- Shirika la kiimani la kutetea haki katika athari za mabadiliko ya tabianchi, Greenfaith, limedai kuwa ujenzi wa Bomba la Mafuta la Afrika Mashariki (EACOP) litaharibu takriban makaburi 2,000 katika eneo lenye urefu wa kilometa 1,441(maili 895) ambako litapita kutoka Ziwa Albert nchini Uganda hadi bandari ya Tanga iliyopo Tanzania.
- Uchunguzi katika maeneo ambayo bomba litapita umebaini malalamiko mengi kutoka kwa wananchi wakidai kuwa TotalEnergies, kampuni kubwa ya Kifaransa inayohusika na ujenzi huo, wala haiheshimu makaburi ya familia na yale ya ukoo hata pale walipojulishwa maeneo ambapo makaburi yalipo.
- Kwa upande wake, TotalEnergies imesema kuwa taratibu za kubaini na kutambua makaburi na kuyahamisha na kulipa fidia kwa wahusika zimefuata maelekezo na viwango vya kimataifa.
- Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2017, mradi wa ujenzi wa Bomba la Mafuta la Afrika Mashariki (EACOP) umekuwa ukisakamwa kwa kukiuka taratibu na kusababisha athari za kimazingira, kijamii na kuchochea athari za mabadiliko ya tabianchi.
Ripoti ya hivi karibuni illiyochapishwa na shirika la kimataifa linalojumuisha watu wa imani tofauti na linalotetea haki sawa ya kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi, GreenFaith, linadai kuwa Bomba la Mafuta la Afrika Mashariki (EACOP) litaharibu au kunajisi makaburi yapatayo 2,000 katika maeneo litakapopita kutoka Ziwa Albert nchini Uganda hadi bandari ya Tanga iliyopo nchini Tanzania.
Lakini kampuni ya mafuta ya Kifaransa, TotalEnergies, inapinga madai hayo na kusema kwamba inafuata taratibu za kimataifa za kubaini, kutambua na kushughulikia makaburi, na maeneo mengine muhimu ingawa jamii zinazoishi katika njia litakazopita bomba hilo wamelieleza GreenFaith kuwa kampuni hiyo haisikilizi wala kutilia maanani maoni na wasiwasi wao kuhusu utunzaji wa makaburi.
Kuanzia Januari hadi Septemba mwaka huu, GreenFaith walifanya uchunguzi katika wilaya sita nchini Uganda na wilaya tatu nchini Tanzania katika njia yenye urefu wa kilometa 1,441 (maili 895) na kuongea na wakazi wengi ambao ni wenyeji wa maeneo hayo. Katika ripoti yenye kurasa 37, ambayo ilichapisha mwezi Novemmba, shirika hilo linadai kuwa wanaosimamia mradi huo wa bomba la mafuta wanafahamu kuwa mradi huo utaathiri maelfu ya makaburi na sehemu “takatifu” na wametoa majibu yasiyoridhisha au kulipa fidia ndogo kwa waathirika.
“Wenyeji wametueleza kuwa TotalEnergies wamekuwa wakiharibu makaburi ya familia zao au ya ukoo mara kwa mara. Uharibifu huu umekuwa ukiendelea hata baada ya wenyeji kuwatahadharisha TotalEnergies kuhusu makaburi hayo na kutoridhishwa kwao na kinachoendelea,” ripoti hiyo inaeleza.

Kulinganan na mwongozo uliotolewa na Shirikisho la Fedha la Kimataifa (International Finance Corporation (IFC), ambacho ni kitengo cha Benki ya Dunia kinachohudumia sekta binafsi, masuala yote yanayohusu urithi wa mila na utamaduni kama makaburi yanatambulika kwa umuhimu wake kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo, na hivyo yanatakiwa kulindwa ili yasiathirike kwasababu yoyote ile, au familia na jamii ilipwe fidia stahiki endapo yanaathirika, inasema ripoti hiyo.
IFC ni taasisi kubwa ya maendeleo duniani ambayo imejikita katika sekta binafsi katika nchi zinazoendelea. Watekelezaji wa mradi wa EACOP wamesema watazingatia viwango vya utendaji vya IFC vinavyotilia maanani maslahi ya jamii.
