- Michelle na Jeremy Muchilwa, ambao ni watoto wa familia moja kutoka nchini Kenya wenye umri wa miaka 19 na 16, ni mfano bora wa vuguvugu la vijana linalokua ulimwenguni kote, likipambana na uharibifu wa mazingira na athari za mabadiliko ya tabianchi katika jamii zao.
- Shule zilipofungwa kutokana na mlipuko wa UVICO 19, mtu na dada yake wakaona kuna fursa ya kujifunza kuhusu teknolojia na mfumo wa ekolojia. Hatimaye wakaanzisha shirika linaloitwa Osiepe Sango (Marafiki wa Ziwa Victoria) likiwa na lengo la kuondoa takataka za plastiki zilizomo katika ziwa hilo. Kutokana na juhudi zao wameweza kuanzisha programu mbalimbali, ikiwemo programu tumizi ya kufuatilia takataka za plastiki na kifaa kinachozamishwa ndani ya maji ili kuondoa takataka hizo.
- Vijana hao wameshinda tuzo nyingi za kimataifa, ikiwemo National Geographic Young Explorer Award na Diana Award, na juhudi zao kutambuliwa na Planeteer Alliance.
- Mwezi Juni Michelle na Jeremy waliongea na Mongabay kuhusu malengo yao, kazi wanazofanya na matarajio yao ya siku zijazo.
Katika miaka ya karibuni vijana kutoka ulimwenguni kote wamekuwa mstari wa mbele katika kupambana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi. Vijana hawa wenye viwango mbalimbali vya elimu katika masuala hayo wamefanya kazi kubwa ya kuelimisha na kuhamasisha vijana wengine wa rika yao ili washiriki kikamilifu katika kampeni mbalimbali za kuhakikisha kuwa maisha yajayo yanakuwa endelevu.
Mfano mzuri ni vijana kutoka familia moja huko Kenya, Michelle na Jeremy Muchilwa, wenye umri wa miaka 19 na 16, ambao walianzisha shirika la Osiepe Sango (Marafiki wa Ziwa Victoria) lenye lengo la kuondoa uchafu wa plastiki katika Ziwa Victoria ambalo ndilo kubwa kuliko maziwa yote ya maji safi barani Afrika. Ziwa hili pia limetanda katika nchi tatu za Afrika Mashariki; Kenya, Uganda na Tanzania.
Wakati ugonjwa wa UVICO-19 ulipojitokeza mwaka 2020, mwezi Machi, shule nchini Kenya zilifungwa. Michelle alikuwa na umri wa miaka 15 na Jeremy miaka 12. Vijana hao waliona hii kama fursa kwao na waliporuhusiwa na wazazi wao, walijikita katika mambo waliyoyapenda badala ya kuendelea na masomo kwa njia ya mtandao. Jeremy alizama katika mambo ya teknolojia ambayo alikuwa akiyapenda, akijifunza kutengeneza programu mbalimbali. Michelle alijikita kwenye mifumo mbalimbali ya kiteknologia kupitia programu ya TED-Ed art school, ambayo ilimpa mwanga kuhusu bayoanuai, ikolojia na masuala ya mazingira katika ulimwengu. Somo moja kuhusu maji lilijadili umuhimu wa bahari, mifumo ya vyanzo vya maji baridi na kuonyesha uchafuzi unaotokana na takataka za plastiki. Michelle alihamasika na akapata habari za Ocean Heroes Boot Camp, mafunzo kuhusu uchafuzi wa mazingira unaotokana na takataka za plastiki na akaomba kushiriki. Alimshawishi pia Jeremy kujiunga na mafunzo hayo.
Ushiriki wao katika mafunzo hayo kwa njia ya mtandao uliwapa wazo la kurejesha hali bora ya awali ya mazingira ya Ziwa Victoria. Kuanzia hapo, kazi zao zimepata kutambuliwa na mashirika kama National Geographic Young Explorer Award ambayo ilimpatia tuzo Michelle, na Diana Award, ambayo walipata wote pamoja. Kadhalika kazi zao zimechapishwa katika vyombo mbalimbali vya habari vya nchini mwao na vya kimataifa, ikiwepo makala iliyochapishwa mwezi Aprili mwaka 2021 kwenye jarida la TIME for Kids, yenye kichwa cha habari “Kid Heroes of the Planet,” ambayo ilihusu jitihada wanazofanya katika kuondoa takataka za plastiki kutoka Ziwa Victoria.
