- Wanasayansi hivi karibuni walibainisha uwepo wa spishi sita mpya za jongoo katika Milima ya Udzungwa, nchini Tanzania.
- Spishi hizo sita ni miongoni mwa maelfu ya sampuli zilizokusanywa na watafiti waliokuwa wakichunguza ikolojia ya misitu katika eneo hilo pamoja na Hifadhi ya Asili ya Magombera iliyo karibu.
- Hifadhi ya Magombera iliharibiwa na ukataji miti wa kibiashara katika miaka ya 1970 hadi 1980, na maeneo yaliyoathirika sasa yamejaa mizabibu pori ijulikanayo kama lianas.
- Hata hivyo, timu zinazofanya kazi katika eneo husika zinaamini kuwa utofauti na wingi wa jongoo katika mapori ya liana ni sawa na ile misitu ambayo haijaguswa, jambo linaloashiria kuwa huenda maeneo hayo yana uwezo wa kurejesha hali ya msitu bila mwingiliano mkubwa wa binadamu.
Wanasayansi hivi karibuni walibainisha spishi sita mpya za jongoo, ikiwemo moja kutoka kwenye jenasi mpya kabisa, katika Safu ya Milima ya Mashariki ya Tanzania. Ugunduzi huu umefanya idadi ya spishi mpya zilizopatikana katika Milima ya Udzungwa tangu mwaka 2014 kufikia 81 — jambo linalothibitisha kwa mara nyingine utajiri mkubwa wa bioanuwai katika safu hizi za milima zilizojitenga na maeneo mengine. Jongoo hao waliogunduliwa hivi karibuni wanawasaidia watafiti kutathmini urejeshwaji wa mfumo wa ikolojia.
Jongoo mmoja kati ya waliogunduliwa hivi karibuni, ambaye kwa kitaalam anajulikana kama, Udzungwastreptus marianae, hukua hadi kufikia urefu wa takriban sentimita 3, na hupatikana katika misitu iliyoko juu ya mita 1,000 kutoka usawa wa bahari. Profesa wa mfumo wa kisayansi wa wanyama na jiografia ya wanyama katika Makumbusho ya Historia Asilia ya Denmark, Henrik Enghoff, ambaye ameelezea spishi 69 kati ya 81 zilizogunduliwa katika milima hiyo, anasema jenasi hiyo imepewa jina Udzungwastreptus kama njia ya kutambua utajiri wa ajabu wa viumbehai katika Milima ya Udzungwa.

Udzungwastreptus marianae, ambao ni aina mpya ya jongoo iliyogunduliwa hivi karibuni katika Milima ya Udzungwa, Tanzania, na jongoo wengine hutambaa juu ya sakafu ya msitu kama vichwa vidogo vya treni, huku wakila mabaki ya mimea iliyokufa na takataka za kikaboni. “Baadhi ya jongoo walikuwa na sifa za kipekee, kama miguu yenye rangi angavu au magamba ya nje yenye kung’ara,” anasema Alain Ngute, mtaalamu wa ikolojia ya misitu ya tropiki ambaye alikuwa sehemu ya timu iliyofanya utafiti katika Milima ya Udzungwa na kukusanya jongoo hao.
Ngute anaeleza kuwa jongoo husaidia katika mzunguko wa virutubisho na kuendeleza rutuba ya udongo, pamoja na kuongeza hewa kwenye udongo na kuhifadhi unyevu — mambo ambayo ni muhimu kwa ukuaji wa mimea na urejeshwaji wa misitu.
Katika maeneo ya misitu iliyoharibika na kufunikwa na mizabibu pori mizito ijulikanayo kama lianas, uwepo wa jongoo unaashiria kwamba mfumo wa ikolojia unaanza kurejea hali yake ya awali. “Jongoo wanaweza kusaidia kurejesha maeneo haya kwa kuvunjavunja mabaki ya viumbehai na kurahisisha ukuaji wa miche na miti michanga,” anasema Ngute.
Hata hivyo, jongoo hawakuwa chaguo la kwanza la utafiti kwa Ngute. Alikulia katika nyanda za juu za magharibi mwa Cameroon, uzoefu ambao anasema ulimsaidia kuendeleza uhusiano wa karibu na misitu ya tropiki. Hapo awali, alivutiwa na kufanya utafiti juu ya athari za uharibifu wa misitu kwa jamii za ndege katika eneo lake la nyumbani.
