- Asilimia 60 ya nguvukazi ya Afrika imeajiriwa kwenye kilimo. Wataalamu wanasema kuwa hiyo ni sababu ya kutosha ya kuwawezesha kupata nishati mbadala ili kuongeza uzalishaji wa chakula na kufikia lengo la usalama na uhakika wa chakula.
- Taasisi ya Rasilimali za Ulimwengu (The World Resources Institute (WRI) inashirikiana na wadau mbalimbali na watunga sera ili kuhamasisha muunganiko wa nishati jadidifu kusaidia wakulima wadogo.
- Taasis ya Uzalishaji Wenye Tija wa Matumizi ya Nishati Jadidifu (The Productive Use of Renewable Energy (PURE)) inalenga kuchangia juhudi za kuleta muunganiko wa nishati jadidifu katika mnyororo wa thamani wa kilimo.
- Ubunifu wa mifumo ya umwagiliaji kwa kutumia nishatijua ni kichocheo muhimu cha kutengeneza ajira katika bara la Afrika lakini mitaji ambayo ingewawezesha wakulima wadogo kupata na kutumia nishati hii bado ni ghali sana.
KIREHE, Rwanda – Kwa miaka mingi Victor Ndwaniye, mkulima mdogo kutoka kijiji cha Nasho kilichopo kandokando ya ziwa katika wilaya ya Kirehe mashariki mwa Rwanda, alikuwa akimwagilia shamba lake lenye aina mbalimbali za mboga kwa kutumia ndoo.
Hata hivyo, kuanzia mwaka 2020, Ndwaniye ambaye ni baba wa watoto sita, amekuwa akitumia njia ya kisasa ya umwagiliaji akitumia mfumo wa umeme jua. “Umwagiliaji wa kutumia ndoo haukuwa na tija. Haukukidhi mahitaji ya wakulima wengi wadogo na ulitoa mazao hafifu,” alieleza Ndwaniye wakati wa mahojiano na Mongabay.
Kwa sasa hali ya wakulima nchini Rwanda imebadilika baada ya kuanza kilimo cha umwagiliaji kinachotumia nishati jadidifu ya umemejua. Teknolojia hii mpya inatumika katika hatua mbalimbali katika mnyororo wa thamani katika kilimo na ni mkombozi wa wakulima wadogo. Maafisa wa kilimo sasa wameweka lengo la kuongeza ukubwa wa mashamba yanayotumia kilimo cha umwagiliaji kupitia umemejua kutoka hekta 646 (ekari 1,600) za sasa hadi kufikia hekta 1,146 (eka 2,830) ifikapo 2029.
Nchi nyingine kama Bangladesh na India nazo zimepiga hatua kubwa katika kilimo cha umwagiliaji kinachotumia umemejua na zina malengo ya kuongeza ukubwa wa mashamba yanayotumia teknolojia hii ya umwagiliaji.
Katika hatua za mwanzo, wakulima wanatakiwa kulipa gharama za utunzaji wa mifumo na miundombinu ya umwagiliaji. Katika hatua hii pia serikali na wadau wengine hutoa msaada wa fedha kuwawezesha wakulima kugharamia teknolojia hii ingawa bado gharama inaonekana kubwa kwa wakulima.
Kulingana na Bodi ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo ya Rwanda (Rwanda Agriculture and Animal Resources Development Board), mpango huu unalenga kuwajenga wakulima wadogo kuhimili majanga yanayohusishwa na mabadiliko ya tabianchi na kuchochea kilimo endelevu ili kuongeza uzalishaji.
Matumizi ya teknolojia hii ya umwagiliaji yanatazamia kupunguza uzalishaji wa gesijoto unaotokana na matumizi ya pampu zinazotumia mafuta ya dizeli, hasa vijijini ambako umeme wa gridi ni adimu. Matumizi ya teknolojia ya umemejua hayahitaji matumizi ya mafuta wakati wote, jambo ambalo linapunguza gharama za uendeshaji.

Kihere ni wilaya ambayo mara nyingi imekuwa ikikabiliwa na ukame na hivyo kuwafanya wakazi wa vijiji vingi kutegemea kuchota maji kwa ajili ya umwagiliaji kutoka katika maziwa yaliyo karibu na mashamba yao.
Msimu wa kiangazi ambao huanza mwezi Juni na kumalizika Septemba, Ndwaniye alikuwa akimwagilia shamba lake angalau mara mbili kwa siku. Alitumia muda mwingi kuchota maji na hivyo kuwa na muda mchache wa kuhudumia mazao yaliyomo shambani.
Tekolojia hii mpya ambayo inatumia mwanga wa jua kuendesha pampu ya kuvuta maji, kiasi kinachotakiwa hata kama maji yatakuwa machache huko ziwani au kwenye chanzo chochote.
Sasa technolojia hii inampa fursa Ndwaniye kutumia nishati safi na kwa jinsi hali ilivyo, idadi ya wakulima wanaotumia umemejua kwa ajili ya umwagiliaji inaongezeka nchini Rwanda.
