- Matumizi ya boma za kuhamishwa, au mazizi, kuweka mifugo salama dhidi uvamizi wa wanyama wanaowinda yameleta manufaa tofauti kwa jamii za wafugaji na wanyamapori katika mbuga ya Maasai Mara ya Kenya.
- Maboma hupunguza hatari ya magonjwa na kuwindwa miongoni mwa mifugo, huku ikiruhusu ufufuzi wa ardhi ya malisho iliyoharibiwa, ambayo inavutia wanyama pori zaidi kwenye eneo hilo.
- Kuongezeka kwa uwepo wa wanyamapori kumesababisha kuimarika kwa utalii wa wanyamapori, wenye thamani ya dola milioni 7.5 kila mwaka katika Hifadhi ya jamii ya Enonkishu yenye ukubwa wa hekta 2,400 (sawa na ekari 6,000).
- Waangalizi wanaonya juu ya madhara yanayoweza kutokea, hata hivyo, ikiwemo pamoja na uhaba wa chakula huku wanajamii wanapoachana na kilimo ili wapate kazi nzuri zaidi ya utalii, na kuongezeka kwa uhasama baina ya binadamu na wanyamapori kadiri idadi ya wanyamapori inavyoongezeka.
ENONKISHU, Kenya — Bernard Leshinga, mfugaji wa jamii ya Kimasai kutoka kusini mwa Kenya, anapenda siku isio na bughdha zozote kuendesha biashara yake ya ufugaji.
Lakini hadi hivi majuzi, Leshinga hakuwa amewazia namna ya kusaidia mifugo yake kushindana kwenye malisho na wanyamapori, au kukaa kando salama dhidi ya wanyama wanaowinda wanyama wengine; wakati wafugaji walio na makazi hapa mara nyingi hujenga boma (mazizi ya kudumu au mabanda) kulinda mifugo yao nyakati za usiku, watu kama yeye ambao hutoka mbali na nyumbani mara nyingi hujitahidi kuzuia uwindaji. Na wakati nyanda za malisho zinaharibiwa na malisho ya wanyama porini kupungua kwa idadi, wanyama wanaokula wenzao katika eneo tata la Maasai Mara nchini Kenya hulenga mifugo mara kwa mara.
Mafanikio kwa wafugaji kama Leshinga yalikuja mwaka wa 2017, wakati maboma ya kuhamishika yalipoanzishwa katika Hifadhi ya Enonkishu. Haya ni maboma yanayoweza kusogezwa, yenye matundu ya waya ambayo wafugaji huhifadhi mifugo yao usiku, salama dhidi ya wanyama wanaowinda wanyama wengine.
Kila baada ya siku 10 wakati wa msimu wa kiangazi, wenyeji wanaowajibikia boma hizo hukusanya nguvu kazi yao ili kuhamisha shehena za maboma hadi kwenye sehemu mpya, kwa kawaida wakiwa na mikokoteni au kubeba vipande kwa mikono. Wakati wa msimu wa mvua, hufanya kazi hii kila baada ya wiki mbili.

“Katika siku za nyuma, kulikuwa na ongezeko la uvamizi wa wanyama wanaowinda mifugo yetu kwa sababu malisho kama nyasi na majani yalikuwa machache kwa idadi, na mazizi ya zamani hayakuweza kuwarudisha nyuma wanyamapori. Maboma ya sasa yaliyoboreshwa yanazuia uvamizi huu,” Leshinga alisema.
Alisema sababu ya kupungua kwa wanyama walao mimea kwenye muongo mmoja uliopita ilikuwa ni kupungua kwa malisho huku kiangazi kinachozidi kuwa kibaya kikiunguza nyasi. Kulingana na shirika la ReliefWeb, ukame mkali uliyakumba maeneo kame na nusu kame ya Kenya kuanzia mwaka 2010-2011, mwaka 2016-2017 na mwaka 2020-2022.