Mtu mmoja nchini Tanzania aliwaambia GreenFaith: “Sijaridhika. Yaelekea mchakato mzima wa kutathmini makaburi ni wa kibaguzi. Sijajua nimewakosea vipi wawakilishi wa watekelezaji wa mradi au viongozi wangu wa serikali ya kijiji. Ingekuwa vizuri kama wangesikiliza madai yangu kwani nina wasiwasi kuwa mwisho wa siku wanahamisha mabaki ya miili ya ndugu zangu na kwenda kuyatupa kusikojulikana.”
Mtu mwingine naye alisema: “Ulipofika wakati wa kuhamisha miili, masanduku ya kuzikia waliyoleta TotalEnergies yalikuwa madogo. Ilibidi mwili wa baba yangu ukatwe vipande ili uweze kutosha kwenye sanduku waliloleta.”
Kwasababu ya tuhuma za vitisho na unyanyasaji ambavyo maafisa wa EACOP wanadaiwa kuwafanyia waathirika wa mradi, GreenFaith imehifadhi majina ya watu waliowahoji kwa usalama wao.
“Inaleta kiwewe na hofu kubwa inapoonekana kuwa TotalEnergies, kwa kushirikiana na serikali za Uganda na Tanzania, imewahamisha maelfu ya watu katika njia ambayo bomba la mafuta litajengwa,” Mkurugenzi wa GreenFaith Meryne Warah alisema katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na shirika hilo. “Inapokuwa kwamba hata wafu hawaachwi kupumzika kwa amani, ni kukosa heshima kwa jambo ambalo linagusa imani za Waafrika.”

Kampuni ya mafuta ya Kifaransa yajieleza
Tuhuma nyingi zimeelekezwa kwa kampuni kubwa ya mafuta ya Kifaransa ya TotalEnergies, ambayo inajenga bomba hilo kwa ushirikiano na kampuni za China National Offshore Oil Corporation, Kampuni ya Mafuta ya Uganda na Shrikia la Maendeleo ya Petroli Tanzania.
Baada ya kuulizwa maswali na Mongabay, TotalEnergies ilitoa majibu kwa maandishi ikijihami dhidi ya tuhuma hizo. Licha ya tuhuma zilizotolewa na GreenFaith, kampuni hiyo ilisema kuwa mambo yote yanayohusu bomba hilo yanatekelezwa kwa ubora wa hali ya juu kulingana na viwango vya IFC.
TotalEnergies waliandika: “Mradi umeandaa mpango wa usimamizi wa maeneo yenye umuhimu wa urithi wa kimila na utamaduni. Tumejadiliana na wadau muhimu wakiwemo wenyeji wa maeneo mbalimbali, na kuorodhesha maeneo muhimu ya kihistoria, kitamaduni na kiimani. Tumefanya kila jitihada kuhakikisha kuwa ujenzi wa bomba utakwepa maeneo haya muhimu. Pale ambapo imekuwa vigumu kuyakwepa maeneo hayo, tumechukua tahadhari kupunguza uharibifu au athari nyingine yoyote… pamoja na kuwaarifu wahusika, ambapo tulijadiliana nao ili kuhakikisha kuwa tunaheshimu mila, utamaduni na desturi zao … Kuhusu makaburi maalumu, wanafamilia huyatambua, na tunayaonyesha wazi kwenye ramani zetu ili yasiharibiwe.”
TotalEnergies walieleza pia kuwa wao huwalipa familia husika wanaotakiwa kuhamisha makaburi na kuwapa muda wa kutosha wa kufanya ibada zinazotakiwa kulingana na maombi yao ili kuzika upya miili hiyo.
Majibu waliyotoa kampuni ya mafuta yanawiana na mwenendo wao wa miaka mingi wa kukataa au kukwepa tuhuma dhidi ya ujenzi huo wa bomba la mafuta likiwemo tamko la Bunge la Ulaya lililotolewa mwaka 2022 likipinga ujenzi huo kwa sababu ya haki za binadamu.
