- Mpango wa Tanzania wa kuboresha boti za uvuvi uliolenga kuwawezesha wavuvi wadogo kwa kuwapatia vyombo vya uvuvi vya gharama nafuu, umewaacha wengi wakihangaika kutokana na kusambaziwa boti zisizo imara kwa mikopo isiyo endelevu.
- Wilayani Kilwa, wavuvi wanasema boti hizo walizosambaziwa na Serikali hazikuwa na vifaa muhimu, zinahitaji gharama kubwa za uendeshaji na zinapata hitilafu za mara kwa mara za kiufundi. Hali hii huwalazimisha wavuvi kukodi vifaa vinavyokosekana na kutumia mafuta mengi zaidi kuliko ilivyotarajiwa.
- Shinikizo la kulipa mikopo linaongezeka na kuwasukuma baadhi ya wavuvi kujiingiza katika uvuvi haramu au hatarishi, jambo linalokwenda kinyume na lengo la mradi huo la kuhamasisha uvuvi endelevu.
- Wataalamu wanaonya kuwa ukosefu wa ushirikishwaji wa kutosha, miundo ya boti isiyolingana na mazingira halisi ya uvuvi, pamoja na kutozingatiwa kwa maoni ya wananchi, huenda vikageuza mpango huo wa kisasa wa uvuvi kuwa mzigo wa muda mrefu badala ya suluhisho.
KILWA, Tanzania – Baadhi ya wavuvi katika wilaya ya Kilwa nchini Tanzania, ambao ni miongoni mwa watu wa kwanza kupokea boti za uvuvi kupitia mpango wa serikali, vyombo hivyo sasa vimegeuka kuwa mzigo na kuwatwisha gharama kubwa badala ya kuwa msaada.
Mpango huo, uliozinduliwa Novemba mwaka 2023 na Wizara ya Mifugo na Uvuvi chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, ulilenga kuboresha sekta ya uvuvi kwa kubadilisha boti za mbao zilizopitwa na wakati kwa vyombo vya kisasa vya kuvulia.
Rais Samia alipotembelea Kilwa miezi miwili kabla ya uzinduzi wa mpango huo, aliahidi kuwa wavuvi wadogo wangepewa boti hizo kupitia mikopo yenye riba nafuu. Ahadi hiyo iliibua matumaini makubwa miongoni mwa jamii za wavuvi ambazo kwa muda mrefu zimekuwa zikikabiliwa na changamoto za boti chakavu na ukosefu wa mtaji wa kununua vyombo vipya.
Ili kufadhili mpango huo, serikali ilishirikiana na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), ambayo hutoa mikopo nafuu kwa vikundi vya wavuvi. Mikopo hiyo ina viwango vya riba vya chini, inatoa muda mrefu kwa marejesho, na inajumuisha kipindi cha msamaha wa malipo cha takribani miaka mitano hadi kumi kabla ya kuanza kulipa.
“Tunatoa tangazo linalowafikia watu nchi nzima pindi boti zinapopatikana,” alisema Mohammed Sheikh, Mkurugenzi wa Uvuvi katika Wizara ya Mifugo na Uvuvi. “Vyama vya ushirika vinavyovutiwa vinatuma maombi, na vikikubaliwa, hupokea boti ambazo zinakuwa zimewekewa bima kamili na ziko tayari kwa matumizi.”
Thamani ya kila boti hutegemea ukubwa wake (kwa kawaida boti yenye ukubwa wa kati ya mita 5 hadi 14, (futi 16 hadi 46), gharama yake ni takribani shilingi milioni 80 za Tanzania (Dola 32,200 za Marekani).
Matarajio chini ya mpango huo ilikuwa kuongezeka kwa uzalishaji, kutoa ajira na kuzuia mbinu za uvuvi zinazosababisha uharibifu kama matumizi ya baruti na nyavu zenye matundu madogo. Njia hizo hunasa samaki wachanga ambao bado hawajafikia umri wa kuzaliana. Kwa kipindi hicho, idadi ya samaki ilipungua kwa sababu ya uchache wa samaki wakubwa wenye uwezo wa kuzaliana, hali iliyosababisha kuporomoka kwa uvuvi wa maeneo husika.