Lakini wanasayansi pia wamehusisha kupungua kwa wanyamapori wenye kwato na vitisho vinavyokabili njia tano za ukanda wa uhamiaji nchini; na mojawapo, njia ya Mara-Loita, imekaribia kutoweka. Nne nyingine, ikiwa ni pamoja na ukanda wa Mara-Serengeti, Greater Amboseli, Manyara-Tarangire na ukanda wa Africa Plains kutoka Hifadhi ya Kitaifa ya Nairobi, pia zinakaribia kutoweka, kulingana na Nicholas Oguge, mkurugenzi wa sera ya mazingira katika Kituo cha Mafunzo ya Juu ya Sheria na Sera ya Mazingira (CASELAP) katika Chuo Kikuu cha Nairobi.
Kuna sababu mbalimbali kuonyesha ni kwa nini kanda za uhamiaji wa wanyamapori zinakabiliwa na shinikizo la kuongezeka, pamoja na mabadiliko ya hali ya anga. Lakini Oguge alisema jambo linalosumbua zaidi ni miradi ya maendeleo ya majengo na upanuzi wa miundombinu, kwani ardhi inahama kutoka kwa jamii hadi umiliki wa mtu binafsi. Huu ni uchunguzi ambao Mongabay ilithibitisha wakati ilipotembelea eneo hilo hivi majuzi.
Kusafiri kutoka Nairobi hadi lango kuu la mashariki la Maasai Mara, ilikuwa rahisi kuona ekari za ardhi ambazo zimezungushiwa uzio zikisubiri kuuzwa ili kuleta maendeleo ya makazi. Mifugo isiyoweza kupita kwenye vizuizi hivi, inalazimika kulishwa kandokando ya barabara.

Bila uzio
Mtindo huu unaigwa kote katika nyanda za juu, hadi barabara inayopenyeza hadi katika mfumo ikolojia wa Mara. Hapa, wenyeji wamekuwa wakiondoa uzio na kurejesha ardhi kwenye mfumo huru wa asili, na kwa sababu bora.
Wakiwa na mazizi yanayoweza kuhamishwa, wenyeji wamegundua kuwa wanaweza kuchanganya sehemu zao za ardhi kuwa hifadhi, kuacha mimea kuongezeka kwa kuhamisha mifugo, na kupata mapato yanayoendelea kutokana na utalii wa wanyamapori, badala ya faida kutokana na mauzo ya mali ambayo huacha familia zikiwa maskini baada ya pesa kutumika
Sio tu kwamba mabanda, ambayo yaanzia uwanja wa tenisi hadi nusu ya uwanja wa soka kwa ukubwa, yanasaidia katika usimamizi wa malisho na ukuaji wa mimea, pia yanalinda mifugo kutokana na uvamizi wa wanyamapori usiku, Leshinga alisema.
Hapa ujanja ni kuendelea kuhama na mazizi na kuyaweka kwenye maeneo yaliyoharibiwa, wakati mifugo hula katika eneo jingine ambalo lina malisho. Wakati wa jioni, wafugaji huleta mifugo wao kupumzika kwa usiku, na kurudia mtindo huo kwa takriban siku nne kabla ya kuhamia eneo lingine, alisema.
“Hata simba hawezi kuingia kwa urahisi ndani ya zizi, kwa sababu linalindwa vyema na uzio wa chuma unaoizunguka,” Leshinga alisema huku akisukuma uzito wake kwenye banda, ambalo halikuyumba.
Sayansi ya uwekaji upya mimea inategemea kinyesi cha mifugo, nguvu zao za kwato, na mvua, kulingana na Daniel Sayialel, afisa wa uhusiano wa jamii kwa takribani hekta 2,400 (ekari 6,000) hifadhi ya Enonkishu. Kinyesi cha mifugo hurutubisha udongo popote pale maboma yanapowekwa kwa muda, na mbegu ambazo hazijameng’enywa ambazo mnyama huyo anaweza kuwa amemeza husambazwa.