Mwanaume mmoja Mkatoliki kutoka Wilaya ya Buliisa kule Uganda alilieleza GreenFaith: “TotalEnergies walikataa gharama ya kuhamisha makaburi ambayo familia yangu tuliandaa, wakatengeneza yao bila kutushirikisha. Kulingana na mila na utaratibu wetu tukitaka kuhamisha makaburi huwa tunakutana na kupanga gharama inayotakiwa. Lakini wao walifanya kila kitu wenyewe.”
Mkurugenzi Mtendaji wa GreenFaith, Fletcher Harper, ambaye yuko New York, aliiambia Mongabay kuwa majibu waliyotoa TotalEnergies hayakumshangaza.
“Sisi tunasimama na ripoti yetu ambayo inapinga kabisa maelezo ya TotalEnergies,” alisema Harper. “Tunalaani kitendo cha kampuni cha kuwadharau wenyeji. Tunalaani kuingilia imani na tunasisitiza kuwa mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta usitishwe.”
Ripoti ya shirika hilo pia imeitaka TotalEnergies kutoa fidia kamili kwa uharibifu wa makaburi na pale ambapo migogoro ya kidini na kitamaduni haikuweza kutatuliwa, kampuni ifuate sheria na taratibu za kimataifa.

Athari kwa mazingira na binadamu
Jitihada za kupinga EACOP zilianza sambamba na mradi ulipoasisiwa mwaka 2017, kwa madai ya kukiuka haki za jamii zilizo katika maeneo ambapo bomba litapita. Madai mengine yaligusia uharibifu wa ardhi, maji na biyonuai, na athari za uzalishaji mamilioni ya mapipa ya mafuta wakati ambapo mabadiliko ya tabianchi yanazidi kushika kasi, huku wito ukitolewa kuacha kutumia nishati ya mafuta duniani kote.
Mnamo mwaka 2021, Mongabay iliripoti kuwa “Iwapo bomba hili litakamilika litasafirisha mafuta mazito kutoka takriban visima 130 vilivyomo ndani ya hifadhi kubwa ya taifa nchini Uganda, ambamo kuna wanyama kama tembo, simba, mamba na zaidi ya aina 400 za ndege. Wahifadhi wanasema kuwa ujenzi huo sio tishio kwa wanyama pori tu, lakini unadidimiza jitihada za kimataifa za kupunguza joto la dunia kwa kuwa kutakuwa na uwekezaji mkubwa kwenye nishati chafu.”
Gharama za ujenzi wa bomba la mafuta zimepanda kutoka dola za Kimarekani bilioni 3.5 hadi bilioni 5.
Mipango inaendelea kana kwamba bomba hili litajengwa, ingawa jopo la makampuni yanayotarajiwa kujenga bomba hilo yana upungufu wa mabilioni ya fedha baada ya taasisi za kifedha, hasa zile za Japan na Marekani, kusita kutoa fedha kutokana na ukosoaji wa mradi kutoka sehemu mbalimbali.
Mratibu wa GreenFaith nchini Ufaransa, Martin Kopp, amekuwa akiratibu upinzani kutoka mashirika ya kiimani dhidi ya mradi huo. Aliiambia Mongabay kuwa nchini Ufaransa kuna watu ambao hawaamini kama kuna mabadiliko ya tabianchi na watu wataendelea kutumia mafuta kama nishati kuu ya usafirishaji kwa miaka mingi ijayo.
“Lakini kwa upande mwingine watu wote wanaoelewa mabadiliko ya tabianchi na athari zake wanaona kuwa mradi wa EACOP na uchimbaji mafuta unaoambatana nao kuwa ukiukwaji wa haki za binadamu, kuchoea athari kubwa za mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira. Ndiyo maana kuna upinzani mkubwa kwa TotalEnergies kutoka kwa makundi mbalimbali wakitumia njia zote za kufikisha ujumbe wa kupinga mradi huo,” alisema Dr Kopp.
Picha ya bango: Mtu ambaye jina lake halikutajwa kutoka Tanzania ambaye ameathiriwa na ujenzi wa bomba la mafuta, Januari 2022. Picha na Thomas Bart.
Justin Catanoso, ambaye mara nyingi huandika katika jarida la Mongabay, ni profesa wa uandishi wa habari huko Wake Forest University, North Carolina nchini Marekani.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 14/11/2023.