Taarifa zilizotolewa hivi karibuni na Bodi ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo ya Rwanda zinaonyesha kuwa jumla ya vyama vya ushirika vya wakulima 299 na wakulima binafsi 1,136 wanaoendesha skimu ndogo za umwagiliaji, wameanza kutumia mifumo mikubwa ya umwagiliaji ili kukabiliana na uhaba wa maji.
Bodi pia imeandaa takwimu zinazoonyesha kuwa vyama vya ushirika vya kilimo 87 vilivyopo mashariki ya Rwanda hasa kutoka sehemu zenye ukame wa mara kwa mara, vinatumia umemejua kwa ajili ya umwagiliaji kuongeza uzalishaji kwani vinatumia maji kulingana na mahitaji na hivyo kuhifadhi maji.
Katika uchunguzi wa hivi karibuni uliolenga nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara, watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Uingereza cha Sheffield wameonyesha kuwa umwagiliaji kwa kutumia umemejua unaleta mabadiliko ya kilimo katika bara la Afrika.

“Ongezeko kubwa la watu na kukosekana kwa uhakika wa chakula linachochea pia kukua kwa kilimo cha umwagiliaji ambacho kinazingatia hifadhi ya mazingira,” alisema Saeed Mohammed Wazed, kiongozi mwandamizi wa utafiti huo.
Ili kufanikisha utafiti huo, timu ya watafiti iliangalia jinsi ambavyo nchi mbalimbali chini ya jangwa la Sahara zinavyotumia nishati jadidifu ili kuachana na matumizi ya pampu ambazo zinatumia mafuta katika kilimo cha umwagiliaji.
Baada ya majaribio kadhaa, Wazed na wenzake waligundua kuwa njia bora ya kutumia umemejua kwa ajili ya umwagiliaji ni kuelewa mahitaji ya maji ya mimea mbalimbali ya mazao na kufanya tafiti za kina katika eneo mimea ilipo ili kujiridhisha na utendaji wa miundo na mifumo mbalimbal ya umwagiliaji.
“Teknolojia hii sasa imekuwa chaguo la kawaida la usambazaji maji katika maeneo ambayo hayako kwenye gridi ya taifa ya umeme nchini Rwanda,” anaeleza Jerome Hitayezu, Mkuu wa Kitengo cha Umwagiliaji cha Bodi.
Wakulima kama Ndwaniye wanasema wanashuhudia ongezeko kubwa la mazao ya shambani, na wanakiri kuwa kutumia umemejua kwa ajili ya umwagiliaji kumebadilisha kilimo.
“Kabla sijaanza kutumia umemejua kwa ajili ya umwagiliaji niliweza kuvuna tani moja tu ya aina mbalimbali za mboga kutoka kwenye hekta moja. Lakini baada ya kutumia umemejua kwa misimu miwili, niliweza kuvuna tani tatu za karoti na kabichi, mara tatu zaidi ya kiasi nilichokuwa navuna hapo awali,” alieleza.
Benki ya Dunia inakadiria kuwa kati ya hekta milioni 183 (eka milioni 452) zinazolimwa katika nchi zilizoko kusini mwa Jangwa la Sahara, asilimia 95 hutegemea mvua na pungufu ya asilimia tano hutumia njia nyingine za kupata maji, “kiasi cha chini kabisa cha kilimo cha umwagiliaji katika eneo lolote duniani.” Hii ina maana kuwa kwa kiasi kikubwa wakulima hutegemea mvua au kutumia pampu za kusukuma maji zinazotumia mafuta, kwa wale wachache wanaoweza kumudu gharama.

Lengo ni kuongeza upatikanaji nishati na kuongeza tija
Taasisi ya Rasilimali ya Dunia (The World Resources Institute (WRI) inaeleza kuwa mojawapo ya mikakati ya kupambana na changamoto ya upatikanaji wa nishati katika nchi zilizopo kusini mwa Jangwa la Sahara ambako watu wengi hawana umeme, ni kubaini fursa za kutumia nishati jadidifu katika uzalishaji na kilimo cha wakulima wadogo.
WRI Africa inasaidia juhudi za kukuza matumizi ya nishati jadidifu katika mnyororo wa thamani wa kilimo katika nchi mbalimbali za Afrika, ikiwemo Rwanda, kufanya kazi na wakulima wadogo, serikali za mikoa, taasisi za kifedha na wazalishaji wajasiriamali wadogo ili kuongeza matumizi endelevu ya nishati jadidifu.
Kulingana na Shirika la Kimataifa la Nishati (International Energy Agency (IEA), watu milioni 600 katika Bara la Afrika hawajafikiwa na nishati ya umeme, jambo ambalo linafifisha maendeleo ya kilimo. Wakati ambapo kilimo kinatoa ajira kwa asilimia 60 ya nguvukazi ya Afrika, wataalamu wanasisitiza umuhimu wa kupanua wigo wa kufikiwa na nishati kama nyezo ya kuongeza tija na uhakika wa chakula.