Na kwato zao pia hujipenyeza kidogo kwenye uso wa udongo ndani ya zizi, ambazo husaidia mvua kunyesha ardhini, ambapo mbegu zinaweza kuitumia kuota, badala ya kumwaga maji kama tope.
“Ikizaliwa upya tena kutokana na mvua, eneo hilo linaunda mapovu yake yenyewe, ambayo yanaizamisha ardhi kuwa malisho na mimea,” Sayialel alisema, akiongeza kuwa zizi moja linaweza kuhifadhi wanyama wa kufugwa 400 hadi 1,000, kulingana na ukubwa.
Utafiti wa kuzaliwa upya
Wakati boma zinazohamishika zilianza kuonekana hapa kusini mwa Kenya miaka sita iliyopita, Kituo cha Utafiti cha Kapiti na uhifadhi wa wanyamapori cha Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Mifugo (ILRI) chenye umri wa miaka 53, ambacho kinapakana na Hifadhi ya Kitaifa ya Nairobi kuelekea kusini mashariki, kimekuwa kikichunguza ufanisi wa boma zinazohama kwa zaidi ya miaka saba.
Nehemiah Kimengich, meneja wa ranchi ya Kapiti, alisema uanzishwaji wa boma ulikuwa kwa madhumuni hasa ya utafiti, na kwamba wamegundua faida za ziada kwenye mabanda. Uhamisho wa mara kwa mara wa maboma na mifugo kutoka eneo moja hadi jingine – angalau kila baada ya siku 10 wakati wa kiangazi na karibu kila wiki mbili wakati wa msimu wa mvua – pia unaonekana kusaidia kudhibiti kuenea kwa magonjwa ya wanyama.
Makundi ya mifugo yanapotunzwa kwenye zizi la kudumu, ukaribu wao na mrundikano wa samadi huleta hali ambapo vimelea vinavyosababisha magonjwa ya mifugo kama vile homa ya Pwani ya Mashariki vinaweza kuzaliana na kuongezeka.

Faida nyingine ni udhibiti wa spishi za mimea vamizi ambazo huikaba mifumo ya ikolojia: wakati boma la kuhamishwa linaekwa katika sehemu ambayo mimea kama hiyo imetawaliwa, misongamano mikubwa ya wanyama mara nyingi huondoa magugu.
Bado kipengele kingine chanya cha maboma ya kuhama-hama ni kuzuia kuzaliana kati ya wanyamapori wanaokula malisho, kwa kuwavutia kwenye maeneo mapya ya nyasi katika mandhari yote na mbali na mifumo inayodhibitiwa kama Hifadhi ya Kitaifa ya Nairobi, kuwaruhusu kupata wenzi wapya.
“Aina ya malisho ambayo huchopoka kutoka kwenye eneo lililopandwa mbegu hukua haraka, ni tamu na yenye ladha kwa wanyamapori. Hii inavutia wanyamapori kutoka kwa mifumo tofauti ya ikolojia kuhamia katika maeneo haya ya malisho,” Kimengich alisema, akiongeza kuwa mpango wao wa malisho unatenga asilimia 40 ya malisho kwa wanyamapori na asilimia 60 kwa mifugo.

Watalii wanavutiwa pia
Matokeo chanya ya boma za kuhamahama pia yamevutia watu kutoka mbali sana. Katika Enonkishu, mafanikio ya ubunifu wao yamekuza utalii wa ndani na kutengeneza nafasi zaidi ya 2,000 za ajira, kulingana na Jumuiya ya Uhifadhi Wanyamapori ya Maasai Mara (MMWCA).
Utafiti wa mwaka 2021 wa Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID) ulichunguza thamani ya kiuchumi ya mali asili ya Afrika Mashariki na kukadiria mfumo wa Ikolojia wa Mara wa Kenya kuwa na thamani ya takriban dola bilioni 6.5 kwa jamii kila mwaka. Katika jamii ya Leshinga, thamani hii inakadiriwa kuwa takriban dola milioni 7.5 katika mapato ya kila mwaka kutokana na utalii, ambayo yamechochewa na kurejea kwa wanyamapori adimu kama vile “wakubwa watano” (simba, chui, kifaru, tembo, na nyati wa Kiafrika) na mbwa mwitu wa Kiafrika.
