- Nashulai, hifadhi ya wanyamapori iliyoko nchini Kenya, inamilikiwa na kuendeshwa na jamii ya Wamasai, na ina jumla ya hekta 2,400 za ardhi kwa ajili ya kulinda bioanuwai na kuhakikisha haki za umiliki wa ardhi.
- Wafugaji wa Kimasai hukodisha ardhi zao binafsi kwa hifadhi hii, kwa makubaliano ya kutouza ardhi hiyo kwa mtu mwingine zaidi ya mwanachama wa hifadhi mwenye madhumuni ya kuitumia kwa ajili ya uhifadhi na hawaruhusu ardhi hiyo kuzungushiwa uzio.
- Mkakati unaozungumzia ardhi ya uhifadhi uliwekwa baada ya matukio ya watu kutoka nje kuanza kununua ardhi katika kaunti hiyo, kuizungushia uzio na hivyo kuzuia maeneo ya malisho ya wanyama na mifugo.
- Hadi sasa wataalam wa uhifadhi wanasema kuwa mpango huu wa uhifadhi umeonyesha mafanikio, lakini wanafafanua kuwa mafanikio zaidi yataendelea kuonekana iwapo wamiliki wa ardhi wa Kimasai wataendelea kunufaishwa na mkakati huu na pia kujumuishwa katika maamuzi.
“Angalia, twiga wanatembea mbele yangu. Tuna mamia ya twiga katika hifadhi yetu. Kuna pundamilia pia, unaona? Na tembo pia,” Nelson Ole Reiyia anaeleza wakati wa mahojiano ya simu na Mongabay, mahojiano ambayo ilibidi yabadilike na kuwa ya video kumpa nafasi mwandishi wa habari kujionea kinachoelezwa.
Ole Reiyia ni mwanzilishi mwenza wa hifadhi ya Nashulai Maasai, iliyoanzishwa mwaka 2016 kwenye mipaka ya Hifadhi maarufu ya Kitaifa ya Maasai Mara katika kaunti ya Narok kusini mwa Kenya, karibu na mpaka wa Tanzania.
Utofauti wa hifadhi hii na zile zinazosimamiwa na serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali mashariki mwa Afrika, ni kwamba Nashulai inasimamiwa na watu wa asili wa Kimasai na ina utaratibu wake tofauti wa kuendesha shughuli za uhifadhi. Hifadhi hii yenye ukubwa wa zaidi ya hekta 2,400 (ekari 5,930) inaundwa na vipande vya ardhi binafsi vinavyomilikiwa na Wamasai walioamua kujiunga pamoja kwa lengo la kulinda mazingira na haki zao.
Wakati katika maeneo mengine nchini Kenya, umiliki binafsi wa ardhi za Wamasai umesababisha kugawanywa kwa maeneo ya malisho na kuleta athari kwenye uhifadhi, Ole Reiyia anasema hali ni tofauti katika hifadhi ya Nashulai kwani utaratibu huo umeleta mabadiliko yanayoonekana na chanya. Badala ya kuacha ardhi ikiwa imegawanywa vipande vipande, wamiliki wa ardhi waliamua kuunganisha mashamba yao pamoja.
“Eneo kubwa la Nashulai lilikuwa ni vumbi tu. Hakukuwa na nyasi kwenye ardhi,” Ole Reiyia aliiambia Mongabay. “Baada ya miaka miwili, kiwango cha nyasi kiliongezeka. Wanawake walifanya kazi na kuhakikisha mto unarejea. Waliondoa tani za taka, kisha wakishirikiana na vijana, wakapanda miche asilia kando ya kingo za mto. Kadri muda ulivyopita, hali ya asili ilianza kurejea. Wanyamapori wakarudi. Hii ni njia inayounganisha hifadhi za wanyamapori na Maasai Mara”.

