- Serikali ya Tanzania ilianzisha maeneo matano ya hifadhi za baharini, au kwa Kiingereza Marine Protected Areas (MPAs), katika miaka ya 1990 ili kulinda idadi ya samaki iliyokuwa ikipungua.
- Kwa kipindi cha karibu miaka 20, vijiji vilivyo karibu na maeneo haya ya hifadhi vilitegemea kidogo uvuvi na kilimo, na viliona hali yao ya maishaikistawi kwa kasi zaidi kuliko jamii zilizoko mbali, utafiti mpya unaonyesha.
- Watafiti hawakupata ushahidi unaoonyesha kama MPAs ziliathiri mafanikio ya uvuvi katika makazi ya karibu.
- Waliweka dhana kwamba MPAs zilikuza uchumi wa maeneo ya karibu kwa kuvutia watalii.
Maeneo ya hifadhi ya baharini nchini Tanzania yameboresha viwango vya maisha katika jamii za karibu kwa kipindi cha karibu miaka 20, kwa mujibu wa utafiti wa hivi karibuni uliochapishwa katika jarida la kisayansi la kimataifa linalojulikana kama Conservation Letters.
Karibu na maeneo haya ya hifadhi (MPAs), hali ya maisha iliimarika na kulikuwa na mabadiliko kutoka kwenye kazi za kilimo, alisema Julia Girard, mwanafunzi wa shahada ya uzamifu (Ph.D.) katika uchumi wa mazingira katika Chuo Kikuu cha Montpellier, Ufaransa, ambaye pia ni mmoja wa waandishi wa utafiti huo.
Namna maeneo haya ya hifadhi ya baharini yanavyoathiri uhifadhi na maendeleo ya jamii ni suala muhimu kwa Tanzania, ambako asilimia 20 ya watu hutegemea sana uvuvi kwa chakula na kipato.
Tanzania ilianzisha maeneo matano ya hifadhi ya baharini yenye matumizi mchanganyiko katika miaka ya 1990, ambayo huruhusu uvuvi kwa kufuata kanuni maalum zilizowekwa ili kuwa na uvuvi endelevu.
Wanasayansi wametambua kuwa MPAs zinazoruhusu uvuvi uliodhibitiwa ni nyenzo muhimu kusaidia Tanzania na mataifa mengine kulinda asilimia 30 ya bahari zao ifikapo mwaka 2030 bila kuwanyima wavuvi fursa ya kuendelea kujipatia riziki.
Ili kuona athari za MPAs kwenye maendeleo ya ndani, timu ya watafiti ilihoji kaya 840 katika vijiji 24 mwaka 2021, wakiuliza maswali kuhusu ajira, historia ya uvuvi, kiwango cha maisha, na mitazamo kuhusu hifadhi hizo za baharini. Kisha walilinganisha takwimu hizo na matokeo ya utafiti unaoshabihiana na ule uliofanywa mwaka 2003. Huu ni miongoni mwa tafiti chache zinazobainisha athari za muda mrefu za MPAs zenye matumizi mchanganyiko kwenye maendeleo ya jamii.
Vijiji vyote vilivyohusishwa katika utafiti vilionyesha kuboreshwa kwa hali ya maisha kati ya mwaka 2003 na 2021, kwa kuzingatia vigezo 18, ikiwemo umiliki wa nyumba, usalama wa chakula, na upatikanaji wa jokofu. Lakini wakazi wa vijiji vilivyo ndani ya kilomita 5 kutoka eneo la hifadhi vilionyesha ongezeko kubwa zaidi la hali ya maisha ikilinganishwa na vile vilivyoko zaidi ya kilomita 10 kutoka kwenye hifadhi, kwa mujibu wa vipimo vya viwango vya maisha vilivyotumiwa na watafiti.