Mpaka sasa, Jeremy na Michelle wamekusanya zaidi ya tani kumi za takataka za plastiki ambazo zimefuatiliwa kupitia programu tumizi ya simu waliyoitengeneza ijulikanayo kama Ziwa Safi, ambayo hukusanya taarifa kuhusu utupaji wa takataka ziwani humo. Kadhalika lengo la programu tumizi hiyo ni kukusanya takwimu kwa kutumia sayansi shirikishi ya raia, ili kuonyesha ukubwa halisi wa uchafuzi wa Ziwa Victoria, unaotokana na takataka za plastiki. Taarifa hizi zitawasaidia watendaji wa serikali na waandika sera na mashirika mengine yanayojihusisha na utunzaji wa mazingira kutafuta suluhisho la uchafuzi wa Ziwa Victoria.
Taarifa iliyotolewa na shirika la mazingira la International Union for Conservation of Nature (IUCN) inasema kuwa zaidi ya tani 460 millioni za plastiki huzalishwa kila mwaka na kati ya hizo, tani ishirini huwa ni takataka. Takataka nyingi hutokana na vifaa vya plastiki vinavyotumika mara moja na kutupwa kama chupa, kofia, vichungi vya sigara, mifuko ya bidhaa madukani, kofia, vikombe na mirija.
Vijana hao waliongea na Mongabay mwezi Juni kuhusu kazi zao na jinsi walivyoanzisha shirika lao. Mazungumzo yao yalikuwa hivi:

Mongabay: Tueleze wewe ni nani, ili watu wakufahamu vizuri.
Michelle Muchilwa: Naishi mjini Kisumu, Kenya. Nina umri wa miaka 19 na ni muanzilishi mwenza wa shirika la Osiepe Sango. Mimi ni mshindi wa tuzo kadhaa za kimataifa ambapo mwaka 2012 nilipata tuzo ya National Geographic Young Explorer, Diana Award na Planeteer. Na hivi karibuni nimehitimu Chuo cha Uongozi cha Afrika. Ninapata msukumo kutoka kwa hayati Wangari Maathai kutokana na mafanikio ya kipekee katika nyanja ya uhifadhi wa mazingira, licha kunyanyaswa na kuwekwa kizuizini mara kwa mara.
Juhudi zake zimesaidia kuhifadhi maeneo ya kijani nchini Kenya, kama Msitu wa Karura, ambao ni maarufu nchini Kenya. Navutiwa pia na Vanessa Nakate kutoka Uganda na Greta Thunberg ambaye alianzisha vuguvugu la Fridays Future. Wote ni wanaharakati waliosimama imara bila kuyumba katika kupigania haki ya kupambana na athari za mabadilikjo ya tabianchi.
Mongabay: Na huyu Jeremy Muchilwa ni nani?
Jeremy Muchilwa: Mimi nina umri wa miaka 16. Naishi Kisumu, nchini Kenya, na pia ni mwanzilishi mwenza wa shirika la Osiepe Sango. Mwaka wa 2022 nilipata Diana Award. Mimi ni mshiriki wa Planeteer na ni mwanafunzi wa Shule ya White Oaks. Shauku yangu na hamasa ya kuhifadhi mazingira nimeipata kwa Dr Jane Goodall, hasa kutokana na namna alivyofanya utafiti wa sokwe na jinsi wanavyohusiana katika maisha yao. Pia navutiwa na hayati Wangari Maathai kwa jinsi alivyovumilia madhila mengi ili kufikia malengo yake ya kuhifadhi na kulinda mazingira.
Mongabay: Osiepe Sango ni jina la kipekee katika majina ya mashirika. Mlipataje wazo la kubuni jina hili na mantiki yake ni nini, hasa kwa kuzingatia hali ya Ziwa Victoria?
