- Aina sita mpya za vinyonga mbilikimo zatambuliwa katika Milima ya Tao la Mashariki iliyoko Tanzania.
- Hata hivyo misitu iliyoko katika milima hiyo inakabiliwa na shinikizo la shughuli za kibinadamu ambazo zinahatarisha aina mbalimbali za wanyama na mimea inayopatikana katika misitu hiyo.
- Uchunguzi wa hivi karibuni uliotumia setilaiti umegundua kuwa katika wilaya moja wakulima wadogo na wafugaji wameteketeza takriban asilimia 27 za misitu ya milimani kuanzia mwaka 2011 hadi 2017.
- Kwa sasa serikali ya Tanzania inafanya jitihada ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo katika eneo ambalo linaingiliana na Tao la Milima ya Mashariki. Jambo hili linaleta wasiwasi kuwa kutakuwa na uharibifu mkubwa wa bioanuai katika milima hiyo.
Hivi karibuni Michele Menegon akishirikiana na timu ya wanasayansi wa Tanzania na wa kimataifa walitambua aina sita mpya za vinyonga mbilikimo katika Milima ya Tao la Mashariki. Ukubwa wa viyonga hao ni kama kidole gumba cha mkono. Milima hiyo ambayo vilele vyake vimegubikwa na misitu imetengeneza aina ya visiwa vya nchi kavu vyenye urefu wa kilometa 900 (maili 560) kuanzia kaskazini mwa Ziwa Tanganyika hadi Milima ya Taita iliyopo kusini mwa Kenya. Milima ya Tao la Masahriki inaundwa na vitalu 13 vya milima vilivyotenganishwa ambavyo vinahifadhi baiyonuai ya kushangaza. Waweza kulinganisha vitalu hivi vya milima na visiwa maarufu vya Galapagos.
Utambuzi huu unafanya idadi ya vinyonga aina Rhampholeon, au vinyonga mbilikimo kuwa 26 mpaka sasa. Nusu ya vinyonga hao wanaishi katika Milima ya Tao la Mashariki ambako vitalu vyake vya milima vinafanana na viswa vya kibaiolojia. Humo kunapatikana aina mbalimbali za reptalia wadogo wafananao na ndege wadogo aina ya chiriku wanaopatikana katika visiwa vya Galapagos ambao Charles Darwin amewahi kusimulia habari zao.
Hata hivyo ustawi wa misitu hii unatishiwa na wakulima na wafugaji ambao hukata miti ovyo ili kupanua mashamba na kupata malisho. Watafiti wanasema kuwa wengi kati ya vinyonga waliotambuliwa hivi karibuni wamo hatarini kutoweka kutokana na makazi yao kuharibiwa.
Menegon ni muikolojia, mhifadhi na mtafiti ambaye amekuwa akifanya kazi katika Milima ya Tao la Mashriki kwa miaka 30. Mara nyingi akimaliza kazi zake za siku huwa anaibuka na orodha ndefu ya aina mbalimbali za wanyama na mimea ambayo haijulikani kuliko ile ya aina inayojulikana.
Vinyonga wengi mbilikimo ni wa asili ya kitalu fulani cha milima au ni aina ya kipekee na hawapatikani katika kitalu kingine cha milima.


Wakati mwingine unabaki kufanya kazi katika eneo dogo la msitu kwenye mlima mmoja tu, alisema Menegon, akiongea na Mongabay. “Ukienda upande mmoja wa mlima kwenye muinuko fulani unakutana na aina fulani, na ukienda upande mwingine wa mlima, kwa muinuko tofauti, unakutana na aina nyingine,”
Mara baada ya kuchapisha ripoti yake, Menegon aligundua aina nyingine na huenda ni aina mpya kabisa. Ugunduzi huo aliufanya wakati alipotembelea eneo moja la msitu pembezoni mwa kitalu cha Milima ya Nguru iliyoko katika Mkoa wa Morogoro nchini Tanzania. Kinyonga huyo alikuwa mdogo, mwenye miiba miiba na pembe ndefu juu ya macho yake. “Nilipomuona yule kinyonga nikasema huyu yuko tofauti; tuanze kazi upya,” alieleza.
Hata hivyo baiyonuai ya Tao la Milima ya Mashariki haihusu vinyonga tu, kuna mambo mengi. Kuna angalau aina 800 za mimea na angalu aina 96 za wanyama wenye uti wa mgongo, wakiwemo ndege, reptalia, mamalia na amfibia ambao huishi humo tu, na hawapatikani sehemu nyingine.
