- Barani Afrika,kuna karibu maeneo 9,000 yaliyohifadhiwa yenye ukubwa wa kilomita za mraba milioni 4.37 (maili za mraba milioni 1.69).
- Maeneo hayani kitovu cha uundaji wa sera za uhifadhi wa nchi za Kiafrika zinazotarajia kulinda asili na wanyamapori walio hatarini.
- Chini ya lengo la Umoja wa Mataifa la Mifumo ya Bioanui “30×30”, kiwango cha ardhi iliyohifadhiwa barani Afrika kinatarajia kuongezeka kwa kiasi kikubwa.
- Kama sehemu ya mfululizo wa ripoti kuhusu lengo hili, Mongabay ilitembelea maeneo yaliyohifadhiwa nchini Uganda, Rwanda na Kenya.
Hii ni makala ya kwanza katika mfululizo wa habari za Mongabay kuhusu ‘Maeneo Yaliyolindwa Afrika Mashariki’. Soma sehemu ya pili na ya nne.
Mnamo Juni 13, 1959, mwindaji wa kabila la Waata, Galogalo Kafonde, alijisalimisha kwa kikosi cha kikoloni cha “Field Force” cha Kenya, kitengo cha kwanza barani Afrika cha kupambana na ujangili. Kwa karne nyingi, watu kutoka kabila la Waata walikuwa wakiwinda tembo. Kumuua tembo mmoja ilikuwa ni ibada ya jandoni. Tofauti na majirani zao waliofuga ng’ombe, jamii ya Waata waliishi kwa kula nyama ya ng’ombe na kuvaa ngozi za tembo. Pembe za ndovu hazikuwa na manufaa kwao, lakini waliziuza kupitia ubadilishanaji wa bidhaa nyingine na wafanyabiashara wa Kiarabu huko Mombasa.
Biashara ya pembe za ndovu ilipozidi kushamiri katika karne ya 17, ikichochewa na ukuaji wa soko la watumiaji wa Ulaya, sifa ya Waata iliimarika. Walikuwa miongoni mwa wafuatiliaji bora wa tembo ukanda wa Afrika Mashariki, wanaojulikana kama “watu wa upinde mrefu” kwa ustadi wao wa kutumia mishale yenye sumu.
Lakini wawindaji wa Ulaya walikuja kuwaona jamii za Waata na jamii nyingine asilia kama ushindani. Mnamo mwaka 1897, Uingereza ilipoweka malengo yake kwa koloni la kudumu la Kenya, ilipiga marufuku uwindaji “wa asili” ambao haujaidhinishwa. Kwa saini moja tu ya kalamu, kiini cha maisha ya Waata kiligeuka kuwa haramu.

Mnamo mwaka 1948, Waingereza waliunda Mbuga ya Taifa ya Tsavo, mojawapo ya mbuga za kwanza nchini Kenya. Lakini upande wake wa mashariki ulikuwa uwanja wa uwindaji wa Waata. Richard Sheldrick, mmoja wa watu mashuhuri zaidi kwenye uhifadhi katika karne ya 20, alipewa jukumu la kumwondoa Kafonde, mwindaji maarufu wa Waata, ambaye alikuwa mlengwa wake mkubwa.
Katika historia ya biashara ya pembe za ndovu, mwandishi Keith Somerville anasimulia kauli ya Kafonde alipokamatwa.
“Tembo wameisha,” alisema. “Matajiri wanaotaka zaidi na zaidi wanawajibika. Kama wewe, ninaogopa kuangamia kwa tembo, kwa sababu ndio msingi wa utamaduni wetu na maisha yetu ya kila siku.”
Kukamatwa kwa Kafonde ilikuwa ni hitimisho la kampeni ya miaka mingi ya kikosi cha Field Force, ambacho kilianzisha mbinu kali ambazo bado zinafafanua operesheni za kupambana na ujangili hadi leo. Tsavo, ambayo sasa imegawanywa katika sehemu za mashariki na magharibi, ilikuwa moja ya idadi kubwa ya maeneo yaliyohifadhiwa na kuanzishwa katika miongo ya mwisho ya utawala wa kikoloni. Kwa upande wa kusini, Mbuga ya Taifa ya Albert – ambayo baadaye ilikuja kuwa Virunga ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na mbuga za taifa za Volcano za Rwanda – iliteuliwa na Wabelgiji mnamo 1925.

