- “Searching for Amani” ni filamu ya makala kuhusu vijana wawili wa Kenya waliounganishwa na kuwa marafikikupitia tukio la mauaji.
- Simon Ali, ambaye baba yake — aliyekuwa akiwaongoza watalii katika Kaunti ya Laikipia, Kenya ya Kati — aliuawa kwa kupigwa risasi mwaka 2019 akiwaongoza wataliikwenye eneo la pori.
- Katika filamu hiyo, mtayarishaji Peter Goetz anamkabidhi Ali kamera huku akitafuta taarifa kuhusu mauaji ya baba yake,huku akihuzunika na kupitia changamoto za ujana ili apate suluhu kwa ajili yake na familia yake.
- Filamu hii ilionyeshwa katika Tamasha la Filamu za Mazingira la DC 2025, ambapo Mongabay ni mshirika wa vyombo vya habari.
Ni hadithi ya kusisimua kuhusu vijana wawili wa Kenya ambao urafiki wao unatokana na tukio la mauaji. Filamu hii ya makala, “Searching for Amani”, inaweka wazi mvutano mgumu iliyo kati ya wanahifadhi, wakulima wa mazao na wafugaji nchini Kenya, huku kipindi kirefu cha ukame kikisababisha migogoro juu ya rasilimali zinazozidi kupungua.
“Wakati kuna amani, huwa watu hawauawi,” anasema Simon Ali, mwenye umri wa miaka 18, ambaye baba yake, aliyekuwa mwongoza watalii, aliuwawa kazini kwenye hifadhi ya wanyamapori miaka mitano iliyopita. “Kama mmoja wa wahanga wa migogoro, ninajua umuhimu wa amani.”
Sauti ya Ali inafichua taswira ya muda ambao umepita tangu alipopata habari kwamba baba yake alipigwa risasi akiwaongoza watalii katika eneo la pori la Kaunti ya Laikipia, Kenya ya Kati.

Miaka mitano baadaye, Ali amepitia majonzi kwenye ujana wake, huku akifanya kazi kwenye mradi wa filamu uliotayarishwa na Backroads Pictures na Nicole Gormley Films, ambamo amekuwa akitafuta majibu kuhusu jinsi, na sababu ya baba yake kuuawa, pamoja muuaji. Wakati huo huo, usuli wa simulizi hili ni ukame sugu, ambao umetajwa kama mbaya zaidi kuwahi kuikumba eneo hilo katika kipindi cha miaka 40.
Ali anapojitokeza mbele ya kamera katika filamu ya “Searching for Amani”, anashika kamera yake na kuchukua jukumu la mwandishi chipukizi wa uchunguzi. Akiwa chini ya ulezi wa kikosi cha filamu, anafunzwa mbinu za uandishi wa habari, zinazomwezesha kuwa na ukakamavu anapowahoji watu wengi waliokuwa na taarifa kuhusu mauaji ya baba yake, Stephen Ali, na hatimaye kupata utulivu kiasi kwa ajili yake na familia yake.
Kenya imeshuhudia migogoro kati ya wanaoshikilia ardhi ya hifadhi yenye uzio, wakulima wa mazao, na jamii za wafugaji ambazo kihistoria zilitembeza mifugo yao kwa uhuru zaidi kuliko walio nao sasa. Ukame unaposababisha upungufu wa maji na malisho, migongano kati na ndani ya jamii huwa hatari zaidi.
Hiki ndicho kilikuwa chanzo cha kifo cha baba yake Ali.
Hata hivyo, urafiki wake na Haron Lenges ndio kiini cha nguvu ya filamu hii.


Familia ya Ali inatoka katika jamii inayotegemea kilimo cha mazao, ilhali ile ya rafiki yake wa karibu, Lenges, ni ya ufugaji. Filamu inavyoendelea, watazamaji wanaalikwa kuketi mezani na kushuhudia mazungumzo ya karibu kati ya vijana hawa wawili, jambo linalomwezesha mtazamaji kutambua tamaduni pana na za muda mrefu wanazoziwakilisha.
“Tulitaka kusimulia hadithi za kukua utu uzima katika jamii mbalimbali za mstari wa mbele duniani,” anasema mtayarishaji na mwandishi mwenza Peter Goetz wa Backroads Pictures. Wazo lao kuu lilikuwa la kuwapata vijana katika maeneo mbalimbali kama Afrika, Aktiki na Pasifiki, ambao hadithi zao zinaonyesha hali ya kuishi na athari mbaya ya mabadiliko ya tabianchi. Azma ilikuwa kuwapa kila mmoja kamera na kuwafanya wasimulizi.
Goetz alipokutana na Ali, hakuwa tu mtu mwenye simulizi binafsi lililo mfano wa wengine wengi ambao maisha yao yamevurugwa na migogoro inayoendeshwa na hali ya hewa nchini Kenya; lakini pia alimkuta akitazamia kuwa mwandishi chipukizi wa uchunguzi. Ilikuwa rahisi kumpa Ali kamera na kumruhusu kuwa msimulizi.
Debra Aroko, ambaye ni mwanamkasi wa filamu jijini Nairobi, alitoka kwenye mradi huu akiwa na hisia upya za matumaini baada ya kufanya kazi na Ali na Lenges, ambao ujana na nishati yao huleta shauku isiyokoseka katika filamu na kwa watazamaji.
“Ilikuwa muhimu kwa filamu hii kuonyeshwa barani,” anasema. “Natumai watoto wengine kutoka barani watautazama, na kuhisi kwamba wanawakilishwa, kando na kuwa na udhibiti katika hadithi za maisha yao, na jinsi ulimwengu unavyoiona, ambayo mara nyingi nahisi hao hunyimwa.”
Aroko anasema kwamba kila Ali anapohudhuria maonyesho ya filamu hii kwa watazamaji vijana wa nchi zilizo Magharibi mwa dunia, ni wazi jinsi wanavyojihusisha naye, na kumthamini kwa kushikilia dhamira yake ya kuvuta watu ili wamsaidie katika uchunguzi. “Kama hivi ndivyo filamu hii inawaathiri watazamaji wa Magharibi, itakuwaje itakaporejeshwa nchini Kenya na Afrika Mashariki?”