“Katika eneo la kilometa za mraba 3,500 (maili za mraba1,350) za msitu mnene katika Tao la Milima ya Mashariki, kuna aina ya amfibia ambao idadi yao inalingana na ile inayopatikana katika nchi yote ya Jamhuri ya Kidemomkrasi ya Kongo yenye ukubwa wa kilometa za mraba 2,3 milioni,” alieleza Menegon. “Ni vigumu kuamini.”
Ukataji miti ovyo na uharibifu wa misitu kwa ujumla kwaajili ya kupanua mashamba unatishia ustawi wa hazina hii ya bioanuai ya kipekee. Idadi ya watu nchini Tanzania imeongezeka. Mwaka 2021, kulikuwa na watu zaidi ya milioni 63 wakati mwaka 2002 kulikuwa na takriban watu 35 milioni tu. Ongezeko hili la watu limeongeza pia mahitaji ya ardhi kwaajili ya kilimo cha mazao kama ndizi, mihogo na mahindi.
Iliki ambayo pia hulimwa katika baadhi ya maeneo ya Milima ya Tao la Mashariki inatakiwa sana sokoni. Iliki inataka kivuli hivyo wakulima huacha miti mikubwa lakini uoto wa chini ya miti hiyo huondolewa. Lakini chini ya miti hiyo mikubwa ndiko vinyonga wanakoishi.
“Tumekwisha poteza baadhi ya vinyonga. Msitu ulivyofyekwa, viyonga wakatoweka,” alisema Menegon ambaye pia ni mkurugenzi mwenza wa PAMS Foundation, asasi inayojishughulisha na uhifadhi.

Serikali ya Tanzania imefanya juhudi ya kupunguza hasara inayotokana na upotevu wa baionuai. Katika miaka kati ya 10 na 15 iliyopita, serikali ilipandisha hadhi ya baadhi ya maeneo ya misitu iliyoko katika Milima ya Tao la Mashariki kutoka misitu ya hifadhi na kuwa hifadhi ya asili. Hatua hii inaipa misitu hiyo ulinzi wa kisheria hata kama uko kwenye maandishi tu. Hali halisi inaonyesha kwamba kuna upungufu wa rasilimali kwaajili ya kufanya doria na kulinda msitu.
“Wakulima wanaingia msituni na kulima mashamba makubwa. Inaelekea hakuna namna ya kudhibiti hali hiyo,” alisema Menegon.
Utafiti mwingine uliotumia picha za setilaiti ulibaini kuwa katika Wilaya ya Mvomero pekee, zaidi ya hekta 20,000 (ekari 50,000) au asilimia 27 ya misitu ya milimani zilipotea kabisa au kuharibiwa kati ya mwaka 2001 na 2017. Wilaya hiyo inajumuisha kitalu cha milima ya Nguru ambako ni makazi ya aina mbili ya kinyonga mbilikimo waliotambuliwa hivi karibuni na ina aina nyingine ya vinyonga wenye pembe ambao Menegon aliwaona wiki chache zilizopita.
Mtafiti aliyebaini upotevu na uharibifu huo wa misitu hiyo ni Eliakimu Hamunyela kutoka Chuo Kikuu cha Namibia. Alieleza Mongabay kuwa ukosefu wa fedha umewafanya yeye na kundi lake la watafiti kushindwa kubaini uharibifu wa misitu ulioendela kuanzia mwaka 2017. Alisema, hata hivyo, kuwa uvamizi wa misitu unaofanywa na wakulima unathibitisha udhaifu uliopo katika mbinu zilizopo za kulinda misitu katika maeneo hayo.
Utafiti wake ulibaini pia kuwa angalau asilimia 12 ya uharibifu wa misitu katika Wilaya ya Mvomero ulitokea katika misitu ya hifadhi na huenda ulisababishwa na wafugaji waliopeleka mifugo huko kwaajili ya malisho.
Kitalu cha milima ya Nguru kina sehemu mbili. Kulingana na Kanzidata ya Dunia ya Maeneo ya Hifadhi (World Database on Protected Areas), eneo la kaskazini limekuwa sehemu ya Msitu wa Hifadhi wa Kanga tangu mwaka 1954 na sehemu ya kusini ambayo ni kubwa zaidi linatambuliwa kama Hifadhi ya Asili ya Msitu wa Mkingu (Mkingu Nature Forest Reserve) kuanzia mwaka 2019. Msitu huo pia umetambuliwa katika gazeti la serikali.
