- Hakuna taarifa za kuthibitisha kuonekana kwa tumbili wa patas wa kusini walio katika hatari kubwa ya kutoweka nchini Tanzania kwa zaidi ya mwaka mmoja, jambo linaloongeza hofu kuwa spishi hiyo inazidi kukaribia kutoweka kabisa.
- Mwaka2021, ilikadiriwa kuwa tumbili wa patas wa kusini waliobaki porini walikuwa chini ya 200, ambao walikuwa wamebaki katika sehemu ya magharibi ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
- Watafiti wamewaomba wananchi kuripoti iwapo watawaona wanyama hawa ambao wana aibu lakini wanaonekana kwa urahisi kutokana na mwonekano wao wa kipekee. Hata hivyo, matukio ya kuonekana kwaoyalikuwa mawili tu, tukio la kwanza likiripotiwa mwaka 2022, na la pili mwaka 2023. Hakukuwa na taarifa ya tukio lolote mwaka 2024.
- Spishi hii inatarajiwa kujumuishwa tena kwenye orodha ya IUCN ya “Primates in Peril”; orodha ya spisji 25 za nyani zilizo katika hatari zaidi duniani — kwa mwaka wa pili mfululizo.
Kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa, hakujakuwa na taarifa zilizothibitishwa za kuonekana kwa tumbili wa kusini wa patas, ambao wako katika hatari kubwa ya kutoweka, katika makazi yao ya mwisho yanayojulikana, magharibi mwa Tanzania. Mwaka 2021, ilikadiriwa kuwa walikuwa wamebaki chini ya tumbili 200 wa aina hii wenye viungo vyepesi na virefu, wanaojulikana kitaalam kama Erythrocebus baumstarki, ambao walipatikana kwenye maeneo ya misitu ya wazi katika ukanda huo na sasa wanasayansi wana hofu kuwa spishi hiyo inakaribia kutoweka kabisa.
Awali, tumbili wa patas wa kusini alikuwa anachanganywa na tumbili wa patas wa mashariki, Erythrocebus patas pyrrhonotus, ambaye hupatikana kwa wingi zaidi katika maeneo mbalimbali ya Afrika Mashariki na Kati, kuanzia Kenya ya kati hadi kaskazini mashariki mwa Chad. Wanyama hawa wanafanana kwa mwonekano, na wote huishi kwenye maeneo ya misitu ya wazi yenye urefu wa mwinuko unaokaribiana. Lakini hata kabla ya mwaka 2015, wakati ambapo patas wa kusini bado walikuwepo nchini Kenya; spishi hizi mbili zilikuwa zimetenganishwa na mamia ya kilomita. Kuna uwezekano mkubwa kuwa hazijawahi kuchanganyika.
Mwonekano wao unaofanana pamoja na tabia nyingine kama vile kuwa na maeneo makubwa ya kuishi na kula gundi kutoka kwenye miti ya miiba inayojulikana kitaalam kama Acacia drepanolobium (whistling thorn); ulisababisha ukosefu wa juhudi maalum za uhifadhi kwa ajili ya kulinda tumbili wa kusini wa patas. Kutokana na ukweli kwamba aina hii ya nyani wana tabia ya uoga, na huonekana mara chache, vilifanya tafiti za kisayansi za kutambua tofauti za spishi kukosekana kwa muda mrefu.
Hata hivyo, Yvonne de Jong, mtaalamu wa masuala ya jamii ya nyani na mwenzake, Tom Butynski, walifanya kazi kuhakikisha tumbili wa kusini wa patas wanatambuliwa rasmi kama spishi tofauti mnamo mwaka 2021, na wakafanikiwa kuiweka kwenye orodha ya “Primates in Peril: Spishi 25 za Nyani Zilizoko Katika Hatari Zaidi Duniani 2022–2023”.

Tumbili wa kusini wa patas wanatarajiwa kuorodheshwa tena kwenye orodha hiyo mwaka 2024. Kwa mujibu wa watafiti, taarifa ya mwisho ya kuonekana kwa spishi hii ilikuwa ya dume mmoja mzima mnamo Juni 2023. Mwaka 2022, kulikuwa na matukio mawili tu yaliyothibitishwa: kundi la tumbili wanane na mmoja aliyekuwa peke yake. Maeneo yote matatu walipoonekana yalikuwa ndani ya misitu ya acacia katika sehemu za magharibi ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Tanzania.
De Jong na Butynski wamekuwa wakihifadhi kumbukumbu ya matukio ya kuonekana kwa tumbili wa kusini wa patas tangu mwaka 2004. Kwa kipindi cha miaka 20 iliyopita, matukio hayo yamekuwa yakipungua sambamba na kupungua kwa idadi ya tumbili hao na maeneo wanayoweza kuishi.
Kulingana na tafiti waliyochapisha mwaka 2009 na 2021, wataalam hao walielezea Pori la Akiba la Grumeti, Pori la Akiba la Ikorongo na Eneo la Usimamizi wa Wanyamapori la Ikona kuwa ngome muhimu kwa ajili ya spishi hii. Haya yote ni maeneo ya hifadhi yanayopakana sehemu ya juu ya ukanda wa magharibi mwa Serengeti, unaoelekea Ziwa Victoria.
“Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni, tumbili hawa hawajaripotiwa tena katika maeneo hayo matatu,” alisema De Jong alipokuwa akizungumza na Mongabay. “Inaonekana kwamba kwa sasa spishi hii inapatikana tu ndani ya sehemu ya magharibi ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.”
Kwa ujumla, De Jong alisema kuwa eneo ambalo tumbili hawa walikuwa wanasambaa — ambalo hapo awali lilijumuisha sehemu za kati na kaskazini mwa Tanzania hadi kusini mwa Kenya, limepungua kwa takribani asilimia 85 tangu mwanzoni mwa karne ya 20.
“Hili linapaswa kuwa angalizo kwa mamlaka za Tanzania zinazohusika na uhifadhi wa bayoanuai ya taifa, pamoja na mashirika ya kitaifa na kimataifa ya uhifadhi,” aliongeza De Jong.

