- Uharibifu wa mikoko unadhoofisha kwa kiasi kikubwa ulinzi wa maeneo ya pwani ya Kenya, huku ukiziacha kwenye hatari ya mmomonyoko wa ardhi, mawimbi makubwa ya dhoruba, na kuongezeka kwa kina cha bahari.
- Hali hii huvuruga mifumo ya ikolojia ya baharini, kupunguza idadi ya raslimali za samaki na pia husababisha kupungua kwa bioanuwai — na kuathiri vyanzo vya maisha vya wakazi wa maeneo ya pwani.
- Shirika la Marekani la Seatrees linafanya kazi kwa kushirikiana na Jumuiya ya Hifadhi ya Mazingira ya Kijamii (COBEC) pamoja na wakazi wa Marereni kwa lengo la kurejesha na kulinda mifumo ya ikolojia ya pwani na baharini, kama sehemu moja ya suluhisho dhidi ya majanga yanayoletwa na mabadiliko ya hali ya hewa.
- Tangu mwaka 2024, Seatrees imewapa wafadhili fursa ya kununua kile wanachokiita “vitalu vya bioanuwai” kwa dola 3 kila kimoja, ambapo kila kitalu huwakilisha hatua moja ya uhifadhi; kupanda mti mmoja wa mikoko huko Marereni. Kazi hii ni zaidi ya kupanda miti tu, kwani imewawezesha wana jamii kugeuza urejeshaji wa mikoko kama chanzo cha kipato kwa kuanzisha na kutunza vitalu vya miche — na wengine kuanzisha biashara ndogo ndogo kwa kutumia kipato hicho.
MARERENI, Kenya — Jua kali la alasiri linawaka kwenye mandhari kame ya Marereni, kaunti ya Kilifi nchini Kenya, ambako chumvi na bahari huathiri ardhi na maisha yanayoitegemea. Eneo hili lijulikano zaidi kwa shughuli za uchimbaji chumvi, lipo katikati ya ukanda wa chumvi wa pwani ya kaskazini mwa nchi. Hata hivyo, zaidi ya kung’aa kwa mabwawa ya chumvi, Marereni pia ina mojawapo ya mifumo ya ikolojia muhimu zaidi pwani: misitu ya mikoko ya ufukweni, ya mtoni, na ya vijito ambayo husaidia bioanuwai nyingi.
Hii ndiyo mandhari ya kuvutia ya eneo la miradi ya urejeshaji inayolenga kufufua mikoko hii muhimu — pamoja na jamii zinazoiangalia na kuitunza.
Habari kutoka kwa Mpango wa Kitaifa wa Usimamizi wa Mikoko wa serikali ya Kenya 2017-27 imebaini jinsi katika miaka ya hivi karibuni eneo la Marereni lilivyoshuhudia kupungua kwa mikoko kutokana na shinikizo la mashamba ya chumvi yanayotumia nishati ya jua, ufugaji wa samaki, na hali kadhalika ujenzi wa nyumba.
Mpango huo umesisitiza kwamba upungufu wa mikoko unadhoofisha ulinzi wa pwani, na fukwe kuathirika zaidi kutokana na mmomonyoko, mawimbi ya dhoruba, na kupanda kwa kina cha bahari. Hili si tu linaongeza hatari kwa maeneo ya bara na miundombinu kutokana na hatari za mabadiliko ya tabianchi, bali pia linavuruga mifumo ya ikolojia muhimu ya baharini, uharibifu maeneo ya kuzaliana na kulelea samaki, kaa na viumbe wengine, hali inayosababisha kupungua kwa raslimali za samaki na bioanuwai.
Kwa jamii za pwani, kama zile za Marereni, upotezaji wa mikoko ni tishio kuu la maisha yao, kwani wengi wao wanategemea mifumo ya ikolojia ya mikoko kwa uvuvi, kuni, vifaa vya ujenzi, na huduma nyinginezo. Wakati mikoko inapungua, fursa za kunufaika kiuchumi pia hudidimia, na hivyo kusababisha kuenea kwa umaskini na ukosefu wa chakula.

