Mahakama inayosimamia masuala ya Mazingira na Ardhi nchini Kenya, imethibitisha uamuzi ulitolewa mwaka 2019, ambao ulibatilisha leseni ya mazingira iliyokuwa imetolewa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa kiwanda cha umeme unaotokana na makaa ya mawe cha Lamu chenye uwezo wa kuzalisha umeme wa megawati 1,050. Kwa uamuzi huo, mradi huo uliogubikwa na utata umesitishwa rasmi.
Jaji Francis Njoroge aliitupilia mbali rufaa iliyowasilishwa na kampuni ya Amu Power kwa hoja kwamba tathimini ya athari za mazingira na kijamii (ESIA) ya mradi huo, haikujitosheleza na wala haikuwashirikisha kikamilifu wananchi. Uamuzi huo umemaliza mgogoro wa kisheria wa miaka mingi na upinzani kutoka kwa wenyeji dhidi ya kiwanda hicho kilichopangwa kujengwa kwenye safu ya visiwa vya Lamu nchini Kenya. Safu hiyo ya visiwa ni eneo la Urithi wa Dunia la UNESCO lenye utajiri wa mikoko, mazalia ya nyasi za baharini na miamba ya matumbawe, ambavyo ni mhimili wa uvuvi na utalii.
Mnamo mwaka 2016, Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Mazingira ya Kenya (NEMA), ilitoa leseni ya awali ya mradi huo kwa kampuni ya Amu Power. Hata hivyo, hatua hiyo ilipokelewa kwa upinzani mkubwa kutoka kwa Save Lamu, muungano wa mashirika yapatayo 40 ya kiraia pamoja na kampeni ya deCOALonize, harakati za kikanda zinayopinga uendelezaji wa makaa ya mawe. Madai makubwa ya makundi hayo ni kwamba thathmini ya ESIA ilipuuzia athari za mradi huo kwa afya ya bayoanuai na pia ushirikishwaji wa wananchi haukuwa wa kuridhisha.
Mnamo mwaka 2019, Mahakama ya Mazingira ya Kitaifa (NET) ilifuta leseni hiyo kwa hoja kwamba utoaji wa taarifa ulikuwa duni na pia hakukuwa na ushirikishwaji wa kutosha wa wananchi kutoka jamii ambazo zingeathiriwa na mradi huo. NET ilitangaza kwamba ushirikishwaji wa wananchi ni sawa na hewa ya oksijeni inayotoa uhai kwenye ripoti ya tathmini ya athari za mradi kwa mazingira, yaani, ESIA.
Amu Power ilikata rufaa dhidi ya uamuzi wa NET
Wakili wa kampeni ya deCOALonize, ambaye pia ni mjumbe wa bodi, Omar Elmawi, aliiambia Mongabay kuwa uamuzi wa mahakama wa hivi karibuni uliothibitisha uamuzi wa NET, “unaashiria mwisho wa mgogoro wa kisheria juu ya suala hilo uliodumu kwa takribani muongo mmoja. Wananchi wa Lamu walisimama imara dhidi ya Amu Power, kampuni kubwa ya makaa ya mawe na NEMA, ambao walitaka kulazimisha mradi wa makaa ya mawe katika maeneo nyeti kiikolojia na tajiri kiutamaduni.”
“Ushindi huu ni ushahidi mkubwa kwamba wana jamii wanapoongea kwa sauti moja, sauti zao zinaweza kuhamisha milima,” aliongeza Elmawi.
Katika taarifa ya pamoja</, watetezi pamoja na deCOALonize waliutaja uamuzi huo kama ushindi wa kihistoria kwa jamii za Lamu na haki ya kimazingira.
Elizabeth Kariuki, Mkurugenzi katika shirika la Natural Justice, kituo cha kisheria ambacho ni mwanachama wa Save Lamu, aliupongeza uamuzi huo akisema umeimarisha dhamira ya katiba ya Kenya kuhusu haki ya kimazingira. “Maendeleo kamwe hayatakiwi kuwa mbadala kwa afya ya wananchi, utamaduni wala mazingira yao,” alisema.
Uamuzi huo wa mahakama unaonekana kama kiashiria cha kubalidilisha mwelekeo wa soko la makaa ya mawe katika Afrika Mashariki. Baada ya uamuzi wa NET wa mwaka 2019, Benki ya Maendeleo ya Afika, (AfDB) ilitangaza kuwa haitafadhili tena mradi huo. Mwaka 2022, AfDB ilitangaza kuwa imeacha kabisa kuwekeza katika miradi yote mipya ya makaa ya mawe.
Ili kufufua mradi huo, Amu Power italazimika kufanya ESIA mpya</ ambayo itashughulikia athari za jumla zinazoweza kutokana na kuanzishwa kwa mradi huo, ikijumuisha ubora wa hewa, mifumo ya ikolojia ya Pwani, pamoja na namna ya kutupa majivu bila kuleta madhara. Kadhalika, kampuni hiyo italazimika kuwasilisha mpango madhubuti wa kupunguza athari zinazoweza kutokea na kuonyesha ushirikishwaji wa wananchi hasa kutoka kwenye jamii za wavuvi na wafanya biashara wadogo ambao maisha yao yanategemea raslimali za baharini na urithi wa kiutamaduni wa Lamu. Taasisi zinazohusika na udhibiti zitatarajiwa kuchapisha maamuzi na njia zitakazotumika kuwezesha uchunguzi huru na wa kina.
Kwa sasa uamuzi wa mahakama umezuia kuendelezwa kwa kiwanda cha makaa ya mawe.
Picha ya Bango: Waandamanaji wanaopinga kuanzishwa kwa kiwanda cha makaa ya mawe wakiwa jijini Nairobi, Kenya. Picha kwa hisani ya DeCOALonize.