Mwaka mmoja baadaye ikaja Hifadhi ya Taifa ya Kruger nchini Afrika Kusini, ambayo ilipewa jina la Rais wa zamani wa Transvaal (na mwindaji simba) Paul Kruger. Baada ya Vita vya Pili vya Dunia, wimbi la hifadhi lilifuata, zikiwemo Tsavo, Victoria Falls katika iliyokuwa, Southern Rhodesia (leo Zimbabwe), Murchison Falls nchini Uganda, na nyingi nyinginezo.
Hifadhi hizi mpya hazikuwa maeneo ya kwanza yaliyohifadhiwa katika bara la Afrika. Watawala wa Milki ya Dahomey nchini Benin walitawala misitu takatifu, ambako uwindaji ulikuwa umepigwa marufuku kama ishara ya kuheshimu roho zilizodhaniwa kuishi ndani ya misitu hiyo. Vilele vya milima ya Rwenzori nchini Uganda vilichukuliwa kama maeneo yaliyozuiwa na jamii ya Bakonzo, ambao waliamini kuwa ni makao ya miungu ya uzazi. Na kuanzia mwishoni mwa karne ya 19, hifadhi za misitu zilianzishwa na serikali za kikoloni katika Afrika Magharibi, Kati na Kusini ili kudhibiti uvunaji wa mbao.
Lakini Tsavo na hifadhi nyingine zilianzishwa kama suluhisho kwa tatizo ambalo wakoloni wenyewe walikuwa wamelitengeneza: mauaji ya halaiki ya wanyama wakubwa wa barani Afrika. Hasa tembo wake walikuwa karibu kutoweka kufikia mwanzoni mwa karne ya 20.

Awali, wafanyabiashara wa Ulaya walinunua pembe za ndovu kutoka kwa Waafrika kama Waata. Lakini kwa kutumia bunduki zao, haraka wakageuka kuwa wauaji wakubwa wa tembo ambao bara lilikuwa haliwaoni. Kati ya mwaka 1850 na 1914, wawindaji waliua takriban tembo 40,000 kwa mwaka ili kuimarisha masoko ya pembe za ndovu huko Bara la Ulaya na Amerika. Mnamo mwaka 1914, ndovu wapatao 4,000 walipigwa risasi kwa ajili ya kutengeneza mipira ya mchezo wa biliadi nchini Marekani pekee.
Wakiwa na wasiwasi wa kupungua kwa idadi ya tembo na spishi zingine kama simba, wawindaji wataalamu katika makoloni, pamoja na washirika wao waliokuwa sehemu mpya za uhifadhi katika nchi zao, walitaka baadhi ya makazi ya wanyamapori ya bara hilo kulindwa. Wakiwa wameiga mfano wa Yellowstone huko Marekani, hifadhi za taifa na maeneo mengine yaliundwa na wakati mwingine yaliruhusu uwindaji mdogo, lakini chini ya mfumo wa kuruhusu ambao kwa kawaida uliwatenga Waafrika waliokuwa wakiishi karibu au wamehamishwa ili kupisha hifadhi hizo.
Serikali za kikoloni zilipata mapato kutokana na mauzo ya pembe za ndovu na mbao, na mojawapo ya malengo ya msingi ya kulinda asili ilikuwa ni kudhibiti thamani yake ya kiuchumi, anaandika Somerville.
Lakini umiliki na ufikiaji wa thamani hiyo ulipingwa tangu mwanzo. Ukoloni barani Afrika ulionyesha uharibifu mkubwa kwa mazingira, na misitu iliyokatwa au kugeuzwa kuwa mashamba na migodi. Makundi makubwa ya tembo yaliangamizwa – kwenye miaka 200, kwa mfano, ndovu wote 25,000 ambao walikuwa wanazurura Cape Colony ya Afrika Kusini walikuwa wametoweka.

Waafrika wenyewe walipata faida chache kutokana na uharibifu huu. Na huku mamlaka za kikoloni zikiitikia kelele za kulinda kile kilichosalia, watu wengi wa jamii za kiasili walijikuta wakisukumwa kando na sheria mpya zilizowekwa kwenye ardhi waliyoishi kwa vizazi vingi.
Maisha ya jamii ya Waata hayakuwa sawa baada ya kampeni ya askari wa Field Force katika eneo ambalo leo ni Mbuga ya Taifa ya Tsavo Mashariki. Kwa kuzuiwa kuwinda, walibaki katika umaskini. Tsavo ilikumbwa na wimbi la ujangili katika miaka ya 2010, na baadhi ya jamii ya Waata walishiriki katika mauaji hayo, lakini leo, tishio kubwa kwa tembo wa mbuga hiyo si mishale yenye sumu, bali ni uzalishaji wa gesi chafu kutoka nchi tajiri.
Wawindaji wa zamani waliojulikana kama wawindaji hodari ambao waliishi katika uhusiano mzuri na mfumo wa ikolojia ya Tsavo, sasa jamii ya Waata inapambana na wawekezaji wa mashamba ya kilimo cha biashara kwenye ukingo wa mbuga hiyo na wanasema wamesahauliwa na Serikali ya Kenya.

