- Shirika lisilo la kiserikali la utunzaji mazingira la Wetlands International lilikuwa na matarajio makubwa lilipoanza mradi wa Chanzo mpaka Baharini (Source to Sea project) katika Afrika Mashariki mwaka 2021 ambao ulihusisha ardhi oevu iliyoko katika Bonde la Ufa na mikoko inayopatikana kwenye Bahari ya Hindi.
- Hata hivyo, utekelezaji wa mradi ulikumbwa na vikwazo,ikiwemo kutofikiria muda ambao ungetakiwa kuwaweka pamoja watendaji wa serikali, azaki na vikundi vya kijamii katika maeneo ya mradi, mipango ambayo haikuzingatia hali halisi na ugumu wa kujenga mawasiliano na wenyeji.
- Wetlands International waligundua mapema kuwa walitakiwa kuzingatia uboreshaji wamaisha ya wenyeji kwanza kabla ya nadharia za kutunza ardhioevu,na usimamizi shirikishi wa vyanzo vya maji.
- Mpaka sasa mradi umetoa mchango muhimu katika kuboresha maisha ya wanavijiji, ustawi wa maeneo ya vyanzo vya maji na kujenga uelewa wa jamii kuhusu mikoko na ardhi oevu,na kuchangia katika sera zinazohusu usimamizi wa vyanzo vya maji.
Miaka mitatu baada ya mradi wenye matumaini makubwa ya kurejesha ubora wa ardhi oevu katika maeneo ya Afrika Mashariki, Mhifadhi Julie Milonga anasema kuwa amejifunza mambo mengi kuhusu thamati ya hatua moja baada ya nyingine, japo ni ndogo, katika kufikia malengo makubwa ya uhifandi na utunzaji wa mazingira. Mradi wa Kutoka Chanzo mpaka Bharini ulilenga kutunza na kulinda maeneo ya ardhi oevu yaliyoko katika Bonde la Ufa na mikoko inayopatikana na Bahari ya Hindi na wakati huo huo kuboresha maisha ya jamii zilizoko katika maeneo ya mradi na kuwajengea uwezo wa kuhimili mabadiliko ya tabianchi.
“Tulianza na maono makubwa katika kutekeleza mradi huu,” anasema Mulonga, ambaye ndiye Mkurugenzi wa Wetlands International kwa upande wa Afrika Mashariki, “lakini nikiangalia tulipoanzia nakiri kuwa tulikuwa na malengo makubwa mno ambayo tulitarajia kuyafikia mapema mno.”
Mradi ulianza kutekelezwa mwaka 2021 ukihusisha maeneo makubwa ya kiikologia ambayo ni Eneo la Maziwa yaliyoko katika Bonde la Ufa, likianzia kutoka Ziwa Albert na Nyanda za Juu za Ethiopia kwa upande wa kaskazini hadi Ziwa Tanganyika kwa upande wa Kusini na eneo la kiikologia la mikoko la Afrika Mashariki likianzia kusini mwa Somalia mpaka Msumbiji likijumuisha eneo la Lamu nchini Kenya, Delta ya Rufiji iliyoko Tanzania na Delta ya Mto Zambezi nchini Msumbiji.


Maeneo Muhimu ya utekelezaji wa mradi yapo Ethiopia, Kenya na Tanzania, ambayo ni pamoja na Hifadhi ya Taifa ya Abijata-Shalla Lakes National Park, iliyopo Ethiopia. Hapa ni kituo muhimu cha ndege wanaohamahama na limeteuliwa kuwa eneo muhimu la ndege wa aina mbalimbali.
Eneo jingine ni Ziwa Turkana, ambalo ni ziwa kubwa zaidi la jangwa duniani, linalodumu. Mabonde ya Mito Ziway Shalla na Omo-Turkana ambako maeneo muhimu ya ndege yaliko yameharibiwa vibaya kwa sababu ya ukataji miti ovyo, uchafuzi wa mazingira, matumizi makubwa ya maji na nyanda za malisho na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Hali hii imesababisha uhaba wa maji na kukosa uhakika wa chakula kunakoathiri mamilioni ya watu wanaoishi katika maeneo hayo.
