- Kuanzia mji wake mkuu wa Nairobi, Kenya sasa imeanzisha mabasi yanayotumia umeme kwenye mzunguko wa magari ya usafiri wa umma, au matatu, ambayo ni maarufu kwa kelele na uchafuzi wa hewa.
- Madereva walioteuliwa kuendesha mabasi haya yanayotengenezwa nchini China na kuunganishwa nchini humo wanasema abiria wanayapendelea kwa sababu ni kimya, yana kasi zaidi, na ni ya kustarehesha.
- Hata hivyo, utekelezaji wa mradi huu bado ni wa kiwango kidogo: bei ya basi moja la umeme, inayofikia dola 200,000 za Marekani, ni ya juu mno kwa wamiliki wengi. Hata hivyo, kampuni inayotengeneza mabasi hayo imeanza kuyakodisha kwa waendeshaji ili kuyafanya yawe nafuu zaidi.
- Changamoto nyingine ni suala la kuchaji betri, ambapo madereva wanasema mabasi yanatembea umbali mfupi kuliko ilivyotangazwa, huku vituo vya kuchaji vikiwa vitatu tu jijini.
NAIROBI — Zaidi ya mabasi 22,000 huwa kwenye mitaa yenye msongamano jijini Nairobi, yakibeba sehemu kubwa ya wakazi milioni 5.3 wa mji huo mkuu wa Kenya.
Mabasi ya abiria, maarufu kama matatu ya Nairobi, ambayo ni mali ya watu binafsi, yanajulikana kwa kupambwa kwa rangi kali na picha za wasanii wa muziki wa rap au vilabu vya soka vya Uingereza.
Miongoni mwa haya magari yanayotumia dizeli yenye kelele nyingi na kutoa moshi mzito, sasa kuna wageni wapya 35 ambao hawana kelele; wageni hao ni mabasi ya umeme yaliyounganishwa na kampuni ya humo humo nchini iitwayo BasiGo.
Kwa miaka sita sasa, Isaac Kamau amekuwa akihudumu kama dereva wa basi jijini Nairobi, akisafirisha abiria kutoka katikati mwa jiji hadi maeneo ya makazi. Mwaka 2022, alipata fursa ya kupewa mafunzo maalum ya kuendesha basi la umeme. “Kila mhitimu alitakiwa kuwa na historia nzuri ya kazi ili kupata nafasi kama hii,” Kamau aliiambia Mongabay.
Mafunzo yake yalilenga zaidi uendeshaji rafiki kwa mazingira na usalama, na sasa anafurahia gari lake jipya. “Abiria wanapendelea mabasi ya umeme kuliko yale yanayotumia mafuta. Hawahitaji kushawishiwa kupanda. Yanafariji zaidi, ni ya haraka na hayana kelele.”
Basi la Kamau ni miongoni mwa mabasi 35 ya umeme yanayofanya kazi jijini, huku mengine 14 yakitarajiwa kuongezwa mjini humo mwishoni mwa mwaka 2024. Kampuni ya BasiGo, ambayo huunganisha mabasi nchini Kenya kwa kutumia sehemu zinazotengenezwa na kampuni ya China ya CHTC, inasema tayari imepokea maagizo ya awali 500 kutoka kwa waendeshaji wa mabasi.

Mkurugenzi wa BasiGo, Moses Nderitu, aliiambia Mongabay: “Hatutegemei kuona mabasi ya mafuta ya dizeli yakitoweka ghafla. Kwa waendeshaji wengi, mafuta ya kisukuku ni suluhisho lililojaribiwa na kuthibitika kwa miaka mingi. Lakini sasa kuna uelewa kuwa kwa siku zijazo usafiri utakuwa wa mabasi ya umeme.”
Kampuni ya Oma Services Limited, mojawapo ya vyama vya akiba na mikopo vinavyohudumia usafiri wa umma jijini Nairobi, tayari ina mabasi manane ya umeme. Mwenyekiti wake, George Githinji, analenga kuwa wa kwanza kumiliki msafara wa mabasi yote ya umeme jijini.
“Nilipozuru nchini China, niliona magari ya umeme yakifanya kazi vizuri, ingawa wakati huo yalitegemea nyaya za moja kwa moja. Niliposikia mabasi ya aina hiyo yanayotumia betri za kuchaji yanajaribiwa nchini Kenya, nilifurahi na nikaamua kuanza kununua mabasi manne ya umeme,” alisema.
“Nina furaha kwamba nalinda mazingira, kelele ni kidogo, na moshi ni sifuri. Tunatunza vizazi vijavyo.”