“Tuliamini tungepata vyombo vilivyobuniwa kwa ajili ya uvuvi wa bahari kuu, vikiwa na vifaa kamili vya usalama, jenereta na taa zinazofaa,” alisema Mbwangali Twalha, Katibu wa Kikundi cha Wavuvi cha Fikirini kilichopo Kilwa Masoko. “Ilionekana kama suluhisho la matatizo yetu.” Hata hivyo, kwa baadhi ya wanufaika wa mpango huo wilayani Kilwa, uhalisia umekuwa tofauti kabisa.

Sekta ya uvuvi nchini Tanzania inategemewa na takribani watu milioni 4.5 moja kwa moja na kwa njia zisizo za moja kwa moja. Pwani ya nchi ina urefu wa zaidi ya kilomita 1,400 (maili 870), na uvuvi unachangia takribani asilimia 1.7 ya Pato la Taifa (GDP).
Wilayani Kilwa, uvuvi ni chanzo kikuu cha watu kujikimu kimaisha. Wavuvi wengi hufanya kazi kwa kiwango kidogo, wakitumia ngalawa za mbao (vyombo vya jadi vya uvuvi), mitumbwi na nyavu za mkono. Mazao yao ya uvuvi, yakiwemo dagaa, anchovi na samaki aina ya jodari (tuna), husambazwa katika masoko ya ndani na pia kupelekwa kwenye majiji makubwa kama Dar es Salaam.
Hata hivyo, changamoto zinazowakabili wavuvi wadogo zinaendelea kuongezeka, miongoni mwake zikiwemo upungufu wa maghala ya kuhifadhia samaki wa baridi, masoko yasiyo ya uhakika, gharama kubwa za mafuta, miundombinu duni ya maeneo ya kuweka samaki baada ya kuvuliwa, pamoja na ushindani kutoka kwa meli kubwa za kibiashara.
Mabadiliko ya tabianchi yamezidisha changamoto hizo kwa kubadilisha mienendo ya uhamaji wa samaki na kuwaacha wavuvi wakiwa hatarini zaidi kutokana na matukio ya hali mbaya ya hewa yanayojirudia mara kwa mara.
Kwa mujibu wa Twalha, miaka ya hivi karibuni imeshuhudia ongezeko la matukio ya upepo mkali yanayoathiri shughuli za uvuvi. “Siku hizi, ni vigumu kupita hata miezi miwili bila kukumbwa na upepo mkali,” alisema Twalha.
Mpango wa boti za uvuvi ulianzishwa katika mwaka wa fedha wa 2022/2023 kama sehemu ya juhudi za serikali za kuboresha uvuvi wa baharini na wa ndani ya nchi. Katika awamu ya kwanza ya mpango huo, jumla ya boti 160 zilisambazwa kwa wanufaika 3,163 kote nchini, kwa gharama ya shilingi bilioni 11.5 (dola za Marekani milioni 4.6).
Mnamo Februari mwaka 2025, Rais Samia Suluhu Hassan alizindua rasmi awamu nyingine ya ugawaji wa boti, ikijumuisha boti kubwa 120 za uvuvi na boti ndogo 118, huku mkoa wa Tanga ukipokea boti kubwa 30 na ndogo 60.
Kwa mujibu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, vigezo vya kupata mkopo wa boti vinategemea mambo kadhaa: mwombaji lazima awe anajishughulisha na uvuvi, awe mwanachama wa chama cha ushirika kilichosajiliwa, na aweze kuonyesha uhitaji pamoja na uwezo wa kurejesha mkopo ndani ya muda uliopangwa.
Kama ilivyo kwa wavuvi wengine wengi, Kikundi cha Wavuvi cha Fikirini kinachoongozwa na Twalha kiliomba kupitia utaratibu rasmi; kiliandaa maombi yake, kikayawasilisha kwenye Ofisi ya Uvuvi ya Wilaya, kisha yakapelekwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Hatimaye, maombi ya kikundi yalipoidhinishwa, walipangiwa boti yenye thamani ya shilingi milioni 105 (dola za Marekani 42,200) kupitia mkopo nafuu.