Katika matukio hayo machache ambayo tumbili wa kusini wa patas wameonekana porini na kuratibiwa kwa kutumia koodinati za mahali walipoonekana, Butynski na De Jong wamezitumia taarifa hizo kukadiria ueneaji wao wa sasa ambao ni mdogo sana.
Mwanasayansi Mkuu wa Grumeti Fund,shirika lisilo la kiserikali linalotekeleza shughuli za uhifadhi na maendeleo ya jamii katika ukanda wa magharibi mwa Serengeti, George Lohay, alisema kuwa wafanyakazi wa Grumeti pamoja na waongozaji wa watalii kutoka Singita, kampuni ya utalii, wa kiikolojia ya hapa nchini, ndio waliorekodi tukio la pili la mwisho la kuwaona tumbili wa kusini wa patas mwaka 2022. Lohay alisema kuwa miaka 15 iliyopita, wanyama hawa walikuwa wanaonekana mara kwa mara katika Eneo la Usimamizi wa Wanyamapori la Ikona lenye ukubwa wa hekta 24,200 (sawa na ekari 59,800).
Mwaka 2022, wenzake waliona jumla ya tumbili tisa pekee. “Kwa bahati mbaya, idadi yao katika eneo hili imetoweka kabisa tangu wakati huo,” alisema.
Lohay aliongeza kuwa Grumeti Fund inapanga kuwasilisha pendekezo kwa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) ili kufanya utafiti wake binafsi kuhusu tumbili hao mwaka ujao. Mpango huo unatarajiwa kujumuisha kuweka kamera za kunasa picha za wanyamapori (camera traps) katika makazi ya mwisho ya tumbili wa kusini wa patas huko Serengeti magharibi.
“Kipaumbele chetu kwa sasa ni kubaini idadi ya sasa ya tumbili hawa na kutambua sababu za kupungua kwao,” alisema. “Hii itatuwezesha kutoa mapendekezo ya uhifadhi yaliyo na msingi wa kisayansi.”
Ni jambo la kuleta wasiwasi kwamba mtandao mpana wa watoa taarifa unaohusisha watafiti, waongozaji wa watalii, wamiliki wa kambi na wafugaji, ulioundwa na kuendelezwa na Butynski na De Jong kwa kipindi cha miaka 20, mwaka 2024, haukuripoti tukio lolote la kuwaona tumbili hawa.
Kwa sura yao ya kipekee yenye “barakoa” nyeusi usoni na migongo yenye rangi ya udongo mwekundu, spishi hii haiwezi kuchanganyikana na mnyama mwingine yeyote.

“Wafugaji ni chanzo kizuri sana cha taarifa, hasa linapokuja suala la kumbukumbu za kihistoria,” alisema Butynski. “Watu kwa kawaida hutambua spishi hii kwa urahisi wakionyeshwa picha au mchoro.”
Ikiwa tumbili wa kusini wa patas sasa wamebaki tu katika eneo la magharibi mwa Serengeti, kuna uwezekano mkubwa kwamba spishi hiyo imekwamia hapo. Maeneo yaliyo nje kidogo ya mpaka wa magharibi wa hifadhi hiyo yamejaa watu na mbwa wao wa kufugwa, ambao ni tishio kubwa kwa tumbili hawa wanapojaribu kufikia vyanzo adimu vya maji.
“Mbwa wa kufugwa huwaua nyani, wakiwemo tumbili wa patas ambao huishi zaidi ardhini,” aliongeza Butynski.
Aidha, alieleza wasiwasi wake kuwa bila hatua za haraka za uhifadhi kuchukuliwa, tumbili wa kusini wa patas, kundi la pili la jamii ya nyani barani Afrika, wanaweza kutoweka kabisa katika miaka ya hivi karibuni. Nyani wa red colobus wa Miss Waldron (Piliocolobus waldroni), waliokuwa wakipatikana Ghana na Côte d’Ivoire, hawajaonekana tena porini kwa zaidi ya miaka 40 na wanaaminika kuwa wametoweka kabisa.
“Inaonekana kuna uwezekano mkubwa kwamba tumbili wa kusini wa patas ndio watakaofuata — tena mapema,” alisema Butynski.
Picha ya bango: Tumbili wa kusini wa patas, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Tanzania. Picha kwa hisani ya Katie Sanborn.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 09/12/2024.