa masuala ya baharini kutoka Shirika la Wildlife Conservation Society (WCS), alisema mbinu ya Tengefu imewapa matumaini mapya wavuvi wengi wanaoishi pwani ya Kenya.
Kulingana na takwimu za shirika hilo, Oddenyo alisema kwa sasa Kenya ina zaidi ya tengefu 20 katika eneo la pwani. Kati ya hizo, shirika hilo linasimamia tengefu 13.
Shirika la WCS, ambalo limefanya utafiti kwa muda mrefu katika masuala ya tengefu na uhusishwaji wa jamii katika uhifadhi, lina ushahidi wa kisayansi kuhusu ongezeko la samaki katika maeneo yanayohifadhiwa.
Takwimu zilizokusanywa na shirika hilo katika tengefu ya Kuruwitu zinaonyesha kuwa kuna ongezeko la samaki kutoka kilo 100 hadi kilo 400 na hata 500 kwa kila hekta.
“Katika eneo la Pwani kuna tengefu moja ambayo ilianzishwa miaka mingi iliyopita. Tengefu hii ni Kuruwitu, na iko kaunti ya Kilifi. Hali yake ya rasilimali imekuwa sawa na inatumika kama mfano mzuri kwa jamii ambazo zinataka kuanzisha tengefu,” alisema Oddenyo.
Kwa wastani, WCS imesaidia jamii kusimamia zaidi ya hekta 252 za bahari ili kuhakikisha wanapata samaki kwa njia endelevu. Wengi wao pia wameweza kutenga takriban asilimia 10 ya maeneo hayo kama tengefu.
Katika maeneo mengine kama vile Jomo Kenyatta, iliyoko Mombasa, ukubwa wa samaki umeongezeka katika maeneo yanayopakana na tengefu.
“Utafiti wetu umeonyesha kuwa mapato kwa wakaazi wanaoishi kando ya hifadhi hizo yameongezeka kwa asilimia 135. Faida pia zimeongezeka kutokana na ongezeko la samaki kwa sababu wavuvi wanachukua muda mfupi sana kupata samaki,” alisema Oddenyo.
Kulingana na utafiti wa mwaka 2023 kuhusu miamba ya matumbawe katika maeneo ya tengefu, uliofanywa na wanasayansi, wakiongozwa na mtaalamu wa kisayansi katika shirika la REEFolution Ewout Knoester, miamba ya matumbawe katika Tengefu ya Kuruwitu imerudi katika hali nzuri. Hii ni kutokana na uvuvi ambao hauruhusiwi katika eneo hilo, jambo linalowezesha matumbawe kuwa na afya nzuri.

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa idadi ya samaki wanaovuliwa katika eneo hilo imeongezeka.
Charles Muthama, ambaye ni mwanasayansi na mtafiti kutoka shirika la KMFRI, anasema tengefu zina manufaa kama vile kuhifadhi mazingira ya bahari na kutoa hifadhi kwa viumbe wa baharini walioko hatarini kuangamia, kwa mfano Kasa. Pia huboresha maeneo ya kuzaa kwa samaki, na kumiminika hadi wavuvi wanaporuhusiwa kuvua.
Zaidi ya hayo, nyasi bahari na miti ya mikoko inayopatikana katika maeneo ya tengefu husaidia sana unyonywaji wa kaboni baharini, hivyo kuboresha mazingira na kusaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Muthama alisema tengefu zinaelimisha jamii kuhusu uhifadhi wa mazingira ya baharini.
Swala la kutengeneza tengefu linaambatana na Sheria za Uvuvi na Maendeleo za mwaka 2016, zinazotoa fursa kwa jamii kushirikishwa katika uhifadhi wa mazingira, hasa ya bahari. Hii inawezesha vikundi vya wavuvi kuhakikisha wanadumisha maeneo wanayovua samaki na kuongeza mapato yao.
Joab Chai, mwenyekiti wa kikundi cha Uvuvi cha Kanamai Kilifi, alisema kuwa mwaka 2018 walianzisha tengefu bila kufanikiwa.
Chai alisema kwa kipindi hicho, aina za samaki kama vile pono, tafi na makangaja walikuwa wengi, lakini wavuvi haramu waliharibu mazingira hayo.
Lakini baada ya kupata mafunzo kutoka kwa mashirika mbalimbali, na kutembelea tengefu ya Kuruwitu, Chai alisema wako kwenye harakati za kuanzisha tena tengefu yao.
“Tengefu yetu ilianguka kwa sababu ya uongozi mbaya. Lakini kwa sasa, kulingana na mafundisho ambayo tumepata kutoka kwa mashirika kama WCS, CORDIO East Africa, na pia kaunti yetu ya Kilifi, tumeona ni heri turejeshe ile tengefu yetu ili tuweze kurekebisha miamba yetu kwa sababu ni makaazi ya samaki.
“Tukifunga ile sehemu, kipato chetu kitaimarika tena kama zamani. Tumeona hali ya matumbawe kule Kuruwitu inafanya vizuri,” alisema Chai.
Tengefu ya Kuruwitu imekua ikiigwa, sio tu na mashirika na taasisi mbalimbali za elimu nchini Kenya, bali pia na zile za nje ya mpaka, ambapo wanafunzi hutumwa katika eneo hilo kuendeleza masomo yao, hasa kuhusiana na masuala ya uhifadhi wa mazingira ya baharini.
Kabibi Joseph, aliyehitimu katika chuo cha Wildlife Research and Training Institute baada ya kusomea usimamizi wa wanyamapori, ni miongoni mwa wanafunzi waliopata mafunzo ya ziada katika hifadhi ya Kuruwitu.
“Nilichagua hifadhi ya Kuruwitu kwa sababu ya ukakamavu wake katika masuala ya uhifadhi na maendeleo ya jamii. Kama mtaalamu wa masuala ya wanyamapori, niliamini kuwa uhifadhi unaosimamiwa na kuendeshwa na jamii ni kigezo muhimu katika juhudi endelevu za uhifadhi. Juhudi za jamii kuhifadhi mazingira ya baharini na maendeleo ya jamii kunaendana vilivyo na malengo yangu,” Kabibi aliiambia Mongabay.
Kwa muda aliokuwa Kuruwitu, kuanzia mwezi wa Juni, 2025 hadi Desemba, Kabibi alishiriki kushika doria na wafanyakazi wengine kukagua tengefu na kuzuia mbinu zozote za uvuvi haramu. Kazi hii ilimsaidia kufahamu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira ya baharini na athari zinazotokana na shughuli za binadamu.
“Nilishuhudia wazi athari za matumizi ya zana haramu za uvuvi katika maisha ya viumbe vya baharini. Nilijifunza mambo mengi sana, ambayo yatanisaidia katika taaluma yangu, mojawapo ikiwa ni umuhimu wa kuhusisha jamii kikamilifu katika juhudi za uhifadhi.
“Pia nilijifunza kuwa kuna haja kubwa ya kuwa na mawasiliano mwafaka pamoja na kuunganisha wanajamii waliouzunguka eneo hilo, wanasayansi na washikadau wengine katika kupangilia mipango ya uhifadhi,” alisema Kabibi.
Picha ya bango: Kasa ni baadhi ya viumbe wanaopatikana katika eneo la Kuruwitu ambapo hutokea kutaga mayai. Picha na KCWA.