- Wakazi wa Kijiji cha Wavuvi cha Munje, kusini mwa bandari ya Mombasa nchini Kenya, wameanzisha eneo maalum la kufunga uvunaji wa samaki aina ya pweza ili kuhakikisha wanakuwa na uvuvi endelevu.
- Kabla ya zoezi hilo, idadi ya pweza waliokuwa wakivuliwa kwenye miamba ya karibu na pwani ilikuwa ikipungua kutokana na ongezeko la wavuvi waliokuwa wakitumia mbinu zisizo rafiki kwa mazingira na zilizolenga aina hiyo ya samaki wenye faida kubwa.
- Kufuatia juhudi za awali za kudhibiti uvuvi wa pweza kukosa mafanikio, kikundi cha usimamizi wa fukwe cha kijiji hicho kilishirikiana na shirika lisilo la kiserikali (NGO) kujifunza mbinu zilizotumiwa na maeneo mengine kupambana na tatizo hilo kwa mafanikio.
- Mawasiliano ya wazi na yanayohimiza makubaliano na kuchukuliana yamewezesha wanajamii kuunga mkono mpango huo, na sasa kijiji kinatarajia msimu wa pili wa mavuno wenye mafanikio ifikapo mwezi Februari.
MUNJE, Kenya — Kuanzia katikati ya mwaka 2023, eneo maarufu la kuvua samaki aina ya pweza lililoko karibu na pwani ya kijiji cha Munje lilionekana wazi na tulivu kwa namna ya kushangaza. Wanachama wa kikundi cha usimamizi wa fukwe cha kijiji hicho (BMU) walikuwa wakililinda kwa umakini ili kuhakikisha hakuna anayevua pweza katika sehemu hiyo ya miamba. Mwishoni mwa mwezi Oktoba, kikundi hicho cha BMU kilijitosa baharini kuvuna matunda ya uvumilivu wao.
Munje ni kijiji kidogo cha wavuvi kilichopo kwenye pwani ya Bahari ya Hindi, takribani kilomita 60 kusini mwa bandari ya Mombasa. Wakazi wake wanategemea kilimo na uvuvi kama vyanzo vya chakula na mapato. Uvuvi wa pweza, hasa aina ya Octopus vulgaris, kwenye miamba ya baharini ni miongoni mwa shughuli zenye faida kubwa zaidi kwao.
Hata hivyo, pweza walikuwa wakipungua kwa kasi kutokana na uvunaji uliopitiliza na uharibifu wa miamba ya matumbawe ambayo ndiyo makazi yao. “Enzi za baba zetu, kulikuwa na pweza wengi sana hapa, lakini siku hizi mvuvi akienda kuvua, anapotoka baharini, anarudi na kilo moja au mbili tu za pweza,” alisema Mwenyekiti wa BMU, Hamisi Bakari Chimete, wakati akizungumza na Mongabay mwezi Agosti. “Hii ndiyo sababu iliyotufanya tuamue kufunga eneo moja la uvuvi wetu ili kuwapa pweza nafasi ya kuzaliana na kuongezeka, na pia kuruhusu miamba ya matumbawe kujirekebisha.”

Kuvua kidogo ili kuvuna zaidi
Kila jamii ya wavuvi nchini Kenya ina kikundi cha usimamizi wa fukwe (BMU), ambacho ni kamati ya wakazi wanaosimamia na kulinda rasilimali za baharini za jamii yao. BMU ya Munje iliamua kutenga sehemu ya bahari kwa ajili ya pweza na kuamuru isiguswe kabisa hadi baada ya miezi mitatu au minne ambapo huifungua kwa uvuvi kwa siku chache tu.
Kufunga eneo hilo kunaruhusu idadi ya pweza waliopo ndani yake kuongezeka tena. Katika kipindi hicho cha kufungwa, mayai ya pweza yaliyotagwa kwenye maficho salama ya miamba huanguliwa, na pweza wachanga hukua kwa kasi hadi kufikia karibu ukubwa wao kamili kabla ya kipindi kifupi cha uvuvi kuruhusiwa.
Endapo mpango huo utasimamiwa vizuri, kufungwa kwa eneo hilo kunapaswa kusababisha ongezeko la mavuno ya pweza, pamoja na spishi nyingine zinazofaidika na ulinzi, hivyo kuboresha mapato ya wavuvi na pia afya ya mazingira ya uvuvi.
Rahisi kusema kuliko kutenda
Munje walijaribu mpango huo mwanzoni kabisa. Hata hivyo, kwa mujibu wa Chimete, wanajamii wengi hawakuelewa kwa nini sehemu hii ya mwamba wa matumbawe ifungwe. Uamuzi wa kufunga haukuzingatiwa, na wavuvi — wakiwemo vijana wengi wasio na uzoefu waliovutiwa na faida ya uvuvi wa pweza — waliendelea kuvua pweza katika eneo hilo lililofungwa, na wakati mwingine waliharibu mwamba huo kwa kutumia mbinu haribifu za uvuvi.