Jeremy Muchilwa:Kwa lugha ya Dholuo (inayozungumzwa na Waniloti wa mtoni na ziwani nchini Kenya), “Osiepe” maana yake ni “rafiki” na “Sango” ni moja wapo ya majina ambayo wenyeji wa asili huliita Ziwa Victoria. Mababu zetu na wazazi wetu walitumia majina hayo katika lugha zao na hivyo kujenga na kuimarisha uhusiano wa kijadi kati ya ziwa hilo na wenyeji wanaoishi maeneo yanayolizunguka. Jina la Victoria halihusiani kwa namna yoyote ile wala halina umuhimu kwa wenyeji, kwani ni jina la Malkia wa Uingereza na alilianzisha John Speke, ambaye alikuwa mzungu wa kwanza kuliona ziwa hilo. “Sango” ndilo jina asili na tunalitumia ili kufufua uhusiano uliopo baina yake na wenyeji wa asili ya maeneo haya, na kusisitiza umiliki wao wa ziwa hilo badala ya kuona kana kwamba raslimali hiyo ni mali ya serikali.

Michelle Muchilwa: Tulichagua kufanyia kazi Ziwa Victoria kwasababu linatuhusu sana, ni sehemu ya maisha yetu. Tumezaliwa na kuishi karibu na ziwa maisha yetu yote, kutoka utoto wetu hadi sasa tunaelekea kuwa watu wazima. Ni kama nyumbani kwetu. Nilipokuwa mdogo sikuona ziwa likifunikwa na takataka za plastiki na maji yalikuwa mazuri tu. Nasikitika sana ninapoona uchafuzi unaoendelea siku hizi.
Kwa bahati mbaya uchafuzi huu hauathiri ziwa peke yake, unaathiri pia jamii kwani idadi na aina ya samaki vyote vimepungua. Pwani ya ziwa imefunikwa na takataka za plastiki. Lakini ziwa hili ni ikolojia muhimu kwani hapa ndipo chanzo cha Mto Nile. Kadhalika ziwa hili ni tegemeo la maisha ya mamilioni ya watu katika nchi tatu za Afrika Mashatriki. Kwa hakika kutoweka biyonuia kama ndege, viboko,fisi maji, baadhi ya aina ya samaki na kaa, kunaleta wasiwasi.
Mongabay: Ni miradi gani ambayo Osiepe Sango mnatekeleza?
Michelle Muchilwa: Miradi yetu inajumuisha mambo mengi ili kupambana na uchafuzi unaotokana na takataka za plastiki. Mbinu zetu hubadilika kulingana na mahitaji ya wakati huo.
Kazi yetu ya awali ilikuwa “Rejesha Mazingira Bora ya Ziwa Victoria” ambapo tulipanga kujenga kituo cha kuchakata takataka kama njia moja wapo ya kudumisha usafi. Lakini taarifa na takwimu ambazo tulizikusanya pamoja na Taasisi ya Kenya ya Utafiti wa Samaki na Viumbe vya Majini (KMFRI) ilibainisha kuwepo kwa ombwe kubwa katika jamii kati ya uelewa kuhusu hatari inayotokana na uchafuzi unaotokana na takataka za plastiki na athari ya uchomaji wa takataka za plastiki.
Tulibaini kuwa jamii ilikuwa inahitaji elimu, hivyo tukaacha mpango wa kujenga kiuto cha kuchakata takataka na kuanza kuelimisha na kuhamasisha jamii.
“Rejesha Mazingira Bora ya Ziwa Victoria” sasa ukawa mradi wenye lengo la kutoa elimu kwa umma kuhusu athari za kimazingira na za kiafya zinazotokana na takataka za plastiki. Kwanza tulifanikiwa kubainisha tatizo kupitia vyombo mbalimbali vya habari vya kitaifa na kuongeza mawasiliano na jamii kwa ujumla kuchukua hatua za pamoja ili kupunguza takataka.
Jeremy Muchilwa: Programu yetu ya pili ilijikita kwenye programu tumizi tuliyotengeneza inayoitwa Ziwa Safi. Wazo la kutengeneza nyenzo hii tulilipata tulipofanya mazungumzo na Dr Chrispine Nyamweya, mtafiti mwandamizi wa sayansi kutoka KMFRI, ambaye alichangia utaalamu wake ili kupata muundo wa awali wa nyenzo hiyo. Shirika la LakeHub lilitupatia sehemu ya kufanyia kazi na ushauri kupitia mkurungenzi mtendaji wake Dorcas Owinoh. Lakini utengenezaji wa nyenzo hiyo ni juhudi zetu wenyewe. Nyenzo hii inasaidia kukusanya taarifa na takwimu mbalimbali wakati wa kufuatilia mambo kama aina ya taka na mtengenezaji wake. Hii inatuongezea kuaminika pindi tunapokwenda kumkabili mtengenezaji wa bidhaa kuhusu taka zao. Kabla ya nyenzo hii tulikuwa tukiandika taarifa zote kwenye karatasi, hali ambayo ilikosa ufanisi kwani tulikuwa tukifanya kazi katika maeneo ya fukwe ambayo hupata mafuriko mara kwa mara.