Pundamilia, nyumbu na twiga: hawa ni wanyama ambao Ole Reiyia alikuwa akiwaona tangu akiwa mtoto. Lakini zaidi ya muongo mmoja uliopita, walianza kupungua kwa kasi, alisema. Hii haikuwa kwa sababu tu ya uharibifu wa malisho, bali kutokana na uzio wa nyaya za umeme uliozungushiwa maeneo ya wazi ambako wanyama huzunguka zunguka. Alisema aliwahi kushuhudia baadhi ya pundambili na twiga wakikabwa na nyaya hizo.
Licha ya athari kwa wanyama, uzio huo umekuwa mwiba wa wafugaji wa Kimasai. Kulingana na maneno ya Ole Reiyia, kadhia ya uzio ilianza baada ya wageni kununua ardhi kwenye kaunti ya Narok na kupata hati miliki na ili kulinda maeneo yao, waliamua kuzungushia uzio.
Kwa vile Wamasai kwa asili yao ni wafugaji wanaohamisha mifugo yao kulingana na misimu ya malisho, huhitaji maeneo makubwa ya wazi. Uzio huo, pamoja na ongezeko la mahitaji ya kilimo nchini Kenya, mbuga za taifa, maeneo yaliyohifadhiwa na juhudi za umiliki binafsi, yalipunguza maeneo yao ya malisho.”
Lakini kupitia mfumo wa hifadhi ya Nashulai, “mtu hupata nafasi ya kuchunga kwa uhuru katika mfumo wa ufugaji wa wazi,” anasema Joyce Mbataru, Meneja Mawasiliano wa chama kinachosimamia hifadhi nyingi nchini Kenya, au Kenyan Wildlife Conservancies Association (KWCA). Hifadhi ya Nashulai ni mwanachama wa umoja huo.

Ulinganishaji wa afya na ongezeko la uoto (NDVI) katika hifadhi ya Nashulai Maasai, kwa kutumia Sentinel-2 kupitia Copernicus, kati ya Julai 2016 na Julai 2025. Hii si taswira halisi kuhusu ukuaji wa uoto bali inatoa picha tu na pia haikuzingatia mabadiliko wakati wa kipindi cha mvua katika miaka hiyo.
“Mkija pamoja kama wamiliki wa ardhi tofauti, basi mtaendelea kuchunga kwa uhuru, na hiyo itaruhusu wanyamapori kusogea karibu. Matokeo yake, wanyamapori na mifugo, vyote vitanufaika,” anasema.
Mfumo huu ni aina nyingine ya ulinzi, anasema Kathleen Klaus, Profesa msaidizi katika Chuo Kikuu cha Uppsala nchini Uswidi, aliyebobea katika masuala ya haki za ardhi, mabadiliko ya tabianchi na uhamishaji wa lazima nchini Kenya.
“Kujenga hifadhi ya jamii kunatengeneza eneo kubwa la malisho, husaidia kuzuia uvamizi zaidi na pia ni njia mojawapo thabiti ya kudhibiti taasisi za kimataifa na kitaifa kufanya ununuzi wa ardhi yao’’.
Kuleta ardhi pamoja
Mara baada ya Kenya kupata uhuru kutoka kwa Uingereza,Wamasai walipata kiwango cha kwanza ya ulinzi kupitia Sheria ya Ardhi (Wawakilishi wa Vikundi). Wazo hilo lilihusisha kutenga kipande cha ardhi kilichorekodiwa na kusajiliwa kama ranchi na ambacho umiliki wake kisheria ulikuwa ni ule wa kikundi cha watu. Mfumo huu uliwapa Wamasai uhakika wa umiliki wa ardhi yao na pia ulizuia maeneo yao kuchukuliwa na makabila mengine.
Ranchi hizo zilisimamiwa na wakuu wa familia za Kimaasai ambao ni wazee waliojikusanya katika vikundi vya jamii. Wote wakiwa wanaume. Hata hivyo baadaye yalifanyika marekebisho ambayo yalijumuisha wanawake na watu kutoka makabila madogo katika maamuzi na umiliki. Licha ya hatua hiyo, ulinzi huo haukutosha; hali iliyosababisha watu wengi katika eneo hilo kuamua kuhamia kwenye umiliki binafsi wa ardhi.

Miaka ishirini iliyopita, ilikuwa ardhi ya jamii. Lakini walihamia kwenye umiliki binafsi kwa sababu waliogopa kwamba wajumbe wa kamati, kwa sababu walikuwa na nguvu sana, wangejitengea wenyewe ardhi kubwa, kitu ambacho kilitokea, Ole Reiyia anafafanua. “Mara nyingi, wajumbe wa kamati walikuwa na maeneo makubwa zaidi.”
Baada ya ardhi kugawanywa na kumilikiwa binafsi, kila mmiliki alikuwa huru kutumia ardhi yake kama anavyopenda.
Hata hivyo, kutokana na ukaribu wake na Hifadhi ya Taifa ya Maasai Mara, ardhi hiyo iligeuka kivutio kwa waendelezaji, na Wamasai wengi walishawishiwa kuiuza ardhi yao. Kutokana na kiasi kikubwa cha fedha walichokuwa wakiahidiwa pamoja na hali ngumu ya maisha ikiwa ni pamoja na ukosefu wa chakula, Wamaasai wengine walikubali haraka kuuza maeneo yao.
“Watu kutokana na umaskini, warubuniwa na watu matajiri waliotaka kununua ardhi kwa bei ya chini sana, bila kujali kwamba ardhi hiyo ilikuwa ni zaidi ya mali isiyohamishika. Wanawapa fedha kidogo kisha wanajenga kambi za watalii, mashamba, bila kujali kwamba ardhi hii ni muhimu sana kwa kuhifadhi bioanuwai iliyopo katika Maasai Mara na Serengeti,” anaeleza Ole Reiyia, huku akitazama hali halisi ya unyakuzi wa ardhi. “Mara Serengeti inayozalisha mabilioni ya dola. Hata hivyo, watu wa eneo hili wanaendelea kuishi katika umaskini.”
Katika nchi ambayo ubinafsishaji wa ardhi ambayo awali ilikuwa ya jamii au ikimilikiwa na vikundi, mfumo huu ulishindwa kutimiza ahadi ya kuwainua watu kiuchumi, ulileta mitafaruki katika jamii na pia uliathiri misitu na malisho ya wanyama ambao hapo awali walikuwa wakisimamiwa kijumuiya, tafiti zinaonyesha.

