- Uchunguzi wa setilaiti unaoendeshwa na akili bandia,yaani AI,umegundua kuwa idadi ya nyumbu wanaohama katika mataifa ya Kenya na Tanzania kila mwaka inaweza kuwa chini ya nusu ya idadi ya milioni-zaidi ambayo inapigiwa debe na wengi.
- Waandishi wa utafiti walisema matokeo yao yanasisitiza haja ya kurekebisha matokeo kutoka kwa mbinu mbalimbali za uchunguzi ili kukadiria kwa usahihi idadi ya nyumbu.
- Uhamaji wa nyumbu ni mojawapo ya uhamaji mkubwa zaidi wa mamalia duniani, huku wanyama hao wakihama kilomita 800 (maili 500) kutafuta nyasi nzuri.
- Kukadiria idadi sahihi ya nyumbu wanaohama ni muhimu ili kufuatilia idadi ya wanyama hao licha ya upotevu wa makazi na kuongezeka kwa uwepo wa binadamu.
Iwapo umetazama filamu maarufu ya The Lion King, pengine unakumbuka tukio ambalo Mufasa anaanguka na kuvyogwa na kundi kubwa la nyumbu wanaokanyagana. Katika maisha halisi, kama mojawapo ya uhamaji mkubwa zaidi wa mamalia duniani, kuna shughuli nyingi kama ilivyo kwenye skrini.
Hata hivyo, uchunguzi wa hivi majuzi wa satelaiti unaoendeshwa na akili bandia, yaani AI, uligundua kuwa idadi halisi ya nyumbu wanaohama katika mfumo ikolojia wa Serengeti-Mara inaweza isiwe juu kama idadi ya milioni-na zaidi iliyotajwa sana kwa nusu karne iliyopita.
Utafiti uliochapishwa katika jarida la PNAS Nexus ulielezea jinsi timu ya wanasayansi walitumia picha za satelaiti na mifano ya kujifunza kwa kina ili kupata “chini ya watu 600,000 – takriban nusu ya makadirio yaliyotajwa sana ya nyumbu – milioni 1.3, ambayo haijabadilika sana tangu miaka ya 1970.”
“Hatujaribu kusema kwamba kuna idadi ya nyumbu 700,000 ambao wamekufa au kwamba wamepotea,” Isla Duporge, mmoja wa waandishi wakuu wa utafiti huo na mshirika wa udaktari katika Chuo Kikuu cha Princeton huko Marekani, aliiambia Mongabay katika mahojiano ya video. “Tulishangaa kupata idadi chache zaidi ikilinganishwa na matokeo ya uchunguzi wa anga. Tunafungua tu swali la kwa nini mbinu tofauti hutoa matokeo tofauti.”
Nyumbu, pamoja na pundamilia na wanyama wengine, hufuata mvua na kuhama kwa njia ya duara kupitia nchi za Kenya na Tanzania. Wanasafiri kilomita 800 (maili 500) wakati wa kila mzunguko wakitafuta maeneo yenye lishe bora na nyasi. Uhamaji huo ni muhimu kwa mfumo wa ikolojia kwani wanyama hurutubisha udongo wakiwa safarini.
Pia hutumika kama chanzo muhimu cha chakula kwa wanyama wanaowinda wanyama wengine katika mazingira, wakiwemo simba, mamba na fisi. Hii inafanya kuwa muhimu kufuatilia idadi ya wanyama hawa wanaotembea katika mazingira, hasa katika kukabiliana na kuongezeka kwa ujangili na kuwepo kwa binadamu.
“Ni muhimu tujaribu kupunguza kiwango cha mwisho ambapo kiwango cha kuzaliwa kimeshuka chini ya idadi fulani,” Duporge alisema. “Sasa ni muhimu zaidi kukuza mbinu za kufuatilia bora mabadiliko ya idadi yao.”
Kwa muda mrefu, uchunguzi wa angani ulitumika kuhesabu idadi ya nyumbu. Hata hivyo, uwanja wa mtazamo wa mbinu hiyo umeekewa vikwazo, kwa kuwa ndege hujongea katika njia zilizonyooka, kama vile mashine ya kukata nyasi. “Wanahesabu idadi ya wanyama wanaowaona kwenye njia, na kisha kuwaweka kwenye eneo kubwa zaidi,” Duporge alisema. “Hatahivyo, pamoja na satelaiti kwenda kwenye njia isiyobadilika ya obiti, kimsingi inachukua picha kubwa sana ya uso wa Dunia.”


Ili kuwafunza mifano hio miwili, Duporge na timu yake walitumia picha 70,000 zilizofafanuliwa za nyumbu kutoka kwa utafiti mwingine waliofanya hapo awali. Kisha walituma ombi la picha za satelaiti kunaswa katika mwezi wa Agosti mwaka wa 2022 na mwaka wa 2023 katika eneo la kilomita za mraba 4,000 (maili za mraba 1,540).
Mfano mmoja ulifunzwa kumtafuta na kumtambua mnyama huyo kama kitu kilicho kamili. Mfano wa pili ulizoeshwa kutambua milia iliosimama wima kwenye nyumbu ambaye anaonekana kama nukta nyeusi katikati ya mwili wa mnyama. “Nambari kutoka kwa mifano yote miwili inafanana kabisa kutokana na wakati unatazama kiwango hiki cha picha chini,” Duporge alisema.
Kwa kuzingatia tofauti kubwa kati ya matokeo yao na nambari kutoka kwa tafiti zilizopita, Duporge alisema hatua muhimu inayofuata itakuwa ni ya kuzingatia kurekebisha mbinu hizo mbili. “Tutarekebisha uchunguzi wa angani dhidi ya uchunguzi wa satelaiti ili kusuluhisha upendeleo wa makosa katika njia zote mbili,” alisema.
Ingawa mbinu mwafaka itakuwa kuangazia zaidi nyumbu, changamoto katika kupata vibali humaanisha kuwa wanaweza kuzingatia spishi nyingine, uwezekano wa vifaru, ili kulinganisha mbinu hizo mbili.
Wakati huo huo, Duporge alisisitiza jinsi mseto wa data za setilaiti na teknolojia ya akili bandia zinaweza pia kutumika kukusanya data zenye mambo mengi kama vile mifumo ya pamoja ya tabia, mipangilio wa mifugo na ujumlisho. Aliongeza kuwa kutoa mafunzo kwa watu zaidi katika mashirika ya serikali na mashirika ya uhifadhi wa wanyamapori pia kutasaidia kuongeza kazi kwa haraka zaidi.
“Ninaamini ni jambo la kimantiki kuwa sasa kwa sababu maazimio ya muda na anga ya satelaiti yanakuwa mazuri,” Duporge alisema.
Picha ya bango: Kundi la nyumbu. Uchunguzi wa satelaiti unaoendeshwa kupitia akili bandia uligundua kuwa idadi ya nyumbu wanaohama ni ndogo mno kuliko ile milioni 1.3 inayokadiriwa na watu wengi. Picha na Charl Durand kupitia Unsplash (Kikoa cha Umma).
Abhishyant Kidangoor ni mfanyikazi mwandishi katika Mongabay. Mpate mtandao wa kijamii wa 𝕏 @AbhishyantPK.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 03/10/2025