Mkurugenzi Mtendaji wa Muungano wa Kitaifa wa Usafiri wa Umma (NAPTA), Charles Aholi, aliambia Mongabay: “Sekta yetu ya usafiri wa umma ina magari ya zamani yasiyotunzwa vizuri, mara nyingi yanasimama kwa muda mrefu yakisubiri abiria, hali inayoongeza kwa kiwango kikubwa utoaji wa moshi. Kuhamia usafiri wa umeme kunaweza kushughulikia tatizo hili na kutoa huduma safi na endelevu kwa mazingira.”
Hata hivyo, kwa gharama ya zaidi ya dola za Marekani 200,000 kwa kila basi, mabasi ya umeme ya BasiGo yanagharimu mara tatu zaidi ya yale ya dizeli wanayochukua nafasi yake. Ili kukabiliana na changamoto hii, BasiGo inawapa waendeshaji chaguo la kukodisha, ambapo kampuni za mabasi hufanya malipo ya awali ya shilingi milioni 1 (sawa na takriban dola 7,700), kisha huilipa BasiGo kiwango maalum cha ada kwa kila kilomita wanayoendesha, kiasi kisichopungua dola 3,000 kwa mwezi.
“Hivi sasa, hakuna basi lolote la umeme Nairobi linalomilikiwa moja kwa moja; yote yamekodishwa kwa muda wa miaka mitano. Tunalipa kwa kila kilomita tunayotembea, jambo linalofanya mpangilio huu kuwa mgumu,” alisema Nelson Mwangi, ambaye anamiliki basi la Super Metro Sacco.
Changamoto nyingine ya kuhamia mabasi ya umeme ni kuhakikisha betri zao hazikosi chaji. BasiGo inasema mabasi yake yenye viti 26 yana uwezo wa kusafiri kilomita 250, ilhali yale yenye viti 36 yanaweza kwenda kilomita 300.
Lakini dereva Stanley Kamau Mwangi, anayeanza kazi saa 12 asubuhi, anasema inapofika saa 10 jioni, anakuwa amefikisha kilomita 140 na chaji ya basi lake lenye viti 26, inakuwa imeshuka hadi kufikia asilimia 10.

“Lazima nichaji tena kufikia angalau asilimia 30 ili niendelee kufanya kazi jioni na nifike kilomita 200,” Mwangi anasema. Lakini anaongeza kwamba akipewa kuendesha basi kubwa zaidi, chaji yake humtosha siku nzima.
Kwa sasa, BasiGo ina vituo vitatu vya kuchaji jijini Nairobi. Hapo mabasi yanaweza kuchajiwa kikamilifu kabla ya saa mbili kuisha. Kwa kawaida mabasi huchajiwa usiku, lakini mara nyingi madereva hulazimika kurejea kituoni kwa kuchaji tena mchana.
Mkurugenzi wa kampuni hiyo anasema mtindo wa uendeshaji wa madereva una athari kubwa kwa kiwango cha chaji kinachodumu, lakini wanaweza kupanga siku zao kuchaji inapohitajika. “Wakati madereva wanapopumzika kati ya saa 5 asubuhi na saa 9 alasiri, tunawaruhusu kuchaji kwa muda mfupi wa mchana,” aliambia Mongabay.
“Kadri wadau zaidi wanavyoingia sokoni, tunaweza kutarajia kuongezeka kwa vituo vya kuchaji, kwa sababu upungufu wa miundombinu ya kuchaji bado ni changamoto kubwa,” alisema Nderitu.
Kampuni pia imeahidi kuwa na modeli mpya na basi kubwa zaidi, hatua iliyochukuliwa kutokana na maoni ya waendeshaji wa Kenya. Basi hilo litakuwa na uwezo wa kusafiri hadi kilomita 400 (takriban maili 250) kwa chaji moja.
Magari ya umeme ni sehemu muhimu ya mipango ya serikali ya Kenya kupunguza utoaji wa gesi chafu kwa asilimia 32 kufikia mwaka 2030. Kufikia mwaka 2025, serikali inalenga angalau asilimia 5 ya magari yote yaliyosajiliwa nchini yawe ya umeme.
Ili kuwawezesha wananchi kumudu, serikali imepunguza kodi kwa watengenezaji na wanunuzi wa magari ya umeme na kuanzisha ada maalum ya umeme kwa magari ya umeme, kufanya gharama ya kuchaji kuwa nafuu zaidi.
Nderitu alisema serikali bado inaweza kufanya zaidi kuunga mkono sekta hii: “Ikiwa wazo la kuondoa kaboni katika usafiri ni kupambana na mabadiliko ya tabianchi, basi motisha inapaswa kuwa kubwa zaidi ili kuruhusu ukuaji wa haraka.”
Picha ya bango: Moja ya mabasi ya umeme ya BasiGo jijini Nairobi. Picha kwa hisani ya BasiGo.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 12/12/2024.