Yasiyojitokeleza wazi katika takwimu zinazoonyesha ukubwa na mwendo wa athari kubwa za mabadiliko ya tabianchi barani Afrika ni maisha ya watu binafsi na jinsi yanaathiriwa na ukame, njaa, joto kali, kuenea kwa jangwa, na migogoro kati ya jamii wenye tamaduni tofauti za kilimo nchini Kenya. Mwandishi wa mfululizo wa maneno ya filamu, Aroko, anatumia mbinu ya kuwaacha utu wa Ali na Lenges kuwakilisha pia ule wa jamii zao.
“Kwa kila tendo au kutochukua hatua (katika filamu) kuna binadamu halisi anayeathirika,” anasema Aroko. “Ni kielelezo kidogo cha tatizo kubwa: familia ambayo maisha yake yalichanwa na kitu ambacho huenda kingezuilika kama tungechukua hatua kupunguza tatizo hili.”
Kiini cha simulizi hili ni ukumbusho kwamba kila mtu anapaswa kuwa na ubora wa maisha, popote anapotoka.
Wakati walipokuwa wakitengeneza filamu, Goetz na timu walishuhudia Ali akikua na familia yake ikiendelea kuomboleza kumpoteza mzazi na mume. “Motisha yangu, siku baada ya siku, ilikuwa kuwapa familia hii moja jukwaa na sauti,” anasema Goetz.
Na ingawa baadhi ya timu ya utayarishaji wa filamu wanahisi tumaini baada ya mradi, Ali anasema alipata namna fulani ya amani kupitia umakinifu wa mchakato wa uchunguzi na majibu uliyoibua.
“Searching for Amani” iliweza kuingiza angalau hadithi moja ya Kiafrika kwenye jukwaa la kimataifa ambako mara nyingi simulizi kutoka Kaskazini ya Dunia ndizo hutawala. Simulizi hilo lina ujumbe kuhusu watu na taasisi ngapi zilizoshindwa kuihudumia familia ya Ali baada ya mauaji ya mpendwa wao. Si tu kwamba mfumo wa haki haukuchunguza kwa kina tukio hilo — dhana ni kwamba wafugaji wenye silaha ndio waliompiga risasi, lakini hakuna mtu aliyekamatwa — bali pia watu wenye ushawishi karibu na mahali pa kazi pa Stephen Ali walikuwa na taarifa kuhusu mauaji, lakini hawakuchukua hatua kuwajulisha waliojeruhiwa zaidi, ambao ni familia ya Ali.
Aroko anasema: “Hakuna mtoto wa miaka 13 anayepaswa kuwa katika hali ya kutafuta majibu ya aina hii.”

Kupitia filamu, Ali na Lenges wanapitia hatua za ukuaji kadri simulizi linavyopevuka katika miaka mitano ya utayarishaji wake. Leo, Ali yuko ukingoni mwa utu uzima — atatimiza miaka 19 mwezi Septemba — na yuko kwenye hatua za mwisho za mwaka wake wa mwisho wa shule ya upili. Anasema anatumaini kuchukua tena kijiti cha uandishi wa habari pindi tu atakapokamilisha masomo ya sekondari.
Tangu alipoanza kushirikiana na Goetz, mazingira ya mgogoro katika Kaunti ya Laikipia yamezidi kuzorota. Watu bado wanahangaika na njaa, asema Ali, akitoa taarifa ya hali ilivyo Laikipia. Tishio la migogoro bado lipo.
Ali naye amekua katika kipindi cha miaka mitano iliyopita. Anapojitayarisha kwa mitihani ya mwisho wa sekondari mnamo mwezi Novemba, bado anatamani kuwa mwandishi wa habari. “Ninaamini uandishi unaweza kuwafanya watu wabadili mtazamo,” anasema. “Naweza kuleta mabadiliko. Kwangu, hiyo ni hadithi nzuri.”
Picha ya bango: Vijana wawili wa Kenya, Haron Lenges na Simon Ali, waliounganishwa na kuwa marafiki kupitia tukio la mauaji.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kingereza mnamo tarehe 14/03/2025.