Hata hivyo, boti zilipowasili miezi mitatu baada ya kuomba, matumaini yao yalianza kufifia. “Wakati tulisaini mikataba ya mkopo na benki chini ya usimamizi wa Wizara ya Uvuvi, hatukuwa tumeziona boti,” alisema Twalha. “Zilipofika, tulishtuka kuona hazikuwa na vifaa vingi tulivyoviomba.”
“Vifaa hivi ni muhimu kwa uvuvi salama na wenye tija,” aliongeza. “Bila hivyo, tunalazimika kukodi vifaa vinavyokosekana, tukilipa takribani shilingi 150,000 (dola 60 za Marekani) kwa siku”, shilingi 60,000 (dola za Marekani 24) kwa boti ndogo na taa, na shilingi 30,000 (dola 12 za Marekani) kwa jenereta.
Athari za kifedha za mradi huu zimekuwa kubwa. “Cha kushangaza ni kwamba boti hizi zililenga kupunguza gharama zetu,” alisema Twalha. “Lakini sasa zinatumia rasilimali nyingi zaidi kuliko hata boti zetu za zamani za mbao.”

Kupanda kwa gharama na matatizo ya kiufundi
Kwa wavuvi wengi, matumizi ya mafuta yamekuwa changamoto kubwa zaidi. Kwa mujibu wa Hamadi Yusufu, Katibu wa Kikundi cha Uvuvi cha Umoja Jimbiza kilichopo kijiji cha Jimbiza wilayani Kilwa, ambacho kinamiliki moja ya boti mpya, gharama za uendeshaji zimepanda kwa kasi kubwa.
“Kusafiri kutoka hapa hadi Sanje ya Kati”, kisiwa kinachotumiwa na wavuvi kama kituo cha kupumzika wakiwa baharini, “hapo awali tulikuwa tunatumia takribani shilingi 100,000 (dola za Marekani 40) kwa mafuta,” alisema na kisha kuongeza, “Sasa, safari hiyo hiyo inagharimu mara mbili ya kiasi hicho. Injini ni kubwa sana na hazifai kwa aina ya uvuvi tunaofanya.”
Changamoto za ubora wa boti zinazidisha tatizo hilo. Inaripotiwa kuwa baadhi ya boti zilipata nyufa miezi michache tu baada ya kuanza kutumika.
Rashid Mohamed Mtile, mnufaika mwingine wa mpango huo, alisema boti yake ilianza kuvuja maji miezi mitatu tu baada ya kuanza kufanya kazi. “Tuliripoti tatizo hilo, na serikali ilikubali kugharamia sehemu ya matengenezo,” alisema. “Lakini uharibifu wa aina hiyo katika muda mfupi unaonyesha wazi ubora duni wa chombo hicho.”
Hata baada ya matengenezo, Mtile alisema boti hizo bado si za kuaminika. “Kwa nje zinaonekana za kisasa, lakini kwa matumizi ya kawaida ni ngumu kuziendesha na kuzitunza.”
Zaidi ya hayo, tofauti kati ya mahitaji ya wavuvi na kile walichopewa haikuishia kwenye vifaa pekee. Baadhi ya vikundi waliomba nyavu za kulaza ndoano, mbinu inayofaa kwa maeneo yao ya uvuvi, lakini badala yake walipewa nyavu ya kuvulia moja tu, ambayo haitoshi kupata samaki wa kutosha kwa ajili ya kuuza kwenye masoko ya ndani.
Katika majibu yao kwa maswali ya Mongabay, maafisa wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) walisema kuwa wavuvi hawakuomba vifaa hivyo, na kwamba wao hutoa kile kilichoombwa.
Mwanaisha Abdallah Mpili, mwanachama wa moja ya vikundi hivyo, alisema: “Tulihitaji angalau seti 30 za nyavu ili kufanya kazi kwa ufanisi. Tulipewa moja tu. Tutavua vipi samaki wa kutosha kulipa mikopo ya zaidi ya shilingi milioni 100 (dola za Marekani 40,200)?”