Takwimu za setilaiti kutoka jukwaa la ufuatiliaji la kimataifa Global Forest Watch, zinaonyesha kuwa ukataji miti ovyo umeongezeka katika misitu hiyo miwili kuanzia mwanzoni mwa karne hii hasa katika msitu wa Mkingu ambako uharibifu uliongezeka karibu mara saba kati ya mwaka 2017 na 2020. Imeonekana pia kuwa mwaka 2021 uharibifu katika misitu yote miwili ya Mkingu na Kanga ulipungua lakini takwimu za awali za mwaka 2022 na 2023 zinaonyesha kuwa uharibifu uliendelea kwa kasi.
Wafugaji wakiwemo wa Wabarabaig, Wamaasai, Wambulu na Wasukuma wamekuwa wakiingia Wilayani Mvomero kutoka maeneo kame wakitafuta maji na malisho. Utafiti wa hali halisi ilivyo uliofanywa na Hamunyela na wenzake uligundua kuwa makundi ya ng’ombe huharibu miche na machipukizi ya miti. Hii ina maana kuwa ardhi ambayo imeachwa na wakulima haiwezi kurejesha uoto wa asili wala miti.
Watafiti hao wamebaini pia kuwa upanuzi wa mashamba katika misitu Wilayani Mvomero umechochewa japo kwa kiasi kidogo na, Southern Agricultural Growth Corridor of Tanzania (SAGCOT) mradi wa ubia ulioanzishwa baina ya wawekezaji na serikali muongo mmoja uliopita ili kuongeza uzalishaji wa chakula katika maeneo hayo kwa kuwaunganisha wakulima wadogo na masoko ya vyakula.
“Kilimo biashara ambacho kinachochewa na masoko kinaweza kusababisha ongezeko la mashamba ambalo huhitaji kufyeka misitu ili kutosheleza mahitaji ya mazao ya kilimo,” alitanabahisha.

Mtendaji Mkuu wa SAGCOT Center Limited, Godffrey Kirenga alieleza Mongabay kwamba siyo sahihi kusema kwamba mradi huo unachochea upotevu wa baionuai, na kwamba taasisi yake ilikuwa ikihimiza utunzaji wa misitu na mazingira kwa ujumla na hivyo kuhifadhi na kulinda baionuai. Baadhi ya shuguli za taasisi hiyo ni kufanya mikutano na jamii katika eneo hilo kuhusu kuacha uchomaji moto kama njia ya kuandaa mashamba kwa kilimo, hasa katika maeneo ya milima. Kirenga alieleza pia kuwa SAGCOT inahimiza utunzaji wa mazingira ili kujenga mifumo endelevu ya uzalishaji wa chakula.
“Tunatunza na kulinda mazingira, udongo, maji na baionuai kwa ujumla. Viashiria vya ustawi wa mazingira kama vipepeo, ndege, vinyonga na wanyama lazima vitunzwe na kulindwa,” alisema.
Jambo moja liko wazi. Kwa nchi kama Tanzania ambayo ina vivutio vya asili vya ajabu kama Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Ngorongoro, na Mlima Kilimanjaro, ni rahisi kusahau hatari ya ustawi wa Tao la Milima ya Mashariki, misitu yake na utajiri wa bioanuai iliyomo humo.
“Katika nchi nyingine, eneo kama hili lingetunzwa na kulindwa kwa gharama yoyote,” alisema Menegon, ambaye ni mtaalamu wa vinyonga. “Nadhani Tao la Milima ya Mashasriki kwa ujumla wake lingepandishwa hadhi na kutambuliwa zaidi.”
Katika kufikia lengo hilo, yeye na watafiti wenzake waliwapa majina vinyonga mbilikimo waliowagundua hivi karibuni.
Mmoja aliitwa kinyonga mbilikimo Princeeai (Rhampholeon princeeai), kutokana na jina la mwanamuziki na mshairi wa Marekani Prince Ea. Huyu amepata heshima kutokana na juhudi zake za kutangaza hatari inayoyakabili mazingira duniani ikiwemo ukataji ovyo wa misitu. Mwingine ni kinyonga mbilikimo wa Wayne (Rhampholeon waynelotteri) kwa heshma ya Wayne Lotter, mhifadhi kutoka Afrika Kusini na mwanzilishi mwenza wa asasi ya PAMS Foundation ambaye alifanya kazi kubwa kupambana na ujangili nchini Tanzania kabla ya kuuawa jijini Dar es Salaam mwaka 2017.