Ili kulinda na kuhifadhi
Chanzo cha hifadhi za taifa kilikuwa cha kikoloni, lakini baada ya kupata uhuru, viongozi wapya wa Afrika walikumbatia sheria na sera za kulinda wanyamapori na mifumo ya ikolojia. Katika hotuba yake maarufu ya “Arusha Manifesto” ya mwaka 1961, Baba wa Taifa wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere, alisema: “Uhai wa wanyamapori wetu ni jambo la muhimu sana kwa sisi sote barani Afrika.”
Hata hivyo, vitisho vimebadilika tangu mwanzoni mwa karne ya 20. Barani Afrika kote, ongezeko la idadi ya watu wanaotafuta kuboresha hali yao ya maisha, pamoja na tamaa isiyoisha ya dunia kwa rasilimali za asili za bara hili na athari zinazozidi kuongezeka za mabadiliko ya tabianchi, vinaendelea kutishia misitu, savana, na maeneo oevu ya kiikolojia.
Kulingana na Ripoti ya Living Planet Report ya mwaka 2024 ya World Wide Fund for Nature (WWF), kati ya mwaka 1970 na 2020, idadi ya wanyama wenye uti wa mgongo barani Afrika ilipungua kwa asilimia 76. Sokwe wa Afrika Magharibi, ambao idadi yao tayari imepungua kwa asilimia 80 tangu mwaka 1990, wanabanwa na uchimbaji madini na maendeleo ya miundombinu. Zaidi ya nusu ya kasuku wa kijivu barani Afrika , wamepotea kufuatia ukataji miti na biashara haramu ya wanyama wa kufugwa. Takriban tembo tisa kati ya 10 wa msituni, wametoweka tangu miaka ya 1960.

Lakini kuna dalili za matumaini. Licha ya kupungua kwa jumla, idadi ya tembo katika Afrika Mashariki na Kusini imeanza kutengamaa, na katika maeneo mengi imeongezeka. Mbinu za kisasa za kupambana na mimea vamizi zimeokoa kaa-pweza wa Cameroon waliokuwa hatarini kutoweka, na idadi ya simba nchini Kenya iliongezeka kwa asilimia 25 kati ya mwaka 2010 na 2020. Katika baadhi ya maeneo, hata vifaru weusi wameanza kurejea upya.
Kuelewa kile kinachofanya kazi na kisichofanya kazi kwa wanyamapori na mifumo ikolojia ya Afrika ni muhimu sasa kuliko ilivyokuwa.
Kama vile ilivyokuwa miaka 100 iliyopita, maeneo ya hifadhi yako katikati ya sera zinazowekwa na Afrika kwa lengo la kuzuia maafa zaidi. Leo, kuna karibu maeneo ya hifadhi 9,000 kote barani Afrika. Haya ni pamoja na mbuga za wanyama kama Serengeti yenye upekee wa aina yake, pamoja na hifadhi nyingi ndogo za misitu na wanyamapori. Kwa pamoja, maeneo haya yanachukua eneo la kilomita za mraba milioni 4.37 (maili za mraba milioni 1.69) – karibu asilimia 15 ya bara zima la Afrika.
Ramani inayoonyesha maeneo yaliyohifadhiwa.
Maeneo haya yaliyohifadhiwa mara nyingi ni vyanzo vya thamani kubwa na nyenzo muhimu kwa serikali za Kiafrika. Utalii wa wanyamapori na asili ni biashara kubwa. Kulingana na ripoti ya mwaka 2019 ya Space for Giants na Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na mazingira, wanazalisha dola za Marekani bilioni 48 katika utalii wa kila mwaka na matumizi mengine. Wakati “uchumi wote wa wanyamapori” – unaojumuisha mauzo ya hewa ukaa pamoja na uwindaji na uvuvi, kwa akaunti zingine takwimu hupanda hadi dola za Marekani bilioni 250.
Nafasi hizi ni makazi ya aina nyingine za thamani pia. Ni sehemu za ibada za kitamaduni, uhusiano wa mababu, maisha ya mimea na wanyama, na nguvu inayoathiri ya uzuri wa asili. Lakini kusimamia eneo lililohifadhiwa mara nyingi huanzia katika kuamua ni maadili yapi yanapewa kipaumbele, na yapi yamepigwa marufuku.
Katika kipindi cha baada ya uhuru na zaidi, nchi nyingi zilihifadhi, kwa kiasi kikubwa, muundo wa polisi wa uhifadhi uliorithiwa kutoka kwa mamlaka ya zamani ya wakoloni. Kwa serikali, thamani inayopatikana kupitia utalii na, kwa ongezeko, masoko ya kaboni katika maeneo ya hifadhi ni kipaumbele. Hata hivyo, manufaa ya asili ambayo watu wanaoishi ndani na karibu na maeneo ya hifadhi wanategemea — kama vile uwindaji, uvuvi, kufuga mifugo yao, na kuvuna kuni — mara nyingi hayazingatiwi.