Mradi huu unatekelezwa na Wetlands International, shirika lililojikita katika kuhifadhi na kuboresha eneo la majibaridi lenye makazi ya ndege na wanyama mbalimbali ambao wako hatarini kutoweka.
Wataalamu wanakadiria kuwa zaidi ya nusu ya maeneo ya ardhi oevu duniani yametoweka tangu mwaka 1900 kwa sababu ya kilimo, uchimbaji madini na upanuzi wa miji.
Mulonga anasema kuwa sababu kubwa ni utekelezaji mbovu wa sera na sheria zilizopo katika nchi mbalimbali. Pamoja na kwamba nchi zimesaini makubaliano mbalimbali ya kulinda na kuhifadhi mazingira kama 2022 Global Biodiversity Framework (GBF), ambayo yanazitaka nchi kuboresha na kurejesha uasili kwa asilimia 30 ya maeneo ya ardhi oevu na asilimia 30 ya maeneo yenye vyanzo vya maji, utekelezaji wake umekuwa hafifu.
Kwa hiyo, mradi wa Kutoka Chanzo mpaka Baharini (Source to Sea) unakuja na mwelekeo mpya kuhifadhi maeneo hayo.
Wetlands International walitambua kuwa ili kuleta mafanikio yanayotarajiwa, mradi lazima utekelezwe kwa kuzingatia uwanda kuliko eneo moja fulani. “Tumekuja na mtazamo tofauti kidogo,” anaeleza Mulonga. “Hatuwezi tena kufanya kazi katika maeneo maalumu madogo madogo. Ni lazima tuzingatie yale yanayotokea eneo la juu kwenye vyanzo mbalilmbali vya maji na sehemu ya chuni ambako maji yanakofika na kushirikiana na jamii zote zilizoko katika eneo hilo kubwa ili kuleta mabadiliko chanya.”


Mbinu hii ya utekelezaji wa mradi siyo mpya. Inafahamika pia kama usimamizi jumuishi wa rasilimali za maji. Mbinu hii inayozingatia uwanda mzima na siyo eneo moja dogo imebadilisha mkakati na mahitaji ya nguvukazi. Shirika ninajenga uwezo wa kuelewa na kukabiliana na mahitaji ya jamii na kuboresha mahitaji yao ya maisha kwa lengo la kuweza kufanya tathmini ya utekelezaji, kusimamia na kuboresha ikolojia ya ardhi oevu.
Hata hivyo, siku zote mwanzo huwa mgumu. Utekelezaji wa mradi haukuanza kwa namna iliyotarajiwa. Shirika lilipofanya tathmini mwishoni mwa mwaka 2022, liligundua mambo mengi magumu, yakiwemo makadirio ya chini ya muda uliohitajika wa kuwaleta pamoja watendaji wa serikali, wananchi, na makundi mbalimbali ya kijamii, ukiachilia mbali mipango isiyotekelezeka, na vikwazo vya mawasiliano na jamii za wenyeji.
Mulonga anasema kuwa ilibidi waweke pembeni maono yao mpaka pale walipojenga imani kwa jamii zilizopo katika maeneo ya mradi na kushughulikia mahitaji yao ya msingi.
Mfano mmoja ni pale Kenya kwenye Kaunti ya Turkana, eneo kame lenye joto kali na ambalo limekumbwa na ukame mkali kuanzia mwaka 2018. Wenyeji wa eneo hili ni wafugaji wanaohamahama. Wetlands International iliposhawishi Shirika la Maendeleo la Wafugaji wa Turkana (Turkana Pastoralist Development Organization (TUPADO) kuungana nao katika utekelezaji wa mradi, Mratibu wa TUPADO, Mohammed Ahmed Yusuf, aliwapeleka kutembelea jamii mbalimbali katika eneo hilo.
Yussuf anasema kuwa hatua hii ni muhimu ili watekelezaji wa mradi waelewe hali halisi ya jamii na kutoa nafasi kwa wanajamii kueleza matarjio yao kutokana na utekelezaji wa mradi.