Matokeo ya utafiti huu yanaonyesha mabadiliko ukilinganisha na ule wa mwaka 2003, ambao haukupata tofauti kubwa katika viwango vya maisha kati ya jamii zilizo karibu au mbali na maeneo ya hifadhi ya baharini (MPAs). Wakati wa utafiti huo wa awali, MPAs zilikuwa zimedumu kwa muda wa kati ya miaka mitatu hadi minane tu.
Watafiti hawakuweza kuhusisha moja kwa moja uboreshaji mkubwa wa hali ya maisha na fursa bora za uvuvi zilizotokana na ulinzi wa maeneo hayo. Badala yake, ongezeko la ajira nje ya uvuvi na kilimo lilikwenda sambamba na kuboreshwa kwa hali ya maisha ya watu.
Matokeo haya yanatofautiana na tathmini ya hifadhi za baharini huko Amerika ya Kati, ambako MPAs za eneo hilo zilibainika kunufaisha watu zaidi kwa kuhifadhi au kuongeza idadi ya samaki.
Aidha utafiti ulionyesha kuwa ongezeko la viwango vya maisha lilitokana na ukuaji wa sekta nyingine nje ya uvuvi na kilimo, ambao ulitokea tu katika jamii zilizo karibu na MPAs. Watafiti walihisi kuwa mwenendo huu unasukumwa na utalii. Wageni huogelea na kuzamia kwenye miamba ya matumbawe, kisha hununua bidhaa za kienyeji kama sabuni za mwani, alisema Narriman Jiddawi, mtaalamu wa biolojia ya baharini na mwandishi mwenza wa utafiti kutoka shirika la Zanzi Marine and Coastal Solutions huko Zanzibar, Tanzania.
Athari za utalii zinaonekana wazi hasa kwenye ukanda wa mashariki wa kisiwa cha Unguja, kisiwa kikubwa zaidi katika funguvisiwa la Zanzibar lililopo nje ya pwani ya Tanzania. Kila mwaka, mamia ya maelfu ya watu hufika kufurahia fukwe zake zenye mchanga mweupe na bahari yenye rangi ya bluu ya samawati.
Ongezeko la wageni lilibadilisha soko la ajira visiwani humo katika kipindi cha utafiti, na viwango vya maisha viliongezeka kwa kasi zaidi katika vijiji vilivyokuwa vinategemea utalii.
“Kwa kutumia takwimu tulizonazo, hatuwezi kuthibitisha kwamba mabadiliko tunayoyaona yamesababishwa moja kwa moja na utalii,” alisema Girard. “Lakini hiyo ni mojawapo ya uwezekano.”
Watafiti pia hawakuwa na takwimu za kutosha kutathmini athari za kiikolojia za wimbi la watalii, lakini Jiddawi alieleza kuwa makundi makubwa ya wazamiaji huenda yanaharibu miamba ya matumbawe.
Licha ya athari za utalii, sekta ya uvuvi nchini nayo inakabiliwa na kupungua kwa samaki kiasi cha kutia wasiwasi.
Watu kutoka vijiji 24 vilivyohusishwa katika utafiti waliripoti kuwa walikuwa wanapata samaki wachache kwa siku mwaka 2021 ikilinganishwa na mwaka 2003. Utafiti uligundua kuwa vijiji vilivyo karibu na MPAs vilishuhudia kupungua huko huko kwa idadi ya samaki waliovuliwa kila siku kama ilivyokuwa kwa wale wanaoishi mbali zaidi. Wakazi wengi walisema MPAs hazikuwa na athari yoyote kwenye idadi ya samaki waliokuwa wakivuliwa.
Utafiti wa kina wa maeneo ya hifadhi ya baharini yenye matumizi mchanganyiko nchini Tanzania unaonyesha kuwa athari zake kwa idadi ya samaki hutofautiana. Katika hali nyingi, watafiti hawapimi moja kwa moja idadi ya samaki bali huangalia kiwango cha samaki kinachovuliwa na wavuvi.