Mtindo unaoenzi yaliyokuwa yakifanyika awali na kukataza yanayofanyika sasa mara nyingi huitwa “uhifadhi wa ngome” na mjadala juu ya suala hili ni wa muda mrefu barani Afrika. Kikosi cha Field Force cha Kenya kiliweka mpango ambao unaathiri jinsi maeneo mengi ya hifadhi yanavyosimamiwa hadi leo. Katika baadhi ya nchi, walinzi wa wanyamapori hawawezi kutofautishwa na wanajeshi, wakivaa sare za kivita na kupewa silaha za kivita.
Wafuasi wa sheria kali za wanyamapori wanaashiria mawimbi makubwa ya ujangili katika bara la Afrika kama sababu ya jibu kali.
Lakini wakosoaji wake wanasema kwamba kwa muda mrefu, ni mbinu ambayo si nzuri kwa wanyamapori, na mbinu nzito zinazotenganisha jamii ambazo ni muhimu katika ulinzi wa asili.
Mjadala huu umechochewa na mfululizo wa migogoro ya hali ya juu. Kufukuzwa kwa wafugaji wa Kimaasai kutoka Hifadhi ya Ngorongoro nchini Tanzania, ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na walinzi katika Hifadhi ya Taifa ya Salonga nchini Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo (DRC), na madai ya kuteswa na askari wa wanyamapori katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kongo, yote yamezua gumzo na kuibua taswira mpya kwenye uhifadhi.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Programu ya Afrika katika Mpango wa Shirika la Rights and Resources, Patrick Kipalu, “Ukiukwaji wa haki za binadamu na kufukuzwa kwa watu wengi kwa jina la uhifadhi sio sehemu ya historia, au jambo ambalo lilifanyika wakati huo. Inafanyika sasa hivi.”

Mpango wa miaka mitano
Katikati ya kuongezeka kwa tahadhari kwa mienendo ya uhifadhi barani Afrika, mpango wa Kiafrika wa bioanuai ulitiwa saini na mataifa 196 mnamo mwaka 2022. Waliotia saini, ambao ni pamoja na serikali zote za Afrika, walikubali kupanua jumla ya idadi ya ardhi ya nchi kavu na baharini iliyolindwa kwa uhifadhi hadi asilimia 30 ya sayari ifikapo mwaka 2030.
Lengo hili, ambalo kwa kawaida hujulikana kama “30×30,” lilisherehekewa sana, lakini pia limezua wasiwasi kwamba linaweza kuja kwa gharama ya watu wanaoishi kwenye ardhi iliyopangwa kwa ajili ya uhifadhi. Duniani kote, hali hii inachochea mjadala upya juu ya jinsi maeneo ya hifadhi yanavyosimamiwa kwa sasa, na jinsi upanuzi mpya wa maeneo hayo unavyoweza kuonekana.
“Kuna maeneo ya hifadhi ambayo yameanzishwa kwa ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu na kuhamishwa kwa watu, lakini pia yako ambayo yamekuwa chanya na yameimarisha haki za jamii za asili katika maeneo yao,” alisema Mkurugenzi wa Shirika la Campaign for Nature, Brian O’Donnell, “Hakuna ukweli wa ulimwengu wote katika hili.”