Hali hii ilimchochea Reiyia na wenzake kuanzisha Hifadhi ya Nashulai Maasai. “Nashulai”, neno ambalo katika lugha ya Kimaa linamaanisha mahali ambapo maelewano na kuishi pamoja kwa kuchukuliana, ndiyo mwongozo wa maisha. Hapa, ubinafsishaji wa ardhi uko tofauti kidogo. Wamiliki wa ardhi wapatao 64 wamesaini mkataba na hifadhi hiyo, wa kukodisha ardhi yao kwa kipindi cha miaka 10 kinachoweza kuongezwa, kwa malipo. Katika kipindi hicho, mmiliki wa ardhi haruhusiwi kuiuza kwa mtu yeyote isipokuwa mwanachama mwingine wa hifadhi anayetaka kuitumia kwa madhumuni ya uhifadhi, wala haruhusiwi kuizungushia uzio.
Wanyamapori ni sehemu ya historia yetu, sehemu ya utambulisho wetu,” anasema Ole Reiyia, ambaye ukoo wake unawakilishwa na mnyama aina ya fisi na ulikuwa na tamaduni zinazohusu mnyama huyo. Miaka iliyopita, fisi walikuwa wakila miili ya wanakijiji waliofariki, na jamii iliamini kuwa roho zao zingeendelea kuishi ndani ya mnyama huyo.
Badala ya kuanzisha mfuko wa ardhi ya jamii au kutumia Sheria ya Ardhi ya Kenya, wanachama walijipanga kama chama cha wamiliki binafsi wa ardhi.
“Nilikuwa nashuhudia hilo wakati nikiwa mtoto, wakati ardhi ikiwa haijagawanywa, kulikuwa na wanyamapori wengi hapo. Jamii ya Kimaasai ni kabila linalojali kuishi kijamii; hawawezi kuishi kwa utengano au kutenganishwa na mazingira,” anaeleza Ole Reiyia.

Kulingana na chapisho kuhusu ubinafsishaji wa ardhi ya Wamasai lililochapishwa katika jarida la Frontiers, mbinu tofauti zinazotumika katika ubinafsishaji wa ardhi, mara nyingi huathiri usimamizi wa rasilimali na matokeo ya uhifadhi.
Kwa mfano, katika ranchi ya kikundi ya Oloirien, eneo la Maasai Mara, umiliki binafsi wa ardhi ulisababisha ongezeko la uzio na pia ulidhoofisha usimamizi wa pamoja, wakati ranchi nyingine ilipata matokeo tofauti.
“Olgulului/Ololarashi, ambayo iliunganisha madai ya haki za umiliki binafsi wa ardhi pamoja na upatikanaji wa pamoja na usimamizi wa rasilimali za jamii, ilifanikiwa kupunguza madhara mengi ya ubinafsishaji, kama vile utegemezi wa mifumo ya zamani na mgawanyo wa rasilimali,” anaandika Gabriella Santini, mtafiti msaidizi katika kitivo cha Anthropolojia cha Chuo Kikuu cha London (UCL) na mwandishi wa chapisho hilo.
Pamoja na KWCA, kutambua mafanikio ya mfumo wa hifadhi ya Nashulai, inaona kuna haja ya kuchukua tahadhari. Kwa mfano, mmiliki binafsi wa ardhi siku moja anaweza kutaka kununua ardhi ya mtu mwingine kwa bei ya juu kuliko ile ambayo hifadhi inaweza kulipa. Ni kitu gani kitamzuia mmiliki huyo kuiuza?
“Changamoto iliyopo ni kuwa na muundo wa mgawanyo wa faida unaofanya kazi kwa kila mtu kwa lengo la kuhakikisha kila mmoja amenufaika, na kuwaleta pamoja kwenye ushiriki wa umma ili kuhakikisha kwamba kila mtu amejumuishwa katika mchakato wa kufanya maamuzi,” Mbataru anasema, “Kama ilivyo katika hifadhi nyingine, mara nyingi uendeshaji wake huwa mgumu.”