Wanajamii wengi ni maskini. Hivyo Wetlands International ilitambua kuwa kipaumbele cha jamii ni kuboresha maisha na kupunguza umaskini. Hilo ni jambo ambalo lilitakiwa kutekelezwa kwanza kabla ya kuleta nadharia ya utunzaji wa ardhi oevu na usimamizi shirikishi wa rasilimali za maji.
Pale Naipa, kijiji kilichopo kando ya mto Turkwel, eneo la kati katika Kaunti ya Turkana, wenyeji walitaka wasaidiwe kuboresha kilimo ili kukabiliana na mafuriko na ukame. Yusuf anaeleza kuwa kwenye vijiji vya wavuvi katika eneo la Ziwa Turkana kama Lokipetot na Todonyang, wenyeji walitaka vichanja ili waweze kukausha na kuhifadhi samaki kwa njia bora zaidi. Nao wafugaji wa Kapua walitaka kuboreshwa kwa nyanda za malisho ili kujihakikishia upatikanaji wa chakula cha mifugo hasa wakati wa kiangazi.
Mukonga anasema kuwa walijifunza kuweka maono yao kando na kushughulikia mahitaji ya msingi ya wanajamii.
Baada ya miaka mitatu ya utekelezaji wa mradi wa Kutoka Chanzo Mpaka Baharini, Yusuf anasema kuwa kumekuwa na mabadiliko makuwa kwa jamii zinashoshiriki utekelezaji wa mradi huo ambazo zinaonekana katika ubora wa mazingira, na maisha ya wananchi. Sasa wafugaji wa Kapua wanapata malisho ya kutosha kwaajili ya mifugo yao wakati pale Naipa wanafunzi wanapata chakula cha kutosha kutokana na kuongezeka kwa maeneo ya kilimo na kuboresha mbinu za kilimo. Utapiamlo pia umepungua.
Hatua hizi pia zimepunguza uvamizi wa maliasili ambazo wananchi hutegemea kwa maisha yao, uvuvi, na maji. Kadhalika maliasili zinalindwa kwa kupunguza mmomonyoko wa udongo. Mazingira kwa ujumla wake yamekuwa bora zaidi.

Kulingana na maelezo ya Yusuf, mradi ulitekeleza mahitaji ya jamii na wananchi wanaelewa umuhimu wa kutunza maeneo yenye maliasili. Anasema kuwaTUPADO wanataka kupanua eneo lao la kufanyia kazi ikiwemo kufanya utafiti wa kujua jinsi shughuli za kibinadamu pembezoni mwa mto Omo zinavyoathiri ubora wa maji katika Ziwa Turkana. Wanataka pia kuhusisha shughuli zao na zile zinazofanyika katika nchi jirani ya Ethiopia na nchi nyingine ambazo mradi unatekelezwa.
Kumekuwa na mafanikio mengine pia. Mulonga anasema kuwa moja ya mafanikio makubwa ni kuongezeka kwa uelewa kuhusu mikoko na maeneo oevu miongoni mwa makundi mbalimbali yaliyohusika. Mafanikio ya pili ni kupata fursa kwa Wetlands International kushawishi sera zinazohusu usimamizi wa rasilimali za maji, kwa mfano, kwa kusaidia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuandaa mpango wa usimamizi wa mikoko katika Bonde la Rufiji.
Mradi wa Source to Sea umepangwa kuendelea hadi mwishoni mwa mwaka 2024, lakini Mulonga anasema kuwa utaendelea ikiwa ufadhili zaidi utapatikana.
Hata hivyo, maono makuu ya kuboresha, kutunza na kuhifadhi maeneo ya ardhi oevu yenye umuhimu wa kipekee katika Bonde la Ufa na mikoko katika pwani ya Afrika Mashiriki bado yako hai na anasema kuwa anaridhika na mabadiliko chanya yaliyotokana na utekelezaji wa mradi mpaka sasa. “Yale maono makuu yasifutike katika vichwa vyetu. Tupige hatua moja baada ya nyingine na hatimaye tutafika tunakotaka,” anasema Mulonga.
Picha ya bango: Ziwa Turkana. Picha na Aocrane, kupitia Flickr (CC BY-NC-ND 2.0)
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 06/08/2024.