Baadaye alipokuwa akifanya utafiti kwa ajili ya shahada ya uzamifu (PhD) katika Milima ya Udzungwa, ndipo mwelekeo wake ukabadilika kutoka kwa ndege na kuelekea kwa jongoo.
“Mwanzoni sikupenda sana kufanya kazi na viumbe hawa, kwani nilikuwa na hofu kutokana na hadithi za kuogopesha za utotoni zinazowahusu,” anasema Ngute. “Hata hivyo, kadri nilivyozidi kujifunza kuhusu ikolojia yao na harakati zao msituni, taratibu nilianza kuvutiwa nao na kushangazwa na maisha yao.”
Wakati msimamizi wa Ngute, Andrew Marshall, ambaye ni mwanasayansi wa uhifadhi, alipoanza kufanya kazi Tanzania mwishoni mwa miaka ya 1990, alionyeshwa maeneo makubwa ya misitu iliyoharibika katika sehemu nyingine ya Safu ya Milima ya Mashariki ya Tanzania.
Kulikuwa na mizabibu tu iliyokuwa imeota juu ya kila kitu,” Marshall anakumbuka. “Sikuwa na wazo lolote kuhusu kilichokuwa kinaendelea, lakini watu waliokuwepo waliniambia kuwa hayo yalikuwa maeneo ya msitu yaliyokuwa yameharibika, ambapo miti ilikuwa imekatwa na mizabibu ikachukua nafasi yote.”
Mizabibu pori (lianas), ambayo hukita mizizi ardhini, hufanana na nyoka wakubwa wanapojizungusha juu ya miili ya miti katika misitu ya mvua. Licha ya mwonekano wao wa kuvutia, mizabibu hii pia ni vimelea vinavyoweza kudhoofisha au hata kuua miti. Katikati ya mwaka 2007, Marshall alianzisha maeneo madogo ya utafiti wa uoto ndani ya Msitu wa Magombera ili kuchambua kasi ya urejeshwaji wa mazingira katika maeneo yaliyoharibiwa na ukataji miti wa kibiashara miongo kadhaa iliyopita.
Matokeo ya awali yalionyesha kuwa mizabibu inayopatikana kwa wingi ijulikanayo kisayansi kama Ucaria africana, na inayojulikana kwa jamii ya Kihehe kama mtonasimba (yaani “mkono wa simba”) kwa sababu ya miiba yake inayong’ang’ania, ilikuwa inaziba maeneo ya msitu yaliyokuwa yanajaribu kupona. Hali hii ilidhoofisha uwezo wa msitu kujiimarisha tena. Nusu ya maeneo ya majaribio yalihudumiwa kwa kukata mizabibu hiyo kwa kutumia mkasi maalum (secateurs), yalionesha kuimarika kwa ukuaji wa miti kwa kiasi kikubwa ndani ya kipindi cha miaka mitano.

Lakini baada ya miaka ya utafiti zaidi katika Milima ya Udzungwa, Marshall pamoja na wenzake wa kimataifa wanaofanya kazi chini ya mpango wa Forest Restoration and Climate Experiment (FoRCE) wameweza kupata mtazamo mpana na wa kina zaidi kuhusu mizabibu pori.
Viumbe wasio na uti wa mgongo, wakiwemo jongoo, wanawasaidia kuona taswira kubwa zaidi ya mazingira hayo.
Jamii za jongoo, pamoja na viumbe wengine kama mchwa na siafu, zinaonekana kuwa nyingi na mbalimbali katika maeneo yenye mizabibu kama ilivyo katika misitu ya asili isiyosumbuliwa. Hii inaweza kuashiria kwamba maeneo yenye mizabibu si ya kufa bali ni maeneo hai yanayoweza kugeuka kuwa msitu kamili kwa kuwepo kwa vichocheo sahihi vya kimazingira au vya usimamizi, anasema Marshall.
“Haya maeneo ambayo kwa juu yanaonekana kuwa yameharibika sana yamechanganyika ovyo na hayafanani kabisa na kile tunachokifikiria kama msitu — lakini kwa kweli yamejaa viumbe mbalimbali vinavyosaidia mfumo huo kuendelea kuishi,” anaeleza.
Marshall na timu yake wanaamini kuwa mizabibu inaweza kufanya kazi kama “vitambaa vya kufunika majeraha”, kwa maana ya kulinda miche ya miti katika maeneo yaliyoathirika dhidi ya vitisho vya nje.
“Ukiyaondoa kabisa hayo maeneo ya juu, unakuwa umeondoa lile tabaka la ulinzi, na tunaona katika (maeneo yetu ya utafiti) kwamba maeneo yaliyofunguliwa huathiriwa na mambo kama tembo, ukame au hata watu wanaokuja na kukata miti,” anasema.