Programu tumizi ya Ziwa Safi hutumia sayansi shirikishi ya raia ili kubaini maeneo yaliyoathiriwa na uchafuzi na hurahisisha kurekodi taarifa na takwimu. Kadhalika nyenzo hii husaidia kufuatilia ufanisi wa kazi zetu na kutuelekeza vilipo vituo vya karibu vya kuchakata ambavyo vinaweza kupokea takataka zetu. Vilevile huweza kubaini nembo ya biashara kwenye chupa za plastiki zilizochakaa, jambo linalotusaidia kutenganisha aina ya takataka kwa urahisi.

Michelle Muchilwa: Programu yetu ya tatu ilikuwa kuandaa Mkutano wa Vijana wa Nam Lolwe (Nam Lolwe Youth Summit (NALYS). Katika programu yetu ya kwanza, tulihudhuria warsha mbalimbali ambapo vijana wengi waliuliza tuliwezaje kufahamu mambo tuliyokuwa tunawaeleza kuhusu uchafuzi wa takataka za plastiki na wangewezaje kushiriki katika vuguvugu hilo.
Baada ya kushiriki mafunzo kupitia Ocean Heroes Virtual Boot Camp, tulihamasika na kuandaa mafunzo kama hayo. Ndipo mimi, Jeremy na vijana wengine watano kutoka Asia na Marekani ya Kaskazini tukaandaa Mkutano wa Mam Lolwe ili kuwajengea uwezo vijana. Mkutano huu ulikuwa na lengo la kutoa fursa kwa vijana kujifunza na kuibua mawazo mbalimbali na kuuliza maswali ya kuwaongezea uelewa. Mkutano ulijikita katika kuwajengea vijana uwezo ili waweze kutatua changamoto za mazingira.
Mikutano ya vijana tunayoandaa hujikita katika mazingira ikilenga mazingira yaliyopo ambayo yanahitaji kuchukuliwa hatua. Kwa mfano, mikutano ya Kisumu inajikita katika mazingira ya Ziwa Victoria na ya Mombasa inahusu Bahari ya Hindi. Kwa kushirikiana na Planeteer Alliance, mikutano hiyo imeweza kuwafikia vijana wengi duniani, katika nchi zaidi ya 17.
Programu yetu ya nne ni mpango wa kutengeneza mashine inayoitwa Waterborne Autonomous Litter and Trash Extraction Robot [WALTER], ambayo imetengenezwa na Jeremy kwa kushirikiana na wahandisi vijana. WALTER ni kifaa kinachofanana na ndege, isiyo na rubani, lakini chenyewe hufanya kazi chini ya maji. Hukusanya takataka za plastiki katika Ziwa Victoria, ingawa kwa sasa kinakusanya takataka zilizopo juu ya maji. Wanakifanyia kazi ili kiweze kukusanya takataka zilizoko chini ya maji. Kifaa hiki kinatumia umemejua, hivyo hakiongezi uchafuzi wa mazingira ya ziwa kwa namna yoyote ile.
Mongabay: Unafikiri shirika hili la vijana linapata mafanikio gani? Tunaweza kutathmini mafanikio hayo?
Michelle Muchilwa: Mashirika yanayoongozwa na vijana mara nyingi huleta mabadiliko chanya kwani hutumia ubunifu kutafuta suluhisho za matatizo badala ya kubaki na njia zilizozoeleka. Kwa mfano tunaweza kupima mafanikio ya Osiepe Sango kwa kulinganisha malengo yetu na maboresho thabiti yanayoonekana hasa kwenye suala hili la kuondoa takataka za plastiki. Tumetoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu uchafuzi unaosababishwa na takataka za plastiki. Ziwa Safi inabaini aina ya takataka za plastiki zilizopo, ukiachia mbali lengo la kuwajengea uwezo vijana hapa Kisumu pamoja na nchi nyingine duniani. Zaidi ya hayo, Osiepe Sango limekusanya tani kumi za takataka kutoka Ziwa Victoria na kuwapa elimu zaidi ya vijana 1,000.