Hata hivyo, kuongezeka kwa shughuli za wanyamapori katika Hifadhi ya jamii ya Enonkishu kutokana na mafanikio haya kunasababisha kuongezeka kwa uhasama baina ya binadamu na wanyamapori, kulingana na sajini mkuu Francis Dapash, Afisa Mhifadhi wa wanayamapori anayehudumu mbuga ya Maasai Mara.
Kuwepo kwa wanyama wa familia ya paka wakubwa kama vile simba kumeongeza uvamizi dhidi ya wanyama wa kufugwa wanapokula wakati wa mchana, wakati wanyama wanaokula sana kama tembo wamekuwa wakivamia mazao ya mashamba pembezoni mwa hifadhi, alisema.
“Malisho katika Enonkishu yanapatikana kila msimu katika vipindi vya mwaka mzima, hata wakati wa kiangazi. Haya yanadilika na kuwa tatizo kwa sababu hatuna udhibiti wa kuongezeka kwa idadi ya wanyamapori wanaokuja hapa,” Dapash alisema.

Sababu nyingine ni kwamba wenyeji ndani ya hifadhi wamekuwa wakibadilisha matumizi ya ardhi zao kutoka kwa kilimo cha mazao hadi kwenda kwa uhifadhi wa wanyamapori, kwa sababu utalii wa uhifadhi unawaingizia mapato zaidi, kulingana na shirika la MMWCA.
Wakati uvamizi wa wanyamapori na kiangazi kinachozidi kuwa kibaya zaidi kikisababisha mavuno kidogo, kubadilisha ardhi kuwa matumizi ya uhifadhi kuna faida za kifedha za haraka na za muda mrefu, alisema Daniel Sopia, Afisa mkuu mtendaji wa shirika la MMWCA.
Zaidi ya hekta 4,000 (sawa na ekari 10,000) za ardhi zilikuwa chini ya kilimo cha mazao ya vyakula huko Enonkishu na maeneo jirani ya hifadhi hio, lakini baadhi ya hekta 3,200 (sawa na ekari 8,000) zimebadilishwa kuwa sehemu za uhifadhi baada ya boma zinazohamishika kupelekwa huko, kulingana na wanachama wa shirika lisilo la kiserikali kwenye mahojiano.
Hii inaweza kusababisha kupungua kwa hifadhi ya chakula kwa sababu vyakula vikuu ambavyo vilipatikana kwenye jamii siku za usoni vingeweza kushindwa kufika kwenye sahani ya chakula cha jioni na mazao finyu ya chakula, Million Belay, mratibu wa Alliance for Food Sovereignty in Africa, alionya.
Hata hivyo, kama jamii ya watu katika hifadhi ambao wananufaika kupitia kwa kutumia ardhi yao kuvutia wanyamapori wanaweza kununua chakula kutoka sehemu nyingine, hii inaweza isilete wasiwasi, na kwa usawa, suluhu rahisi ya maboma ya kuhama-hama inaonekana kuwa chanya kwa jamii na uhifadhi.
Picha ya bango: Ng’ombe na pundamilia katika moja ya hifadhi za taifa nchini Kenya. Miongoni mwa sababu za kupungua kwa wanyama wala majani katika muongo uliopita ni kupungua kwa malisho kutokana na vipindi virefu vya ukame vilivyokausha nyasi. Hali hii imewaathiri zaidi wanyama wanaokula nyama na kuwafanya kulenga mifugo.
Ingia hapa kwa taarifa za makala zaidi kama hii, kwa lugha ya Kiingereza, kutoka kwa sehemu zaidi ya Suluhisho za Uhifadhi wa Mongabay.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 06/11/2023.