Tangu mwaka 2022, shirika moja la Marekani lisilo la kibiashara, linalojulikana kama Seatrees (awali likijulikana kama Sustainable Surf/SeaTrees) limekuwa likishirikiana na wanajamii huko Marereni ili kurejesha na kulinda mifumo ya ikolojia ya pwani na baharini, kama suluhisho la asili la mabadiliko ya hali ya hewa.
Kabla ya Marereni, shirika hili lilifanya kazi kama hii kuanzia mwaka 2020 katika eneo la Mida Creek, huko Pwani. “Kama mvuvi, niliona faida ya kujiunga na mpango huu,” anasema Emmanuel Gona, mkazi wa kijiji cha Muyu wa Kae, katika eneo la mradi wa Marereni, na ambaye amefanya kazi hizi tangu 2020. “Kurejesha na kupanda mikoko husaidia kuzidisha idadi ya samaki, hatua ambayo inawezesha uwepo wa mapato kwa watu kama mimi”.

Miradi mingi ya Seatrees kote duniani imefanikiwa kutokana na ufadhili wa njia za jadi, pamoja na michango ya mashirika, watu binafsi na ruzuku. Hata hivyo, mnamo mwaka 2024, Seatrees iliamua kuwapa wafadhili fursa ya kununua “vitalu vya bioanuwai” kwa dola 3 kila kimoja, ambapo kila kitalu kiliwakilisha hatua moja ya uhifadhi kama vile kupanda mti mmoja wa mikoko huko Marereni.
Seatrees imetangaza “vitalu” hivyo kama sehemu ya programu ya kwanza duniani ya kukopa bioanuwai ya baharini, iliyo na uwezo wa kurejesha na kulinda mifumo ikolojia ya baharini, ambayo kihistoria haijazingatiwa vya kutosha katika mambo ya ufadhili wa uhifadhi.
Bahari ni zaidi ya asilimia 70 ya ulimwengu na ina jukumu muhimu katika kudhibiti hali ya hewa ya dunia. Hata hivyo bahari haijapewa kipaumbele katika ufadhili wa uhifadhi wa kimataifa. Ripoti ya Umoja wa Mataifa ya 2022 imeonyesha kuwa maeneo yaliyohifadhiwa baharini duniani kote yamekuwa yakipokea takribani dola za Marekani 980 kila mwaka — ambayo ni sawa na asilimia 4 ya dola za Marekani bilioni 23 zinazotengwa kwa maeneo yaliyohifadhiwa nchi kavu kila mwaka.