Uongozi wa BMU ulitafuta msaada kutoka kwa watu wenye uzoefu kwa jaribio jipya, kupitia mojawapo ya mikutano ya wazi iliyoandaliwa na serikali ya kaunti ya Kwale. Mwaka 2021, walikutana na shirika lisilo la kiserikali la Coastal and Marine Resource Development (COMRED), shirika la Kenya linalofanya kazi na BMU 15 katika Kaunti za Kwale na Kilifi. COMRED huzingatia mbinu shirikishi zinazounganisha sayansi na usimamizi kupitia mafunzo ya uongozi, ufuatiliaji wa uvuvi, pamoja na kuanzisha na kusaidia maeneo ya baharini yanayosimamiwa na jamii za wenyeji.
“Jaribio letu la kwanza la kufunga eneo la kuvua pweza lilishindikana kwa sababu jamii haikuwa imehamasishwa vya kutosha kulichukulia kuwa ni mradi wao wenyewe,” alisema Chimeta. “Wavuvi wengi walilipinga wakidai kuwa huu ni mradi wa serikali wa kugeuza eneo hilo kuwa hifadhi ya baharini.” Kwa msaada wa COMRED, BMU ilianza juhudi za kujenga uungwaji mkono wa jamii kwa ajili ya kufunga tena eneo jipya la pweza.

Afisa Mradi wa COMRED anayeshughulika na usimamizi wa uvuvi Maryline Chebet, aliieleza Mongabay kwamba wavuvi mara nyingi huogopa kwa kudhani kwamba kufungwa kwa eneo la kuvua pweza kutawatenga kabisa na eneo hilo, kama inavyokuwa wakati hifadhi za baharini zinapotangazwa rasmi. Hata hivyo, alisema kwamba ulinzi wa miamba ya bahari iliyo karibu na Munje unasimamiwa na BMU, ambayo ndiyo itakayopitia matokeo na kuamua yenyewe ni kwa muda gani itaendelea na mpango wa kufunga eneo na kuruhusu uvuvi kwa vipindi maalum.
“Tulichukua baadhi ya wanajamii kwenda kujifunza kwa wenzao katika jamii ya Lamu, ambako wamefanikiwa kuanzisha kufungwa kwa eneo la kuvua pweza,” alisema.
“Baada ya ziara ya kujifunza kwa wenzao, wanajamii pamoja na COMRED walianza kampeni kubwa ya kuyahamasisha makundi mbalimbali ndani ya BMU, yaani wavuvi wanaotumia vifaa tofauti vya uvuvi, wanajamii kwa ujumla, BMU za jirani, na hili lilifanyika kupitia mikutano ya kujenga makubaliano na mabaraza katika jamii.”
Salim Juma Shee alikuwa mmoja katika ya kundi la wavuvi 20 waliopinga vikali kufungwa kwa eneo hilo.
“Kati ya timu yangu, mimi ndiye niliyekuwa nikienda mara kwa mara kwenye mikutano kuhusu kufungwa kwa eneo la pweza ofisini kwa BMU. Sikukosa mkutano hata mmoja, lakini sikukubaliana na walichokuwa wakisema,” alisema. “Nina familia inayonitegemea na kazi yangu kuu ni uvuvi, lakini sasa walikuwa wanasema tusivue?”
Sababu mojawapo ya kupinga mpango huo ilikuwa ukosefu wa taarifa kuhusu jinsi kufungwa kwa eneo hilo kutakavyofanyika na wapi watu kama yeye bado wangeendelea kuruhusiwa kuvua; eneo lililopendekezwa kufungwa lilikuwa dogo zaidi ya uwanja wa mpira wa miguu — takribani mita za mraba 4,000 (eka 2.5) — lakini lilikuwa miongoni mwa maeneo mazuri zaidi ya uvuvi pwani.
“Siku moja, BMU walituita sisi wavuvi waliopinga kufungwa kwa eneo hilo. Lakini kati ya 20, ni wawili tu tuliokwenda: mimi na mdogo wangu wa kiume. Walitueleza kwa kina kuhusu umuhimu wa kulinda eneo hilo, ndipo tulipobadilisha mawazo na kuanza kutetea jambo hilo,” alisema Shee.
Shee alijiunga na timu ya watu 10 waliokuwa wakifuatilia na kulinda eneo lililowekwa. Jukumu lake lilikuwa kuogelea kwenye mwamba wa matumbawe na kuangalia dalili za uharibifu au ugonjwa wa mwamba. Wavuvi kutoka kijijini walilazimika kuvua katika maeneo mengine.