Utafiti mmoja uligundua kuwa wavuvi waliokuwa ndani ya Hifadhi ya Baharini ya Mnazi Bay walivua samaki mara nne zaidi mwaka 2010 ikilinganishwa na mwaka 2006.

Utafiti mwingine ulipima samaki waliovuliwa na kuletwa pwani kati ya Oktoba 2019 hadi Machi 2020. Matokeo yalionyesha kuwa boti zilizo ndani ya hifadhi mbili za baharini nchini Tanzania zilileta samaki wachache ikilinganishwa na zile za maeneo yasiyolindwa, lakini samaki waliotoka kwenye hifadhi walikuwa wakubwa zaidi kwa wastani. Waandishi wa utafiti huo walieleza kuwa kanuni za hifadhi za baharini zilipunguza idadi ya samaki waliovuliwa na kusaidia samaki wachanga zaidi kukua.
Hata hivyo, sheria za MPAs zinazodhibiti uvuvi huenda hazitoshi kupunguza shinikizo kubwa linalokabili mifumo ya ikolojia ya baharini.
Kati ya mwaka 2000 na 2020, idadi ya watu iliongezeka mara mbili, kadhalika na mabadiliko ya tabianchi, alisema David Obura, mwanasayansi wa miamba ya matumbawe na mwanzilishi wa CORDIOEA, shirika lisilo la kiserikali la uhifadhi wa bahari nchini Kenya. “Kwa hiyo, shinikizo linalosababisha kupungua kwa idadi ya samaki hivi karibuni linaendelea kuongezeka.”
Utafiti huu wa hivi karibuni unaonyesha kuwa hatua moja ya uhifadhi inaweza kusababisha athari mbalimbali katika maeneo tofauti, alisema Obura, ambaye hakuhusika moja kwa moja na utafiti huo.
“Kuanzisha maeneo ya hifadhi hakujaboresha uzalishaji wa samaki moja kwa moja,” alisema, “lakini kumesaidia kupanua vyanzo vya kipato.”
Picha ya bango: Wavuvi wakiwa baharini karibu na Dar es Salaam, Tanzania. Picha na UN Photo/Milton Grant via Flickr (CC BY-NC-ND 2.0).
Nukuu:
Desbureaux, S., Girard, J., Dalongeville, A., Devillers, R., Mouillot, D., Jiddawi, N., … Leblois, A. (2024). The long-term impacts of Marine Protected Areas on fish catch and socioeconomic development in Tanzania. Conservation Letters, 17(6), e13048. doi:10.1111/conl.13048
Gill, D. A., Lester, S. E., Free, C. M., Pfaff, A., Iversen, E., Reich, B. J., … Warmuth, L. M. (2024). A diverse portfolio of marine protected areas can better advance global conservation and equity. Proceedings of the National Academy of Sciences, 121(10). doi:10.1073/pnas.2313205121
Machumu, M. E., & Yakupitiyage, A. (2013). Effectiveness of marine protected areas in managing the drivers of ecosystem change: A case of Mnazi Bay Marine Park, Tanzania. Ambio, 42(3), 369-380. doi:10.1007/s13280-012-0352-8
Nowakowski, A. J., Canty, S. W., Bennett, N. J., Cox, C. E., Valdivia, A., Deichmann, J. L., … McField, M. (2023). Co-benefits of marine protected areas for nature and people. Nature Sustainability, 6(10), 1210-1218. doi:10.1038/s41893-023-01150-4
Salema, F. G., Mbije, N. E., Mwakalapa, E. B., & Rija, A. A. (2022). Patterns of fish community structure in protected and non-protected marine areas of mainland Tanzania. Western Indian Ocean Journal of Marine Science, 21(1), 91-101. doi:10.4314/wiojms.v21i1.7
Tobey, J., & Torell, E. (2006). Coastal poverty and MPA management in Mainland Tanzania and Zanzibar. Ocean & Coastal Management, 49(11), 834-854. doi:10.1016/j.ocecoaman.2006.08.002
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 24/03/2025