“Kwa sasa ulimwengu umekumbwa na mgogoro wa mabadiliko ya tabianchi na upotezaji wa bioanuwai, mambo ambayo yanaingiliana. Hata hivyo, bahari haina nafasi kubwa katika hadithi hiyo,” anaeleza Michael Stewart, mkurugenzi na mwanzilishi mwenza wa Seatrees.
Dhana ya mikopo ya bioanuwai ya baharini inakuja kufuatia kuanzishwa kwa programu za mikopo ya bioanuwai katika maeneo ya nchi kavu, ambazo zilitengenezwa hivi karibuni, na sasa zinafadhili miradi kama vile uhifadhi wa misitu na urejeshwaji wa makazi ya viumbe mbalimbali. Programu hizi hufanya kazi kwa kutoa thamani ya kifedha kwa matokeo ya uhifadhi yanayoweza kupimika, na hivyo kuwaruhusu wanunuzi kuunga mkono mafanikio maalum ya bioanuwai kwa kubadilishana na mikopo ya bioanuwai iliyosanifiwa.
Makampuni au watu binafsi wanaweza kutumia mikopo hii kufikia malengo ya hiari ya kimazingira au kuonyesha kujitolea kwao kwa usimamizi wa bioanuwai.
Hata hivyo, programu hii imekumbwa na utata katika utaratibu wa ufadhili wake, huku wakosoaji wakisema kuna hatari ya kuwa chombo cha kujionyesha kuwa na mwamko wa kimazingira bila vitendo halisi, endapo haitasimamiwa kwa uangalifu mkubwa, na inaweza pia kupotosha juhudi kutoka kwenye hitaji la kuwa na kanuni madhubuti na hatua za moja kwa moja za kulinda mazingira. Pia kuna utata kubaini tofauti kati ya mikopo ya bioanuwai ya Seatrees na michango ya mtandaoni.
Mwanzilishi mwenza na mkurugenzi wa Seatrees, Kevin Whilden, alipoulizwa lengo la mradi wao alisema ulikuwa kuhamisha ufadhili wa uhifadhi kutoka kwenye michango ya mara moja, na kuelekea mfumo wa muda mrefu, ambao pia unaoweza kupanuka.
“Badala ya kuzingatia mipango ya upandaji miti au urejeshaji wa miamba ya matumbawe kama miradi iliyotengwa, hivi vitalu vyetu vinahimiza usimamizi endelevu, kama vile Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs)”.
Kufikia sasa, Seatrees imetoa mikopo ya bioanuwai ya baharini 300,000 Marereni. Mikopo hiyo ina thamani ya Dola za Marekani 900,000 kupitia wanunuzi binafsi pamoja na makampuni madogo. Kulingana na hesabu ya Seatrees, mapema mwaka 2025, tayari shirika hilo lilikuwa limepanda miti 190,000 ya mikoko, huku miti zaidi 30,000 ikipandwa kila mwezi. Seatrees ilikadiria kuwa vitalu vyote 300,000 vya bioanuwai ya mikoko vingekuwa vimepandwa kufikia Julai 2025.

Kurejesha mikoko ya Marereni
Kijijini Muyu wa Kae, mvuvi anatayarisha wavu wake kivulini mwa mnazi unaoyumba yumba, huku upepo ukivuma. Kando ya pwani, boti za mbao zimetulia kwenye unyevu unyevu, zikingoja kurudi kwa wimbi. Kaa wadogo wadogo waonekana wakitambaa ndani na nje ya mashimo yao kwenye sehemu ya bahari iliyo wazi karibu na miti ya mikoko.
Muyu wa Kae iko ndani ya eneo la urejeshaji la Seatrees, ambalo linashughulikia hekta 600 (ekari 1,483). Hapa kazi hufanywa kwa ushirikiano na Jumuiya ya Hifadhi ya Mazingira ya Kijamii (COBEC). Seatrees hutuma ufadhili kwa COBEC ili itekeleze miradi Kenya. (Pia kuna vikundi viwili ambavyo vinashirikiana kupanda mikoko kule Mida Creek, lakini sio sehemu ya mpango wa mikopo ya bioanuwai ya baharini).
Licha ya kupanda miti, COBEC hufanya kazi moja kwa moja na jamii, kwa minajili ya kuhakikisha kuwa juhudi za urejeshaji zinawanufaisha. “Huwezi kutekeleza miradi ya uhifadhi bila ushiriki wa jamii,” Edward Mwamuye, meneja wa programu wa COBEC, anasema. “Tunawekeza katika programu za kuboresha maisha kama vile kilimo bora, ufugaji nyuki, na biashara ndogo ndogo”.