Benson Ireri, mtaalamu kutoka WRI inayosimamia masuala ya nishati kwa upande wa Afrika, alieleza kuwa ukiacha kilimo cha umwagiliaji ambapo ndipo miradi mingi ya nishati inatekelezwa, nishati jadidifu inahitajika katika kila hatua ya mnyororo wa thamani wa kilimo. Hatua hizi ni pamoja na kupooza na kugandisha, kuongeza thamani, kuhifadhi na kusafirisha mazao kutoka shambani mpaka kwenye masoko na kuweka viwango vya ubora.
“Kutumia nishati jadidifu kama umwagiliaji wa kutumia umemejua kunapunguza gharama za uzalishaji na gharama za mategenezo ya mashine za kusukuma maji zinazotumia mafuta. Matumizi ya nishati jadidifu huongeza kipato cha wakulima wadogo,” alieleza Ireri.
Kwa sasa WRI inahamasisha matumizi ya nishati jadidifu katika uzalishaji kupitia mradi unaoitwa PURE. Matumizi haya yanawawezesha wakulima na wafanya biashara ya kilimo kuongeza tija, kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno na kujiongezea kipato. Taasisi hiyo pia inashirikiana na wadau wa maendeleo katika nchi za Afrika Mashariki na Kati, taasissi za fedha na wazalishaji mbalimbali ili kukuza matumizi ya nishati jadidifu.
Matokeo ya utafiti yaliyochapishwa mwaka 2023 na Taasisi ya Kimataifa ya Uchambuzi (The International Institute of Analysis) yanaonyesha kuwa mifumo ya umwagiliaji katika maeneo mbalimbali inayotumia umemejua imeleta mabadiliko katika nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara kwani vyanzo vya nishati jadidifu ni vingi na havijatumika ipasavyo.

Kuondoa kabisa matumizi ya pampu ghali za maji zinazotumia mafuta?
Ireri ana matarajio makubwa kuhusu matumizi ya nishati jadidifu katika kilimo. Anaona kuwa matumizi hayo siyo tu yataondoa pampu za maji zinazotumia mafuta ambazo humuingizia mkulima mdogo gharama kubwa lakini pia kutachochea mahitaji, hasa katika jamii za vijijini. Hatua hii inaweza kutatua changamoto ya upatikanaji wa nishati yenye gharama nafuu ambayo itawafikia wakazi wa vijijini.
Nchini Rwanda, kilimo ndiyo mzalishaji mkubwa wa gesijoto ambapo huchangia asilimia 70 ya gesijoto yote inayozalishwa nchini, kulingana na ripoti ya 2019 ya Mamlaka ya Mazingira ya Rwanda (The Rwanda Environmental Management Authority (REMA).
“Wakulima watumie nishati jadidifu kama njia ya kufikia kilimo endelevu kinachopunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kinachokuza uchumu,” anasema Ireri.
Mapitio yaliyofanywa na Wakala wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu (The International Renewable Energy Agency) na Shirika la Kazi la Umoja wa Mataifa yanaonyesha kuwa teknolojia za nishati ambazo hazikuunganishwa na gridi za taifa zinazalisha fursa kwa jamii katika nyanja mbalimbali zikiwemo za ufundi, huduma kwa jamii na ushirikiano wa jamii katika nchi zilizopo kusini mwa Jangwa la Sahara.
“Matumizi ya nishati jadidifu katika kilimo katika taifa na kanda yatasaidia pia kupnguza gesijoto,” alieleza Ireri.
Pale Kirehe, wakulima wadogo kama Ndwaniye wanaeleza kuwa matumizi ya umemejua kwaajili ya umwagiliaji yamewawezesha kulima mazao mengi ya aina mbailmbali kwa mwaka mzima.
“Matumizi ya umemejua kwa umwagiliaji yameondoa utegemezi wa mvua ambayo kwa sasa msimu wake haueleweki,” alieleza.
Picha yay bango: Matumizi ya nishati jadidifu kama umemejua kwa ajili ya umwagiliaji na hatua nyingine katika mnyororo wa thamani ya kilimo yanaweza kupunguza gharama za uzalishaji kwa kuepuka gharama za matengenezo ya pampu zinazotumia mafuta. Mkulima kutoka Kihere, Mashariki mwa Rwanda, atumia umemejua kwaajili ya umwagiliaji. Picha na Aimable Twahirwa wa Mongabay.
Nukuu:
Mohammed Wazed, S., Hughes, B. R., O’Connor, D., & Kaiser Calautit, J. (2018). A review of sustainable solar irrigation systems for sub-Saharan Africa. Renewable and Sustainable Energy Reviews, 81, 1206-1225. doi:10.1016/j.rser.2017.08.039
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kingereza mnamo tarehe 31/03/2025.