“Sio rahisi tu kusema: toa mizabibu, halafu miti itaota yenyewe.”
Ingawa swali la kama mizabibu huzuia au husaidia urejeshwaji wa misitu ya kitropiki bado halijapata jibu la moja kwa moja, vita ya kuendeleza ‘nadharia ya vitambaa vya majeraha’ imekuwa ngumu na yenye changamoto. Maeneo ya utafiti wa uoto huko Tanzania hayajawahi kuwa sehemu rahisi za kufanya kazi.
“Wakati tunapofanya tathmini, tunalazimika kutambaa chini ya mizabibu, na maeneo hayo huwa yenye joto kali, unyevunyevu, jasho na yaliyojaa miiba na wadudu wengi – hivyo tunachomwa sana na pia kukwaruzwa sana,” anasema Marshall.

Kwa bahati nzuri, jongoo ni rahisi zaidi kufanyiwa utafiti kuliko mchwa au siafu wanaoishi katika makoloni makubwa na ambao ni shida kufuatilia. Baadhi ya siafu, kama wale wa jenasi Dorylus wanaojulikana kwa Kiswahili kama siafu, huuma binadamu kwa uchungu mkubwa endapo watakatiza kwenye njia zao.
Kupata spishi mpya za jongoo ni sehemu ya kuvutia ya kazi ya uchunguzi wa kiikolojia, anasema Marshall, na inaonekana kuwa Safu ya Milima ya Mashariki ya Tanzania (Eastern Arc Mountains) ina utajiri mkubwa wa viumbe hawa. Hali hii haiwezi kusemwa kuhusu maeneo mengine ambako timu ya FoRCE hufanya kazi.
“Duniani kote, makundi mbalimbali ya viumbe wasio na uti wa mgongo (invertebrates) huwa yanatawala kwa njia tofauti, hivyo hakuna makubaliano ya pamoja kuhusu ni kundi gani hasa ni bora kufanyiwa utafiti,” anafafanua. Katika misitu ya kitropiki ya kaskazini mwa jimbo la Queensland, Australia, ambako wanafunzi wa Marshall wanafanyia utafiti kuhusu “nadharia ya vitambaa vya majeraha,” jongoo wanaopatikana ni “wachache sana” ikilinganishwa na maelfu ya viumbe wengine wanaokula mabaki ya mimea ardhini, kama mende na nzi.
“Jongoo tunawaona kwa nadra sana,” anasema.
Kwa namna utafiti unavyoendelea hapa Tanzania, wanasayansi wanatarajia kugundua jongoo wapya, na cha kuvutia zaidi, aina mpya za uyoga pia. Ingawa bado haijafahamika kwa nini hali hii hutokea, aina ndogo kabisa za uyoga — nyingi zikiwa hazizidi nusu milimita kwa urefu — huota juu ya jongoo na viumbe wengine wadogo wa ardhini, anasema Enghoff, mtaalamu wa wanyama wa Copenhagen, Denmark, anayechunguza sampuli zinazotumwa kwake kutoka Milima ya Udzungwa.
Uyoga huu mara nyingi huota kwenye sehemu za miili ya jongoo wa kiume na wa kike ambazo hugusana wakati wa kujamiiana. Kwa njia hii, uyoga unahakikisha kwamba mbegu zake zinarutubika kwa mafanikio.
Aina moja ya uyoga, iliyokutwa ikiota pembeni mwa Udzungwastreptus marianae – jenasi na spishi mpya ya jongoo iliyoelezewa na Enghoff na wenzake — ilielezewa kwa mara ya kwanza mwaka 2016, miaka kadhaa kabla ya mwenyeji wake (jongoo huyo) kutambulika rasmi.
Mtaalamu huyo wa wanyama kwa sasa anafanyia kazi chapisho lingine – la 12 katika mfululizo unaoitwa “Mountain of Millipedes” – ambalo litazungumzia spishi nyingine saba mpya kutoka Milima ya Udzungwa.
“Kwa vitu nilivyonavyo, vinanitosha kwa maisha yangu yote,” anasema Enghoff, ambaye amefanya kazi katika taaluma yake kwa zaidi ya miaka 50.
“Sitakaa bila kufanya kazi.”
Picha ya bango: Mtafiti Alain Senghor K. Ngute akitengeneza kielelezo cha jongoo. Picha kwa hisani ya Hamidu Mnendendo.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 26/03/2024