Kupitia vikundi walivyounda wao wenyewe, wanajamii hubadilisha urejeshaji wa mikoko kuwa riziki kwa kuanzisha na kuendeleza vitalu vya mikoko. COBEC na Seatrees huwapa vikundi baadhi ya vifaa vinavyohitajika ili kukuza vipandikizi na kuvitunza kwa miezi kadhaa hadi viwe tayari kupandwa. Baadaye COBEC hununua miche hiyo ili kuitumia kwenye maeneo yake ya mradi ya Seatrees, ambapo mikoko imeharibiwa na watu wanaokata miti ili kupata kuni, vifaa vya ujenzi wa nyumba, mchanga au malisho ya mifugo.
Vitalu pia huuzwa kwa mashirika mengine. Baadhi ya vikundi hutumia mapato kutoka kwa uuzaji wa vitalu kuanzisha biashara ndogo ndogo kama vile ufugaji wa mbuzi.
Kwa sasa kuna zaidi ya vikundi 30 vya mradi Marereni vinavyohusisha wanajamii 640 (wanaume 218, na wanawake 422). Vikundi hivi hulima spishi nne za mikoko asili ya pwani ya Kenya, ambayo kitaalam inajulikana kama Rhizophora mucronata, Avicennia marina, Ceriops tagal, na Bruguiera gymnorrhiza. Mpango huu umekuwa chanzo cha kipato kwa wanajamii wanaoshiriki.

Zena Hamisi, mwenyekiti wa Kundi la Wanawake wa Kiislamu la Neema huko Mto wa Mawe Creek, Marereni, anasema mradi huo umeinua wanachama. “COBEC imetushika na kutuunga mkono hadi kufikia mahali ambapo sasa tunapata kipato,” anasema. Mche huuzwa kwa shilingi 20 (takriban $0.15). Nusu ya mapato hugawanywa kati ya wanachama wa kikundi, na kiasi kilichosalia huwekwa kwenye akaunti ya akiba ili kudumisha miradi inayoleta kipato. Kwa mfano, Hamisi anasema wao walitumia akiba yao kununua mashine ya kukoboa mahindi, ambayo huikodisha kwa wakulima misimu ya mavuno.
Anasisitiza athari za urejeshwaji wa mikoko kwenye maisha ya wenyeji, hasa uvuvi: “Chanzo kikuu cha mapato kwa wakaazi Marereni ni uvuvi, na kila mikoko inapopungua, idadi ya samaki waliovuliwa pia hupungua. Tangu tuanze hizi juhudi za urejeshaji, tumeona uboreshaji”. Hata hivyo, tatizo la ukataji haramu wa mikoko bado lipo, na anasizitiza uelimishaji zaidi wa wanajamii. “Baadhi yao wanajua kuwa ni kosa, lakini bado huikata wakiamini itaota upya”.