Kwa wavuvi hawa, boti mpya zimegeuka kuwa mtego wa kifedha. “Masharti ya mkopo hayakuwa wazi,” alisema Twalha wa Kikundi cha Wavuvi cha Fikirini. “Hatukupewa maelezo ya kina yanayoonyesha gharama ya boti, injini na vifaa kwa kila kipengele. Bila uwazi huo, hatuwezi kuthamini mali zetu ipasavyo.”

Shinikizo la mikopo na hatari ya uvuvi haramu
Mnufaika mwingine wa mpango huo, Said Mohamed Kilimba, alisema shinikizo la kutafuta fedha za kulipa mikopo linawasukuma baadhi ya wavuvi kujiingiza katika matumizi ya mbinu haramu za uvuvi.
“Unapokwenda baharini ukijua lazima upate fedha za kulipia mafuta, posho za wafanyakazi na marejesho ya mkopo, vishawishi vya kuvunja sheria vinaongezeka,” alisema. “Wengine wameanza kutumia nyavu zenye matundu madogo au kuvua katika maeneo yaliyopigwa marufuku ili kuongeza mavuno. Sio kwa sababu wanataka kuharibu bahari, bali ni kwa sababu wanahangaika kuendelea kuishi.”
Aliongeza kuwa kutokana na gharama kubwa za uendeshaji na mavuno yasiyo ya uhakika, vikundi vingi vinajikongoja kulipa marejesho ya mikopo yao. “Boti zilipaswa kuboresha maisha yetu,” alisema Mohamed, “lakini sasa kila safari ni kama kamari. Tukirudi na samaki wachache, tunapata hasara, lakini benki bado inadai malipo.”
Alionya kuwa bila hatua za haraka kuchukuliwa, “madeni haya yanaweza kuwarudisha wavuvi kwenye tabia zilezile za uvuvi haramu ambao serikali ilikuwa inajaribu kuutokomeza.”
Leonard Pesambili, nahodha wa boti kutoka Jimbiza, aliunga mkono hoja za wenzake akisema kuwa kabla ya kupata boti mpya walikuwa wakivua karibu na pwani na kugawana kidogo walichopata. Lakini sasa, mikopo iliyowabebesha mzigo imefanya hali kuwa ngumu zaidi.
“Ikitokea kundi moja likavua zaidi, mengine yanalazimika kufuata maeneo hayo hayo, hata kama inamaanisha kuvunja mipaka ya uvuvi au kwenda baharini wakati hali ya hewa si salama,” alisema. “Ushindani umeleta migogoro kati ya makundi ya wavuvi na pia umeongeza ajali baharini.”
Kwa mujibu wa Pesambili, serikali ilikuwa na nia njema ya kuboresha sekta ya uvuvi, lakini bila mafunzo ya kutosha, ruzuku ya mafuta au bei ya haki sokoni, mikopo hii inageuza ndugu kuwa washindani.
Wasiwasi wa Pesambili ni kwamba iwapo watashindwa kulipa marejesho ya mikopo, watalaumiwa kwa makosa ambayo si yao. “Watu watasema tumeshindwa kusimamia mikopo,” alisema, “lakini ukweli ni kwamba muundo wa mradi wenyewe uliweka mazingira ya kutufanya tushindwe.”

Benki: Boti zilitolewa kama ilivyokubaliwa
Faithful Joshua, Afisa wa Huduma kwa wateja katika TADB, benki pekee inayotoa mikopo kwa wavuvi chini ya mpango huu, alisema mchakato unaanza pale Wizara ya Mifugo na Uvuvi inapotangaza mikopo kwa ajili ya boti, vifaa vya kutunzia samaki au vifaa vya kilimo cha mwani.
“Waombaji lazima wakidhi vigezo vilivyowekwa na watume maombi yao kupitia wakurugenzi wa wilaya kwenda wizara, ambayo inayapitia na kuyapeleka TADB kwa ajili ya ufadhili,” alisema.