Tim Davenport ambaye ni mwakilishi katika Afrika Mashariki wa Key Biodiversity Areas Program anakiri kuwa zinahitajika juhudi za ziada ili kutambua Milima ya Tao la Mashairi kama sehemu muhimu ya uhifadhi na utalii.
Hivi karibuni mkurugenzi mstahafu wa Wildlife Conservation Society upande wa Tanzania Davenport ameanza kutangaza utalii katika Tao la Milima ya Mashariki na Nyanda za Juu ambako watalii wanaweza kuona aina mbalimbali za nyani wasiokuwepo sehemu nyingine ukimwenguni.
Ilikuwa katika Nyanda za Juu Kusini ambako yeye na watafiti wenzie walifika na kuutangaza Mlima Rungwe wenye volcano mfu, mlima ambao misitu yake ya kijani ilikuwa imevamiwa na wachoma mkaa na wakataji haramu wa magogo, lakini ulipandishwa hadhi na kuwa hifadhi ya asili, hatua ambayo ilikomesha uharibifu uliokuwepo.

Kinyonga aina ya Rhampholeon nicolai. Picha kwa hisani ya Michele Menegon.
Baada ya uhifadhi ulioshirikisha jamii kwa miaka 13 kuzunguka Mlima Rungwe na Mlima Livingstine ambao sasa ni sehemu ya Hifadhi ya Taifa ya Kitulo, idadi ya nyani aina ya kipekee ambao walikuwa hatarini kutoweka, kipunji (Rungwecebus kipunji), iliongezeka kwa asilimia 65.
“Unahitaji rasilimali na watu sahihi wenye moyo wa kusaidia kulinda na kuhifadhi baadhi ya misitu na milima. Tunahitaji miradi ambayo itajikita zaidi katika kulinda, kuongeza usimamizi wa sheria, kusaidia jamii na kuendesha mambo kisayansi zaidi,” alisema.
Utafiti wa kipunji ulisaidia kuhifadhi, kulinda na kuboresha makazi yao maeneo ya Mlima Rungwe, vivyo hivyo utafiti wa kinyonga mbilikimo na aina nyingine ya wanyama unaweza kuboresha uhifadhi wa misitu ya Tao la Milima ya Mashariki.
“Hawa vinyonga watasaidia kufikia azma hiyo lakini hatuwezi kufanikiwa tukiwategemea wao tu,” alishauri Menegon, na kuongeza kuwa PAMS Foundation imeanza mradi unaowashirikisha wakulima 180 kupanda upya miche ya miti ya asili 300,000 upande wa magharibi mwa Milima ya Nguru.
“Ni fursa ya kipekee kurejesha msitu na uoto wa asili uliopotea miongo na karne kadhaa zilizopita. Hii inaleta matumaini mapya,” alisema.
Picha ya bango: Vinyonga mbilikimo wengi ni wa kipekee na hawapatikani kwingine zaidi ya vitalu vya milima ya Tao la Mashariki (Picha: Menegon)
Nukuu:
Menegon, M., Lyakurwa, J. V., Loader, S. P., & Tolley, K. A. (2022). Cryptic diversity in pygmy chameleons (Chamaeleonidae: Rhampholeon) of the eastern arc mountains of Tanzania, with description of six new species. Acta Herpetologica, 17(2), 85-113. doi:10.36253/a_h-12978
Hamunyela, E., Brandt, P., Shirima, D., Do, H. T., Herold, M., & Roman-Cuesta, R. M. (2020). Space-time detection of deforestation, forest degradation and regeneration in montane forests of eastern Tanzania. International Journal of Applied Earth Observation and Geoinformation, 88, 102063. doi:10.1016/j.jag.2020.102063
Burgess, N., Butynski, T., Cordeiro, N., Doggart, N., Fjeldså, J., Howell, K., … Stuart, S. (2007). The biological importance of the eastern arc mountains of Tanzania and Kenya. Biological Conservation, 134(2), 209-231. doi:10.1016/j.biocon.2006.08.015
Lyimo, E. (2014). An analysis of the stakeholders and drivers of deforestation and forest degradation in the South Nguru landscape. TFCG Technical Paper, 45, 1-59.
Davenport, T. R., Machaga, S. J., Mpunga, N. E., Kimiti, S. P., Mwalwengele, W., Mwaipungu, O., & Makumbule, P. M. (2022). A reassessment of the population size, demography, and status of Tanzania’s endemic Kipunji Rungwecebus kipunji 13 years on: Demonstrating conservation success. International Journal of Primatology, 43(2), 317-338. doi:10.1007/s10764-022-00281-3
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 03/03/2023