Kulingana na hifadhi hiyo, Nashulai ni makazi ya takribani pundamilia 500 (Equus quagga), nyumbu 200 (Connochaetes taurinus), maelfu ya ngiri (Phacochoerus africanus) na idadi kubwa zaidi ya twiga (Giraffa tippelskirchi), wanyama ambao wanapatikana zaidi sehemu ya mashariki ya mfumo wa ikolojia wa Mara.
Licha ya kwamba watafiti hawajakamilisha ripoti huru kuhusu idadi kamili ya wanyamapori katika hifadhi hiyo, takwimu za setilaiti zilizokusanywa na Mongabay zinaonyesha hifadhi ya Nashulai tangu ilipoanzishwa mwaka 2016 hadi mwaka 2025, imekuwa na ongezeko kubwa la uoto.
Mwaka 2020, Hifadhi ya Nashulai Maasai ilipata Tuzo ya Equator, kutoka kwa Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) kutambua juhudi za jamii katika kupunguza umaskini kupitia uhifadhi.
Kuangalia mbele
Katika kaunti ya Narok, kilimo ni njia kuu ambayo inawaingizia wananchi kipato kwa ajili ya kukidhi mahitaji yao. Zaidi ya wakazi asilimia 46 wanajishughulisha na kilimo. Hata hivyo, kutokana na mabadiliko ya tabianchi, katika kipindi cha miaka 20 iliyopita, misimu ya mvua imekuwa haitabiriki, na hali hii imeathiri upatikanaji wa mazao. Kwa mfano, mwaka 2021, kaunti hiyo ilikuwa na kiwango cha umaskini cha asilimia 34, wakati asilimia 12 ya wakazi walikabiliwa na ukosefu wa chakula. Hifadhi hiyo inajaribu kukabiliana na changamoto hizo kupitia sekta ya utalii.

Hifadhi hii huwaajiri wanajamii kama walinzi wa wanyamapori ili kuongeza kipato chao. Pia imeanzisha kituo cha elimu na mafunzo kwa ajili ya kuwaandaa kwa ajira katika sekta ya utalii, kama vile uhudumu wa hoteli, upigaji picha na usuluhishi wa masuala ya kitamaduni.
“Kuna kambi na loji nyingi sana ndani ya mbuga. Lakini nyingi haziajiri watu wa eneo hili; wanadai kwamba watu wa maeneo haya hawana ujuzi unaohitajika kupata ajira. Ukiingia tu kwenye lango la Mara, utawaona wanawake wengi wakiuza mapambo mbalimbali kwa kuyasukuma kupitia kwenye madirisha ya magari ya safari, hii ni kwa sababu hawana kipato. Hivyo, tunajaribu kubadili hali hiyo,” anasema Ole Reiyia.
Licha ya kuboreshwa kwa hali ya kifedha ya wananchi Ole Reiyia anakiri kwamba bado ni vigumu kupata ufadhili.
“Mfumo wetu wa uhifadhi si wa kuwavutia wafadhili wakubwa kwa sababu sisi ni wadogo, na tunaendeshwa na jamii. Wazo letu ni geni,” anasema. “Unawezaje kuwa na jamii zinazoishi bega kwa bega na wanyamapori? Watalii hawataki kuona ng’ombe; hawataki kuona Wamaasai; wanataka kuona vijiji vya kitalii, wanataka kuona ‘big five’, wanataka kupata hisia za enzi za dhahabu za safari za Kiafrika zilizokuwepo miaka ya 1900, unajua, ardhi zisizo na watu.”
Picha ya Bango: Wamasai wakiwa katika hifadhi ya Nashulai Maasai. Picha na Marianne Nord, kwa hisani ya Nashulai Maasai.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 01/12/2025
Nukuu:
Warrier, R., Boone, R., Keys, P., & Galvin, K. (2024). Exploring linkages between protected-area access and Kenyan pastoralist food security using a new agent-based model. Ecology and Society, 29(1). https://doi.org/10.5751/es-14455-290118
Santini, G. (2025). The Community Land Act and the subdivision of Kenya’s Maasailand’s remaining commons: implications for community conservation. Pastoralism Research Policy and Practice, 15. https://doi.org/10.3389/past.2025.14918