Aliongeza kwamba boti zote zimekatiwa bima kupitia Kampuni ya Bima ya Taifa (NIC), mtoaji wa bima wa umma. Ikiwa tatizo litatokea, mnufaika anawasilisha ripoti kwa TADB, ambayo inaipeleka NIC kwa tathmini. Mara tu madai yanapoidhinishwa, NIC inalipa TADB, ambayo inamlipa mtoaji huduma kwa ajili ya ukarabati.
“Hali ilikuwa hivyo kwa Kilwa na kwa boti nyingine ambazo zilitolewa. Boti zote zilitolewa kulingana na makubaliano, na kwa njia ya uwazi kabisa,” alisema Joshua, na kisha kuongeza: “Wizara inatoa zabuni za utengenezaji wa boti na kuhakikisha boti zote zinakidhi viwango vya kitaifa kabla ya kugawanywa.”
Hata hivyo, licha ya taratibu hizi kuwepo, wavuvi wengi wa Kilwa wanasema mawasiliano kati ya wizara, mamlaka za mitaa na makundi ya wavuvi yalikuwa duni. Wanasema kwamba maelezo muhimu kuhusu aina ya boti, vifaa vya ziada na mipango ya malipo hayakuwekwa wazi kabla ya kusainiwa kwa mikataba ya mkopo.

Mpango bado uko njia panda
Maafisa wa serikali wameutetea mpango huo, wakisema kuwa wao wanaamini bado ni hatua muhimu kuelekea uvuvi wa kisasa. “Tunawasaidia wavuvi katika kila hatua,” alisema Ulimboka Ndile, Afisa wa Uvuvi wa Wilaya ya Kilwa.
Kwa mujibu wa Ndile, umiliki wa boti uko katika mifumo miwili: baadhi ya wavuvi wanamiliki boti kwa vikundi, huku wengine wakimiliki binafsi.
TADB na Wizara ya Mifugo na Uvuvi zilisema kuwa boti zote zinapaswa kukabidhiwa zikiwa na vifaa vyote kama ilivyoainishwa kwenye mikataba, na kwamba vifaa vyovyote vinavyokosekana vinapaswa kushughulikiwa kupitia taratibu za ufuatiliaji.
Hata hivyo, kwa wavuvi wa Kilwa, ahadi hizo zinaonekana hazina maana. Wanasema kile walichoahidiwa kwenye nyaraka kinatofautiana kwa kiasi kikubwa na kile walichokabidhiwa katika uhalisia.
Kikundi cha Twalha, kama vilivyo vikundi vingine, kinaendelea kuiomba serikali iwapatie wavuvi vifaa vinavyokosekana kwenye boti. “Hatuupingi mpango huu,” alisema. “Tunachotaka ni kupata vifaa tulivyoahidiwa.”
Philip Bwathondi, mtaalam wa baiolojia ya baharini na mbobevu wa masuala ya uvuvi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema tukio la Kilwa linaakisi changamoto pana zaidi katika juhudi za Tanzania za kuboresha sekta ya uvuvi.
“Mipango mingi ina nia njema, lakini mara nyingi haizingatii uhalisia wa jamii za wavuvi wadogo,” alisema. “Wakati mwingine boti hubuniwa bila kuzingatia uhalisia wa eneo husika, ufanisi wa matumizi ya mafuta au aina ya zana zinazofaa kwa samaki wanaolengwa.”
Aliongeza kuwa tofauti hizo si tu zinawabebesha wavuvi mzigo wa kifedha, bali pia zinaweza kudhoofisha uvuvi endelevu.
“Wavuvi wanapolazimika kutumia boti zisizofaa, hulazimika kuvua kupita kiasi maeneo ya karibu ya pwani ili kurejesha gharama, jambo linaloongeza shinikizo kwa mifumo ya ikolojia ya baharini ambayo tayari ni dhaifu,” alisema Bwathondi. “Mageuzi ya uvuvi yanapaswa kwenda sambamba na mafunzo, utafiti na ushirikishwaji wa kutosha wa jamii zenyewe.”
Picha ya Bango: Ngalawa ya mbao Kiwla, Tanzania. Picha na Richard Mortel kupitia Flickr (CC BY 2.0).
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 30/12/2025