15 Oct 2025 Habari Fupi za Waanzilishi
Alizaliwa katika misitu ambayo baadaye ingekuwa sehemu muhimu ya maisha yake. Katika Bonde la Kilombero, nchini Tanzania, ambako ukungu hushuka kutoka Milima ya Udzungwa, kijana Aloyce Mwakisoma alijifunza majina ya mimea kabla hata ya kujua majina ya kisayansi ya mimea hiyo kwa lugha ya Kilatini.
Baba yake, ambaye hapo awali alikuwa mwindaji, aligeuka kuwa msaidizi wa watafiti baada ya uwindaji kupigwa marufuku katika miaka ya 1990, akiwaongoza wanasayansi kupitia msitu wenye kijani kibichi kama maficho. Aloyce alimfuata, akijifunza lugha ya sayansi pamoja na hekima ya kale ya wazee wa Kihehe, ambao kwao kila mmea ulikuwa na jina, matumizi, na hadithi yake.
Akiwa mvulana, alikuwa akifuatana na baba yake na wanasayansi waliokuwa wakitembelea eneo hilo msituni, akisikiliza majadiliano yao kuhusu spishi na vipimo, huku yeye akikumbuka majina ya kienyeji na magonjwa ambayo kila jani au mzizi ungeweza kutibu.
Baadaye, yeye mwenyewe alikuja kuwa mtafiti msaidizi. Wakati fulaini, alipokuwa akifuatilia tumbili wekundu wa Udzungwa kwa ajili ya utafiti, chui aliruka kutoka kwenye vichaka na kumkamata tumbili jike akiwa umbali wa mita chache tu kutoka alipokuwa amepumzika, tukio hilo lilimkumbusha hali halisi ya pori na maajabu yasiyotabirika ya msitu alioufahamu vizuri.

Kadri miaka ilivyopita, ndivyo alivyoendelea kujiimarisha hadi akawa mmoja wa wataalamu wa mimea na utafiti wanaoheshimika zaidi katika Milima ya Tao la Mashariki, safu ya milima yenye wingi wa viumbe hai iliyoenea kote Tanzania. Uelewa wake wa kina, uliosheheni maarifa ya kiasili kuhusu maisha ya msituni, ulimfanya awe mtu wa kuaminiwa na kutegemewa zaidi na wanahifadhi. Aliweza kutofautisha mamia ya spishi kwa kugusa au kunusa, akikumbuka matumizi yake ya tiba asilia na majina ya kienyeji yaliyohifadhi kumbukumbu za uhai wake.
Wanasayansi waliokuwa wakifanya naye kazi bega kwa bega, akiwemo Andrea Bianchi, walitegemea maarifa yake sawa na walivyotegemea vifaa vyao vya kisayansi. Wakati wanasayansi walipotambua mti mpya mkubwa wa msitu wa mvua, unaojulikana kwa kitaalamu kama Tessmannia princeps, ni maarifa ya Mwakisoma kuhusu misitu yaliyosaidia kuthibitisha ugunduzi huo.
Alikuwa amepata ajira ya kuaminika ya kurekebisha misitu ya Udzungwa, kazi ambayo ilihitaji atumie kila alichokijua: ni miti ipi inayohitaji vivuli ili kustawi, ni matunda gani yanayokomaa mapema, na ni mbegu zipi zinazosubiri moto au mvua. Siku chache kabla ya harusi yake, alikufa katika ajali ya basi iliyotokea karibu na eneo la Sanje, akiwa na umri wa miaka 45. Ameacha watoto watano, mwenzi wake aitwaye Salma, na misitu ambayo bado imebaki na alama zake.
Alichokiacha nyuma hakikuwahi kurekodiwa kwenye vitabu, lakini kinaishi ndani ya misitu aliyosaidia kurekebisha na maarifa aliyoshirikisha,ushahidi kwamba uelewa wa mtu mmoja, ulioota mizizi mahali fulani, unaweza kusaidia misitu kudumu.
Picha ya Bango: Aloyce Mwakisoma. Picha na Andrea Bianchi
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 15/10/2025.