Hamisi anapendekeza ushiriki zaidi ili kuzidisha ufanisi wa kazi ya Seatrees na COBEC. “Wanajamii wengi zaidi wanapaswa kuelimishwa, kutembelea hifadhi mara kwa mara, kufuatilia maendeleo na kutuunga mkono katika miradi ya muda mrefu kama vile ufugaji kaa kwenye mabwawa”.
Hamisi anaonya kuwa miradi ya mazingira ina muda maalum. “Ni hatua gani hufuata kukombolewa kwa miti? Miradi kama vile ufugaji kaa inaweza kuwapa vizazi chanzo endelevu cha kipato”.
Mojawapo ya mikakati ambayo Seatrees na COBEC hutumia kupunguza ukataji miti haramu, ambayo ni kikwazo kikubwa cha urejeshaji wa mikoko, ni kutoa udhamini chini ya mpango unaojulikana kama Treeducation Scholarship Fund. Huu mpango hutoa udhamini 300 kwa muda wa miaka 10 kwa wanajamii wa eneo hilo, kwa lengo la kusaidia ada za shule na uanzishwaji wa mashamba ya miti ya kukata mbao. Hii itawezesha kukuzwa kwa miti isiyo ya mikoko ambayo inaweza kukatwa kama chanzo cha mapato, na hivyo kuwa na misitu endelevu ya mikoko.
“Nia yetu ni kudumisha na kupanua mfuko wa elimu katika muda wote wa mradi wa vitalu vya bioanuwai, yaani ndani ya miaka 10,” anasema Orion McCarthy, kiongozi wa sayansi wa Seatrees.
Gona, mvuvi kutoka Muyu wa Kae, anasema kabla ya juhudi za urejeshaji, wavuvi walikuwa wakipata samaki wanaogharimu shilingi ya Kenya 500 (chini ya dola za Marekani 4) kwa siku. Hivi sasa wanapata kati ya shilingi ya Kenya 900 na 1,000 sawa na dola za Marekani 7.75. “Uboreshaji uko wazi, hasa ukienda kuvua samaki usiku,” anasema Gona.
Utafiti umebaini kuwa mikoko huboresha jamii za samaki na krasteshia. Hata hivyo, Gona anasemaushiriki wa wanaume katika juhudi hizi bado ni mdogo. Katika kikundi chake kuna wanaume 10 tu na wanawake 27.
“Baadhi ya wanaume huona kazi hii kama ya wanawake au watu wavivu. Katika kikundi chetu, hata tukiuza miche 3,000, kila mwanachama hupata takriban shilingi za Kenya 1,000 ambayo ni chini ya dola za Marekani 8, pesa ambayo haitoshi. Ni muhimu kuwa na njia mbadala za kujikimu”. Anapendekeza kuwepo kwa mawasiliano bora kuhusu umuhimu wa mradi na motisha bora za kifedha ili kuwahimiza wanaume wengi zaidi kujiunga.

Kupima na kufuatilia
Seatrees hutathmini uboreshaji wa bioanuwai na mafanikio ya kazi ya urejeshaji katika maeneo yake ya mradi Marereni na Mida Creek kwa kutumia “kikapu cha metriki”. Hii ni pamoja na tafiti za shambani zinazofanywa na wafanyakazi ambao COBEC imewandisha kupima utofauti wa spishi za mikoko, msongamano wa mizizi, kifuniko cha matawi, msongamano wa miti midogo, na urefu na kipenyo cha mikoko ndani ya viwanja vya mita 10 kwa mita 10 (futi 32 kwa futi 32) vya uwakilishi, kila kimoja kikiwa na takribani miche 200, ili kukadiria biomasi iliyo juu ya ardhi. Wao pia hutathmini utofauti na wingi wa kaa na konokono. Doria za skauti zinahudumia hadi hekta 1,248 (ekari 3,084).
Licha ya hayo, Seatrees imeshirikiana na kampuni ya Ocean Ledger, iliyo London, Uingereza, kuchambua picha za satelaiti zinazoonyesha urefu, kifuniko cha matawi, na biomasi iliyo juu ya ardhi ya miti ya mikoko katika eneo kubwa zaidi kuliko lile ambalo COBEC inaweza kufikia ardhini. Vyanzo hivi viwili vya data — tathmini za shambani na data za satelaiti — hutumika pamoja, huku kila kimoja kikithibitisha na kuimarisha matokeo ya kingine. Julius Sila, ambaye ni mratibu wa urejeshaji mikoko na mtaalamu wa GIS katika COBEC, asema tathmini hufanyika kabla na baada ya kazi hizo za urejeshaji.
Viwango vya msingi huwekwa kutumia data ya kulinganisha kutoka maeneo ya karibu ambayo yanachukuliwa kuwa safi dhidi ya yale yaliyoharibiwa zaidi. Kisha, anasema, “baada ya urejeshaji, tutatembelea maeneo hayo kila mwaka ndani ya kipindi cha miaka 10], tukitumia viwanja vilivyoteuliwa vya mita 10 kwa 10 kwa ufuatiliaji wa muda mrefu. Kulinganisha data hizi kwa muda inatuwezesha kubaini kiwango cha uboreshaji wa bioanuwai”.
Ikiwa watapata viwango vya ustawi, eneo hilo litapandwa upya na miche mipya ya mikoko kuchukua nafasi ya ile iliyoshindwa kustawi. Data ya msingi kwa eneo la Marereni ilikusanywa awali kati ya Mei na Septemba 2024, kabla ya upandaji kuanza Oktoba. Mzunguko wa kwanza wa ukusanyaji wa data ya bioanuwai imepangwa Oktoba 2025, na matokeo yanatarajiwa mapema 2026. Matokeo yatatolewa kwa umma.
Utafiti wa mwaka 2022 ulibaini kuwa licha ya uwekezaji mkubwa katika urejeshaji mikoko duniani, viwango vya kustawi kwake bado viko chini kutokana na uteuzi mbaya wa maeneo, ushiriki duni wa jamii husika, na upandaji katika ardhi isiyofaa yenye maji mengi au mchanga.
Hata hivyo, Seatrees na COBEC wameripoti kiwango cha kustawi cha karibu asilimia 80 kwa mikoko waliyopanda. Sila anasema matokeo haya yamewezeshwa na kushughulikia masuala kama vile chanzo cha uharibifu, kulinganisha spishi na hali sahihi za eneo, na pia kutumia tathmini za kisayansi kama vipimo vya chumvi ya udongo kabla ya upandaji. “Haya yote yakishughulikiwa, huwa kuna mafanikio,” Sila anasema.