Baadhi ya watu katika kijiji walisema kufungwa kwa eneo hilo kuliwalazimisha kufanya mabadiliko makubwa zaidi. Walisema waligeukia kilimo, wakipanda aina za mahindi na mtama zinazokomaa haraka pamoja na mboga za jadi kama vile sukuma wiki ili kula na familia zao na kufidia mapato waliyopoteza. Mwuuzaji mmoja wa samaki, Mwanaharusi Ali, alisema kufungwa kwa eneo hilo kumelazimisha kufanya mabadiliko makubwa zaidi. Aliiambia Mongabay kwamba yeye huuza pweza kwa kiasi kikubwa, lakini kwa kuwa eneo la uvuvi lilifungwa, alilazimika kusafiri kwa umbali kama wa kilomita 20 kwenda kununua samaki katika mji jirani.
“Nilitumia shilingi 500 za Kenya [dola za Marekani 3] kwa ajili ya usafiri kwa sababu ya bei kubwa za mafuta. Ilikuwa ghali sana, kwa sababu gharama ya usafiri ilikuwa zaidi ya pesa niliyokuwa nayo kununua samaki. Nililazimika kujinyima,” alisema. “Na ninaporudi na mizigo, huwa ninachanganyikiwa kwa sababu sijui jinsi ya kukata samaki kwa njia itakayoniwesesha kupata fedha za kufidia gharama ya usafiri na pia kupata faida.”
Chebet alisema wengi wa wauzaji wa samaki huuza aina mbalimbali za samaki, na kwa kuwa kufungwa kwa eneo hilo kunahusu sehemu ndogo tu ya eneo la uvuvi la kijiji, kunapaswa kuwa na samaki wengine wa kuuza, au pweza wanaovuliwa katika maeneo mengine.

Alama za mwanzo za mafanikio
Jumamosi mwezi Oktoba, siku iliyochaguliwa kwa ajili ya ufunguzi wa kwanza wa uvuvi wa pweza wa Munje, hali ya hewa ilikuwa mchanganyiko wa jua na mvua iliyokuwa ikinyesha juu ya paa za bati na minazi na miembe yenye matunda mengi ambayo hayajaiva. Ilionekana kuwa karibu kila mtu kijijini alikuwa pwani.
Bahari ilikuwa tulivu yenye mawimbi madogo. Samaki wadogo na pweza wa baharini walionekana kwenye ufukwe. Watoto walikimbia kila mahali, na wazee walijiunga na wageni chini ya hema kuangalia vijana wanawake wakiimba nyimbo na kucheza ngoma za jadi. Wengine walikuwa ufukweni wakipokea makapu yaliyojaa pweza kutoka kwa wavuvi waliokuwa majini.
Uvuvi wote ulikuwa unafanywa na wanachama wa kitengo cha usimamizi wa pwani. Wakati samaki hao watakapouzwa, faida hugawanywa kwa utaratibu waliokubaliana; mfuko wa ustawi wa jamii hupata asilimia 30, wanachama wa BMU asilimia 30, pesa za kuendeleza ofisi ya BMU asilimia 20, na wavuvi waliovua pweza hupata asilimia 20 ya faida.
Kassim Ali Siwa alifika ufukweni na mtumbwi wake uliojaa pweza majira ya mchana. Hapo awali, hata yeye alikuwa akipinga kufungwa kwa eneo hilo, lakini sasa anasema anafurahia kuunga mkono mpango huo.
“Nilivua pweza wengi, nilianza kuvua saa 3 asubuhi na kurudi saa 12:20 mchana,” alisema. “Nilipata zaidi ya kilo 30 za pweza; kabla ya kufungwa kwa eneo hili, nilikuwa navua kati ya kilo moja na nusu na kilo mbili tu za pweza.”
Katika siku tatu, wanachama wa BMU walivuna kilo 650 za pweza. Wavuvi walichukua baadhi ya samaki hao kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kwao, lakini sehemu kubwa ya mavuno iliuzwa, na kupatikana takriban dola za Marekani 1,200 kutoka kwa wanunuzi waliokuwa na hamu ya samaki hao.
Kufungwa kwa eneo la uvuvi wa pweza Munje kumeanza kwa mafanikio makubwa. Jamii ya wavuvi inatarajia kipindi cha pili cha uvuvi kufanyika mwezi Februari.

Picha ya bango: Mvuvi wa pweza, Kassim Ali Siwa, wa Munje, Kenya. Picha na Diana Wanyonyi kwa niaba ya Mongabay.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 24/01/2024