Jeremy Muchilwa: Tulipoanza hatukuwa na uzoefu wa kuendesha asasi ya kiraia, kwa hiyo tukatumia utaalamu wetu. Vijana siku zote huleta mawazo mapya na kuondoa mfumo dume na hivyo kuleta suluhisho yenye tija. Zipo asasi ambazo zimekuwa zikifanya kazi kwa zaidi ya miaka hamsini, lakini hazijatatua matatizo ya mazingira ya Ziwa Victoria. Sisi vijana hatujaanza miaka mingi lakini matunda ya kazi yetu yanaonekana.
Mongabay: Familia na marafiki wamewasaidia vipi katika kutekeleza majukumu ya Osiepe Sango?
Michelle Muchilwa: Wametusaidia sana. Tulipoanza hatukuwa na chanzo cha uhakika cha kupata fedha…walitusaidia. Wazazi wetu wametupa mtaji kwaajili ya kutekeleza programu zetu. Wametusaidia kulipa gharama za usafiri na wametupa moyo ili tuendelee kutekeleza kila hatua ya malengo yetu. Hatukuwa na wafadhili wakubwa lakini tumekuwa tukipata ruzuku ndogo ndogo.
Jeremy Muchilwa: Marafiki zetu wengine wamekuwa wakijitolea kukusanya takataka, jambo ambalo ni muhimu kwani shirika letu lina wafanyakazi wasiozidi 15.
Mongabay: Je, kuna changamoto zozote mnazokabiliana nazo?
Jeremy Muchilwa: Kuna shida kidogo katika kutekeleza majukumu ya shule na kufanya kazi za shirika. Kwahiyo kuna mikutano muhimu ambayo sikuweza kuhudhuria ili niendelee na masomo. Ziwa Safi imetupa shida kidogo kwani kukidhi matakwa ya watumiaji mbalimbali kumekuwa na changamoto kubwa. Tumepata mrejesho mbalimbali ambao ulisababisha tufanye mabadiliko ya muundo wa nyezo mara tatu ili kukidhi matarajio ya watumiaji.
Jeremy Muchilwa akiwaeleza wageni katika Banda la Mafunzo la Wake wa Marais kuhusu nyenzo ya Ziwa Safi na WALTER wakati wa Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi wa Afrika 2023. (Picha familia ya Muchilwa.)
Michelle Muchilwa: Changamoto nyingine ilikuwa kusajili shirika letu, kwani wakati huo wote tulikuwa hatujatimiza umri wa miaka 18. Hivyo kisheria nyaraka zetu hazikutambuliwa na serikali. Kukosa wafadhili kwa programu za gharama kama WALTER bado ni changamoto na hili linachangiwa pia na umri wetu, kwani sio rahisi kuaminiwa katika muktadha wa taaluma.
Mongabay: Mna matarajio gani ya siku zijazo? Mna wasiwasi wowote?
Jeremy Muchilwa: Bado tuna muda wa kuokoa mazingira ya Ziwa Victoria na ikolojia nyingine za aina hiyo. Naamini tutafanikiwa. Kenya imepiga hatua nzuri ya matumizi ya nishati jadidifu ingawa bado kuna kazi kubwa mbele. Lakini nina wasiwasi mkubwa kuhusu ongezeko la mabadiliko ya tabianchi na athari zake. Kuendelea kutumia nishati ya mafuta kunaongeza athari hasi kwa mazingira na bayonuai.
Michelle Muchilwa: Nafikiria sana kuhusu vizazi vijavyo, kwani huenda hawatakuwa na cha kurithi kutokana na uchafuzi wa mazingira unaoendelea. Jeremy na mimi tumejikita kupambana na uchafuzi wa mazingira ili kubadili hali iliyopo na kuleta matumaini mapya ya maisha endelevu kwa vizazi vijavyo.
Picha ya bango: Jeremy (wa kwanza kushoto) na Michelle Muchilwa (aliyesimama katikati) na wafanyakazi wenzao wakiwahamasisha wanajamii kuhusu uchafuzi wa takataka za plastiki mwaka 2023. Picha na Osiepe Sango.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 31/07/2024.