Changamoto za mradi
Kulingana na Sila, hali halisi Marereni ina changamoto, ikiwemo mabadiliko ya kihaidrolojia au maji. “Mikoko hustawi pasipo na mawimbi mengi, ila ubadilishanaji wa maji mara kwa mara kutoka baharini,” anasema. “Hata hivyo, mchanga umebadilisha ikolojia ya vijito hivi, na kudhoofisha mchakato wa urejeshwaji”.
Shida huwa wakati maji ya kijito yanapotuama kutokana na kuzibwa kwa njia, na kuzuia mtiririko wa mawimbi ipasavyo. “Kawaida mikoko huwa imezama majini kwa takriban saa sita katika kipindi cha mawimbi. Hata hivyo, mabadiliko ya maji na mchanga yamefanya baadhi ya vijito kuziba na kusababisha kutuama kwa maji au hata kukauka kwa mikoko,” Sila anasema. Maji yaliyotuama, yakiambatana na joto kali na uvukizi, yamesababisha uwepo wa chumvi nyingi, ambayo inaweza kukausha mikoko. Isitoshe, mmomonyoko wa fukwe umesababisha kutawanyika kwa mchanga na hata kufunikwa kwa maeneo yaliyopandwa, na kuzuia ukuaji wao.

Suala lingine lililopo ni uchafuzi kutokana na uvujaji kutoka mabwawa ya chumvi yaliyo karibu, ambayo pia yanapakana na msitu wa mikoko Marereni. “Kwa sasa, sio mabwawa yote yanakidhi viwango vinavyohitajika kisheria. Kwa sabsabu hiyo, kuna uvujaji chini ya ardhi, ambao unaathiri vibaya mazingira, ikiwa ni pamoja na mikoko,” Sila anasema, akiongeza kuwa ukosefu wa fedha umezuia kushughulikiwa kwa masuala hayo. Licha ya changamoto hizi, Seatrees na COBEC wamedhamiria kuendelea kujitolea kurejesha misitu ya mikoko ya Marereni na kuhakikisha uendelevu wa muda mrefu. Wananchi katika eneo hilo nao wamekubali kuendelea kujitolea.

Picha ya bango: Mvuvi na skauti wa jamii ya Muyu wa Kae, kijijini Marereni, Emmanuel Gona anaamini kuwa kuhifadhi na kurejesha mifumo ya ikolojia ya mikoko, ni jambo la msingi katika kuongeza idadi ya samaki baharini. Picha na Juliet Ojwang.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya kiingereza mnamo tarehe 01/07/2025.