Wakati makundi yote ya ulinzi, rasmi na yasiyo rasmi, yanapojumuishwa pamoja, karibu asilimia 20 ya ardhi ya bara la Afrika tayari imehifadhiwa, kwa mujibu wa Protected Planet. Ili kufikia lengo la “30×30” takriban kilomita za mraba milioni 2.4 (sawa na maili za mraba 930,000) za ardhi na za maeneo ya maji, zitalazimika kuongezwa kwa jumla ya sasa – ukubwa unaokaribia ule wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ambayo ni nchi ya pili kwa ukubwa barani Afrika.
Ardhi hiyo ingetoka wapi?
Wimbi jipya la maeneo ya hifadhi ya mtindo wa zamani, yaliyoanzishwa kupitia kuhamishwa kwa watu na kunyang’anywa ardhi, linaonekana halitakuwa jambo la kawaida tena. Maandishi ya utoaji wa 30×30 wa mpango wa bayoanuwai yanatambua “haki za watu wa asili na jumuiya za mitaa, ikiwa ni pamoja na haki juu ya maeneo yao ya jadi.”
“Serikali zinataka kufanya uhifadhi, na jamii zinafanya uhifadhi kama mtindo wa maisha,” alisema Kipalu. “Tofauti ni mbinu. Nadhani kuna uwezekano wa watu kukaa pamoja na kukubaliana jinsi ya kufanya hivyo. Kuunda maeneo ya hifadhi kwa mtindo wa kale wa ngome siyo njia muafaka.”

Ripoti za Mongabay
Wakati mijadala ya kimataifa kuhusu jinsi ya kulinda bayoanuwai ya sayari ikiendelea, Mongabay ilisafiri hadi nchi tatu za Afrika Mashariki ambapo wanyamapori wana mchango mkubwa katika uchumi: Rwanda, Uganda na Kenya. Katika kila nchi tulichagua aina tofauti ya mazingira na mfano wa ulinzi wa kinga.
Nchini Uganda, tulitembelea Mbuga ya Taifa ya Malkia Elizabeth, nyasi ya savanna kwenye mpaka na DRC, inayosimamiwa na Mamlaka ya Wanyamapori ya Uganda (UWA). Nchini Rwanda, tulichunguza Mbuga ya Taifa ya Msitu wa Nyungwe Forest National Park, msitu wa mvua wa milima ya tropiki ambao usimamizi wake ulitiwa saini na shirika lisilo la kiserikali la African Parks lenye makao yake nchini Afrika ya Kusini kwa ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi. Na nchini Kenya, tulisafiri hadi eneo kame la kaskazini ili kuzungumza na watu wanaohusika katika hifadhi za jamii zilizoanzishwa na shirika lisilo la kiserikali la Northern Rangelands Trust.

Katika filamu za asili, maeneo yaliyolindwa kama haya matatu mara nyingi huonekana kama mandhari ambayo hayajaguswa zaidi na wanadamu. Lakini ukweli ni kwamba mara nyingi watu wanaishi karibu au hata ndani yao.
Tembo hurandaranda ndani na nje ya miji iliyo karibu, sokwe huvamia mashamba ya mboga, na wawindaji haramu hujaribu kuwakwepa walinzi wa wanyamapori usiku kucha wanaporejea nyumbani kwa familia zao. Simba au nyati ambaye hutoa uzoefu wa kipekee mara moja moja kwa watalii wa kigeni, ni jambo la kawaida kwa majirani wanaoishi karibu naye.
Tulizungumza na maafisa wa serikali, walinzi wa wanyamapori, viongozi wa jamii, wamiliki wa biashara, na wananchi wa kawaida katika maeneo haya ili kuelewa kwa undani maisha yanavyokuwa pale yanapokuwa yameunganishwa moja kwa moja na mazingira na uhifadhi. Tulikutana na watu waliopitia miaka ya migogoro ya kivita, na ambao sasa wanakabiliwa zaidi na mabadiliko ya tabianchi na ukame. Wengine walikuwa wakijifunza kuzoea kazi mpya kama walinzi wa jamii baada ya kushawishiwa kuacha ujangili. Na baadhi yao walikuwa wamepoteza wapendwa wao kutokana na madhara ya upande wa giza wa uhifadhi.

Picha ya bango: Tembo wa Savannah katika Mbuga ya Taifa ya Malkia Elizabeth nchini Uganda. Picha na Ashoka Mukpo wa Mongabay.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 17/12/2024.